Dec 19, 2012

Urasimishaji sekta ya burudani: TRA inapojitwisha zigo isilolifanyia utafiti kwa lengo la kuongeza pato!


Wasanii wakifuatilia semina ya TRA kwenye ukumbi wa maonesho wa Makumbusho ya Taifa, Jumanne wiki hii

Pia nilikuwepo kwenye semina hiyo, hapa nipo na mdau

NIMEKUWA nikisisitiza kuwa hakuna 'excuse' yoyote kwa wasanii katika kukuza pato lao, kuondokana na umaskini na hata kushindana kimataifa kama hawataingizwa kwenye mfumo rasmi ambao utawafanya watambulike ndani na nje ya nchi ili kujenga mazingira ya wao kuweza kukopesheka, kupata fursa za kikazi na kukuza kazi wanazozifanya. Katika mataifa mengine wasanii wako rasmi na wameweza kuvuma na kupaa kiuchumi.

Lakini pia nimekuwa nikitoa wito kwa serikali kutumia fursa ya kuirasimisha tasnia ya burudani hususani filamu kwa kutuanzishia chombo cha kusaidia maendeleo ya miradi kama sehemu muhimu ya kuifanya sekta hii ifikie tunapopataka, na ni msingi muhimu ambapo mkakati wowote wa utengenezaji wa filamu unapaswa kujengwa.

Dec 12, 2012

Kurasmisha sekta ya filamu/muziki sawa lakini kwa hili la stempu tunakurupuka


Afisa Utafiti Mwandamizi wa TRA, Ephraim Mdee, akielezea
kuhusu stempu maalum zitakazoanza kutumia mwakani

BADO naikumbuka hotuba ya Waziri wa Fedha na Uchumi, William Mgimwa, aliyoitoa katika kikao cha bunge la bajeti kwa mwaka 2012/13, pale aliposema: “Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho katika Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, SURA 147 kama ifuatavyo:-
“Mheshimiwa Spika, kumekuwa na kilio cha muda mrefu cha wasanii kudurufiwa kazi zao za sanaa na kukosa maslahi kwa kazi wanazofanya. Ili kutatua tatizo hili, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato itaanza kurasimisha biashara ya bidhaa za muziki na filamu kwa nia ya kuhakikisha kwamba uasili wake unatambulika na hivyo kuzuia vitendo vya kudurufu kazi za sanaa hali ambayo inadumaza ukuaji wa sanaa na vipaji hapa nchini.

Nov 27, 2012

Ni wiki ya majonzi kwa wasanii na wadau wa filamu nchini


 Mlopelo enzi za uhai wake

Wiki iliyopita ilishuhudia msanii aliyepata umaarufu mkubwa enzi za Kaole ya ITV, maaruf kwa jina la Mlopelo aliyefariki dunia mchana wa Alhamisi kwenye hospitali ya Temeke, jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa msemaji wa familia aliyejitambulisha kwa jina moja la Azizi aliyesema kwamba katika maisha yake yote, Mlopelo alikuwa anasumbuliwa na maumivu ya mwili yaliyokuwa yakitulia na kuibuka tena hadi umauti ulipomfika.

Oct 31, 2012

Tujifunze kutoka Sekta ya filamu ya Afrika Kusini

 Hii ni sehemu ya sinema ya Blood Diamond 
iliyotengenezwa Afrika Kusini

TASNIA ya filamu nchini haiwezi kukua kama tutaishia kusema bila kutekeleza tunayoyasema huku kukiwa na mambo mengi yanayoirudisha nyuma. Nimekuwa nikisisitiza kuhusu uanzishwaji wa chombo maalum kitakachosimamia utoaji wa mafunzo ya weledi kwa watengenezaji filamu kiwe kipaumbele cha kwanza.

Ni muda mchache umebakia kufika tarehe 1 Januari, 2913 ambapo ule mpango wa Serikali kama ulivyoainishwa na Waziri wa Fedha, William Mgimwa, kuhusu Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, Sura 147, ambapo Mamlaka ya Mapato Tanzania itaanza kuweka stampu kwenye bidhaa za sanaa ili uuzaji wa kazi hizo uwe rasmi na kuwawezesha wasanii kupata kipato stahili kutokana na kazi zao.

Ni katika kipindi hicho Serikali itaanza kurasimisha biashara ya muziki na filamu kwa nia ya kuhakikisha kwamba uasili wake unatambulika na hivyo kuzuia vitendo vya kurudufu kazi za sanaa (piracy of artists work) hali ambayo inadumaza ukuaji wa sanaa na vipaji hapa nchini.

Narudia tena, kama kweli tumedhamiria kuiokoa tasnia hii na wasanii, tunapaswa kuelekeza nguvu nyingi katika suala la utoaji wa mafunzo kwa wasanii na watengeneza filamu. Serikali inapaswa kwanza kutafuta gharama za mafunzo katika kuutambua mchango wa sekta ya filamu kabla ya mambo mengine yote.

Pili, iangalie uwezekano wa kuanzisha chombo kitakachokuwa na uwezo wa kuzitangaza filamu zetu kitakachoitwa, ambacho kitakuwa na idara tano: ya utoaji wa taarifa za upatikanaji wa pesa (funding information) na kutoa fursa kwa watengeneza sinema, ya kuandaa takwimu za kina na kutoa fursa ya kuzitangaza kazi zetu katika masoko mengine ya Afrika, na duniani na hivyo kuongeza uwezekano wa kuuza kazi zetu kimataifa na kuigiza pesa za kigeni.

Nyingine ni idara itakayowalazimisha wadau katika sekta ya filamu kupata mafunzo ya weledi (professionalism), itakayosimamia mapato (revenue generation) yatokanayo na filamu, na itakayosimamia kwa ukamilifu sheria za uharamia/wizi (piracy) wa kazi za sanaa na hivyo kuwafanya watengenezaji wa kazi hizi kutokuwa na hofu ya kupoteza mapato (economic reward) yatokanayo na kazi zao.

Ili kufanikisha haya tunapaswa kujifunza kutoka sekta ya filamu ya Afrika Kusini ambayo inakua na kuzidisha ushindani katika anga za kimataifa. Watengenezaji wa filamu wa nchi hiyo wanatumia fursa mbalimbali zilizopo ambazo hazitofautiani sana na hapa kwetu.

Sekta hiyo imeweza kuwa na hazina ya kujivunia ambayo ni filamu ya ‘Tsotsi’ iliyoshinda tuzo ya Academy (Oscar) katika kipengele cha filamu bora za lugha ya kigeni mwaka 2006. Filamu nyingine zilizofanya vizuri kimataifa ni ‘Yesterday’ iliyoshiriki tuzo za Oscar na imewahi kushinda katika tuzo mbalimbali za kimataifa, na ‘U Carmen E Khayalitsha’, iliyoshinda tuzo ya Golden Bear mwaka 2005 katika Tamasha la Filamu la Berlin.

Hivi sasa sinema nyingi zenye mafanikio makubwa za kimataifa zimekuwa zikipigwa nchini humo, ikiwa ni pamoja na ‘Blood Diamond’ iliyomshirikisha Leonardo DiCaprio na ‘Lord of War’, iliyomshirikisha Nicholas Cage akicheza kama muuza silaha duniani, Lord of War imesaidia kutangaza maeneo tajiri nchini Afrika Kusini - huku eneo la Cape Town likionekana kama maeneo tofauti 57 yaliyofanywa kuonekana kama meneo katika Mashariki ya Kati, Afghanistan, Bolivia, Sierra Leone na kwingineko.

Afrika Kusini imetambua kuwa sekta ya filamu ni sekta yenye nguvu na inayochangia kwa kiwango kikubwa ukuaji wa uchumi. Ingawa mchango wa Afrika Kusini kwa pato kimataifa unasimama katika asilimia 0.4 tu, sekta ya filamu kwa ndani ya Afrika Kusini inazidi kupata nguvu wakati wote.

Mwaka 1995, wakati nchi hiyo ilipoanza kutumika kama eneo muhimu kwa ajili ya uzalishaji wa filamu na televisheni, sekta hiyo ilitoa ajira nchini kote kwa watu 4 000. Imepanda hadi kufikia watu wapatao 30,000, pamoja na ajira zaidi - na mapato - vikitengenezwa katika filamu - ikihusisha usafiri, malazi na chakula.

Kwa mujibu wa Idara ya Biashara na Viwanda, sekta ya burudani nchini Afrika Kusini ina thamani ya karibu Randi bilioni 7.4, huku filamu na televisheni zikichangia zaidi ya Randi bilioni 5.8 katika shughuli za kiuchumi kila mwaka. Na kulingana na matokeo ya utafiti wa tathmini ya kiuchumi ya hivi karibuni uliosimamiwa na Tume ya Filamu ya Cape, sekta hiyo ina mapato ya moja kwa moja kila mwaka ya zaidi ya Randi bilioni 2.65 na huchangia mapato ya moja kwa moja kila mwaka ya zaidi ya Randi bilioni 3.5 ya pato la taifa la nchi hiyo (GDP).

Faida za ukuaji haraka wa sekta ya filamu ziko wazi, hasa linapokuja suala la kuingiza fedha za kigeni. Ushiriki katika uzalishaji na matokeo ya makampuni ya kimataifa katika uwekezaji wa moja kwa moja wa mamilioni ya randi katika uchumi.

Afrika Kusini imetiliana saini mikataba ya ushirikiano katika uzalishaji filamu wa pamoja na nchi nne: Canada, Italia, Ujerumani na Uingereza. Hii inamaanisha kwamba ushirikiano katika uzalishaji filamu wowote rasmi unachukuliwa kama uzalishaji wa kitaifa kwa kila nchi mwenza iliyohusika katika uzalishaji, hufanya hivyo kwa faida au mipango ya kwa msaada wa kila nchi inayohusika. Afrika Kusini pia ina mkataba wa makubaliano kuhusiana na filamu na nchi ya India.

Serikali ya Afrika Kusini imekuwa ikisisitiza umuhimu wa filamu katika kujenga urithi wa nchi hiyo kwa kuwasimulia watu hadithi zao wenyewe, na imejiweka katika “kuwezesha udhibiti” kwa kuhimiza uzalishaji wa bidhaa za ndani. Vyombo vya utangazaji vya Afrika Kusini vimekusudia kufikia lengo la kutoa kipaumbele kwa kazi huru za ndani, ambazo zimesababisha kuongezeka kwa mahitaji ya vipindi vya ndani. Zaidi ya tamthilia saba zinazorushwa kila siku Afrika Kusini zinazalishwa nchini Afrika Kusini.

"Ni maadili muhimu ya taifa ya kujenga majukwaa ya Waafrika Kusini wa kawaida kuwa na uwezo wa kubeba ushawishi katika maelezo ya picha zao wenyewe," anasema Eddie Mbalo, mtendaji mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Filamu na Video (NFVF). "Kwa njia hii, kama sekta, tunaweza kuchangia kuendeleza maadili yetu ya kidemokrasia na kuleta mafanikio."

Serikali, kupitia Taasisi ya Taifa ya Filamu na Video (NFVF), Shirika la Maendeleo ya Viwanda na Idara ya Biashara na Viwanda, ni mwekezaji mkuu katika sekta ya filamu. Taasisi ya Taifa ya Filamu na Video husaidia katika upatikanaji wa fedha katika tasnia, kupromoti maendeleo ya watazamaji wa filamu na televisheni wa Afrika Kusini, kuendeleza vipaji na ujuzi katika nchi - kwa msisitizo maalum kwa makundi maalum - na kuwasaidia watengeneza filamu kuwakilisha na kuuza kazi zao kimataifa.

NFVF hutoa fedha kwa ajili ya uzalishaji wa filamu na makala (documentaries) kwa njia ya mikopo au ruzuku. Husaidia makampuni ya uzalishaji yanayomilikiwa na Waafrika Kusini, na hutoa kipaumbele kwa miradi au mashirika yanayoweka umuhimu wa kitaifa na mapendekezo ambayo yanasisitiza kazi za ndani na ambayo yana uwezeshaji au mafunzo.

Pia inagharimia fedha za elimu na mafunzo kwa njia ya masomo mbalimbali; kutoa tuzo za maendeleo; na misaada ya maombi ya fedha kwa ajili ya uuzaji na usambazaji, inaruhusu wazalishaji filamu wa kujitegemea na wasambazaji upatikanaji wa maeneo ya kuoneshea filamu na uzinduzi wa filamu. Mnamo Machi 2007, NFVF ilitoa kiasi cha Randi milioni 26 katika ruzuku.

Taasisi ya maendeleo ya fedha inayomilikiwa na serikali, Shirika la Maendeleo ya Viwanda (IDC) imekusudia kujenga sekta endelevu ya filamu ambayo ujuzi utasambaa kwa watu kutoka makundi yaliyokuwa chini ya ubaguzi wa rangi na "kazi za ndani" za filamu zinatengenezwa na kuangaliwa na Waafrika Kusini.

Kituo cha utoaji fedha cha Mkakati wa Biashara ya Filamu na Habari cha IDC, mradi wa utangazaji na uhariri. Msaada ya fedha kwa kawaida hutolewa katika mfumo wa mkopo. Ushiriki wake wa chini ni Randi million 1 na si zaidi ya asilimia 49 ya mradi. Mnamo Juni, 2008, IDC imewekeza zaidi ya Randi milioni 500 na kufadhili filamu zaidi ya 30 nchini humo.

Idara ya Biashara na Viwanda (DTI) inatoa motisha maalum katika sekta ili kuhamasisha kazi za ndani pamoja na kuvutia uzalishaji wa kimataifa. DTI imetangaza marekebisho ya motisha za uzalishaji filamu na vipindi vya televisheni mnamo Machi 2008, ikiondoa kizingiti na kufungua mlango kwa ajili ya filamu za bajeti ndogo kutoka kwa watengeneza filamu wanaoibukia.

Kwa nini na sisi tusifikirie kufuata njia waliyoipita Afrika Kusini kama kweli tumedhamiria kuinua sekta ya filamu? Ni wakati sasa tuache blah blah na tujikite katika kutekeleza tunayoyahubiri.

Alamsiki.

Oct 24, 2012

Tunahitaji mabadiliko ya kweli na si blah blah


Watanzania wana mapenzi na sinema au michezo ya TV 
kama inavyoonekana kwenye picha hii

NI Jumapili tulivu inayoambatana na mvua ya rasharasha. Watu kadhaa wamejazana kwenye chumba kimoja katika nyumba moja wakiangalia filamu ya kusisimua ya Kitanzania. Tukio (scene) katika filamu hiyo linaanzia pale sebuleni. Ni tukio ambalo linaonekana kuvutia kiasi; linaikamata dunia ya wapenda sinema na kuwafanya watazamaji hawa waamini kuwa wanachokiona ni cha kweli.

Oct 17, 2012

Wasanii, tumieni Jukwaa la Sanaa kutatua matatizo yenu


Katibu Mtendaji wa Basata, Ghonche Materego, akisisitiza
jambo kwenye moja ya midahalo ya Jukwaa la Sanaa

NI ajabu, wasanii kulia kilio cha kuilalamikia Serikali kuwa haisaidii juhudi za wasanii katika masoko na usambazaji kwa ajili ya filamu ambazo ni kwa maslahi kwa watazamaji wa Tanzania, kilio cha kuibiwa kazi za sanaa ingawa kuna uwezekano mkubwa wanaolia kutojua wanaibiwaje kazi zao, lakini wanakwepa majukwaa ya upashanaji habari ambayo yangetumika kufikisha kilio chao na kwenda kusemea pembeni.

Hili ni jambo la ajabu sana! Ni kwewli mfumo wa usambazaji ni mbovu, lakini wasanii wanadharau majukwaa muhimu ya habari na hata vyama na mashirikisho yao wakisahau kuwa umoja ni nguvu. Ikumbukwe kuwa utengenezaji sinema ni jambo linalohitaji sana mgawanyo wa kazi. Kuna waongozaji, waigizaji, waandishi wa miswaada na kadhalika, huku msingi mkuu wa sinema yoyote ukiwa ni mwongozo (script).

Oct 10, 2012

Mtalalamika na kuponda kazi zetu hadi lini?


Cover ya filamu ya handsome wa Kijiji

WIMBI la wanaojiita wakosoaji wa filamu nchini limeibuka kiwa kasi ya ajabu, wengi wamecharuka kuandika maoni na ujumbe mbalimbali kupitia mitandao ya kijamii wakiponda sinema za Kitanzania kila kukicha pasipo hata kutoa ufumbuzi wa nini kifanyike ili kuboresha kazi zetu.

Mojawapo ya ujumbe maaruf unaotumika kuponda sinema za Kibongo katika mitandao kama facebook, Jamii Forums na twitter ni huu:

Oct 9, 2012

Nafasi muhimu kwa Watanzania kujitangaza kupitia Tuzo za Filamu Afrika (AMVCA)


Meneja Uhusiano wa Multichoice Tanzania, Barbara Kambogi, akizungumza katika semina fupi ya wadau wa Tasnia ya Filamu nchini pamoja na waandishi wa habari

Mashindano ya Tuzo za Filamu Afrika (AMVCA) yatakayofanyika jijini Lagos, Nigeria Machi 9 mwakani na kushirikisha wasanii na watengenezaji wa filamu barani Afrika yalizinduliwa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam katika hafla iliyoshirikisha makundi mengi ya filamu nchini.

Hafla hii imekuja kufuatia matukio mengine mawili yaliyofanyika mjini Lagos na Nairobi, ambapo AfricaMagic na Multichoice Africa walitangaza mpango wao mpya unaojulikana kama ‘Tuzo za Chaguo la Watazamaji wa AfricaMagic’.

Oct 8, 2012

Filamu ya Chungu ni somo kwa waandaaji filamu nchini

Dk. Vicensia Shule, mtayarishaji wa filamu ya Chungu

Filamu ya Kitanzania iliyoandaliwa na Mtanzania na kuongozwa na Mtanzania mwaka huu imeibuka na tuzo ya filamu bora Tanzania katika tuzo zilizotolewa na waandaaji wa tamasha la 15 la maonesho ya Kimataifa ya Filamu kwa Nchi za Majahazi (ZIFF).

Filamu hiyo ya Chungu iliibuka kidedea katika tuzo hizo baada ya kufanikiwa kuwa filamu bora huku pia ikitoa mwigizaji bora wa Tanzania, Richard Mshanga, maarufu kama Masinde ambaye katika filamu hiyo alitumia jina la She Mdoe.

Oct 3, 2012

Baraza la Sanaa la Taifa latoa tamko zito


Katibu Mtendaji wa Basata, Ghonche Materego

Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) limewaagiza viongozi wa Mashirikisho ya sanaa hapa nchini kufuatilia kwa karibu matukio ya ukiukwaji wa maadili yanayoendelea katika Sanaa hivi sasa na kuchukua hatua kwa wanaobainika kufanya hivyo.  

Mbali na Basata kuwakemea vikali wasanii wanaotumia majukwaa kwa kuidhalilisha Sanaa wao wenyewe na Watazamaji pia limeyataka mashirikisho kushirikiana na vyama vyao kuwaita wale wote watakaohusika na uvunjwaji wa maadili ili kuwakanya katika hatua ya kwanza na kama wasipoacha tabia hizo Baraza litawafungia kujishughulisha na kazi ya Sanaa hapa nchini.

Skendo ya picha chafu, hivi Watanzania tumeingiwa nini?


Wasanii wa filamu Aunt Ezekiel na Wema Sepetu wakiwa jukwaani

INASHANGAZA sana! Katika kipindi cha miaka michache tu iliyopita taratibu kumeingia mdudu mbaya sana katika tasnia nzima ya burudani, huku tasnia ya filamu ikionekana kuongoza. Tumekuwa tukishuhudia jinsi wasanii wa kike wanavyokuwa nusu watupu kitu kinachosemwa eti ndiyo maendeleo (kupiga hatua), na pengine inabainishwa kuwa hiyo ndiyo dalili ya kuwepo kwa mafanikio katika tasnia hii.

Sep 14, 2012

Tanzania na nchi za SADC bado zina nafasi ya kufanya vizuri


Wakati wa upigaji wa sinema ya Tsotsi, nje ya jiji la Johannesburg

NCHI za kusini mwa Afrika zina nafasi kubwa ya kutoa mchango katika tasnia ya filamu na televisheni duniani. Kumekuwepo makubaliano miongoni mwa wadau na wachunguzi wa tasnia hii, kwamba, utajiri uliopo wa ubunifu miongoni mwa vijana na hadithi zilizopo katika ukanda huu vitumike vyema. Hata hivyo, pia wote wanakubaliana kwamba tasnia ya filamu katika nchi hizi bado iko chini sana na, katika hali halisi, inazidi kushuka.

Utafiti unaonesha kuwa tasnia ya filamu ya nchi za SADC ni ndogo na haijapiga hatua, ingawa inaonekana kutoa fursa nyingi katika kuendeleza miundombinu na hadithi zetu. Makampuni mengi katika sekta hii ni madogo madogo na yanayoonekana kuchangia katika ajira na ukuaji wa uchumi.

Aug 29, 2012

Kama inataka kuboresha filamu, Serikali ituondolee kwanza huu mkanganyiko

Katibu Mtendaji wa Bodi ya Ukaguzi wa Filamu, Joyce Fisoo

Katibu Mtendaji wa Basata, Ghonche Materego

WIKI iliyopita niliandika makala kuhusu umoja mpya wa wasanii, watayarishaji na wadau wa filamu ulioanzishwa hivi karibuni kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Leaders Club na kuweka historia mpya kwa kuifanya tasnia ya filamu kuzaliwa upya kwa kuwa na kundi moja lenye nguvu na uhamasishaji katika kutafuta maendeleo na pia kupambana na uharamia ambao umekuwa ukiwarudisha nyuma wasanii na kuwanufaisha wachache bila ya wao kutokwa jasho hata kidogo.

Aug 22, 2012

Umoja huu mpya wa wasanii usiishie kwenye kupambana na uharamia tu, uende mbali zaidi

TAFF mpya

KAMA tukiamua kuangalia sekta iliyosheheni utajiri mkubwa lakini inayoongoza kwa wadau wake kuwa fukara (imefukarishwa makusudi na watu wachache) na inazongwa na matatizo makubwa, basi sekta ya filamu itashika namba moja. Tathmini nyingi zilizofanyika na zinazoendelea kufanyika zinabaini kuwa chanzo kikuu cha matatizo haya ni kutoeleweka kwa dhana nzima ya biashara ya burudani hususan filamu, kutothaminiwa kwa filamu, kutokupewa kipaumbele na watunga sera katika mipango ya maendeleo ya nchi yetu, na mgawanyiko miongoni mwa wadau wa tasnia hii.

Jul 18, 2012

Tasnia ya filamu Tanzania: Tumetokea wapi na tunaelekea wapi?

 Jacklin Wolper akiwa na tuzo yake

KATIKA wasanii mastaa ambao wangepaswa kuishi maisha mazuri nchini kwa sasa, ni wale wa filamu ndio wangepaswa kuwa wanashikilia chati za juu kutokana na jinsi kazi zao zinavyotengeneza fedha nyingi. Kwa mujibu wa takwimu, kazi za wasanii hao zimekuwa zikiingiza fedha nyingi katika miaka ya karibuni tofauti na ilivyokuwa awali, lakini masilahi hayo hutofautiana kwani wapo baadhi ambao hawashikiki.

Wasanii wa filamu wamejijengea majina maakubwa kwenye jamii ya wapenzi wa filamu kufikia kiwango ambacho bila wao kazi hazinunuliki madukani na baadhi ya waandaaji wa filamu hizi wamekuwa wakieleza waziwazi kuwa wengine hata kutokea sura zao tu kwenye sinema ni biashara tosha hata kama wameigiza upuuzi!

Jul 4, 2012

Tupige vita matumizi ya lugha za kigeni kwenye filamu zetu

 Sinema nyingi za Tanzania zimeingia kwenye mkumbo wa kutumia majina ya kigeni

KIPINDI fulani niliwahi kuandika kuhusu suala la mila na utamaduni wa Mtanzania ambapo kwa kiasi kikubwa lilikuwa likinitatiza sana. Nilikuwa nikifikiria sana; tunaposema utamaduni na mila za Watanzania hasa tunamaanisha nini kwa Tanzania yenye zaidi ya makabila 120 ambayo kila moja lina mila na utamaduni wake? Huu utamaduni na mila za Watanzania ni upi hasa?

Haya ni maswali yaliyonitesa kila mara nilipokuwa nikiufikiria utamaduni wa Mtanzania. Lakini baada ya kufanya utafiti niligundua kuwa, neno “utamaduni” linatumika kimsingi katika njia tatu zifuatazo:

Jul 2, 2012

Wasanii maarufu wamepamba tamasha la filamu Tanga

Umati wa watu waliohudhuria tamasha la filamu jijini Tanga

Sehemu ya wasanii nyota katika tamasha hilo

Nyota  mbalimbali wa filamu nchini, akiwemo Wema Sepetu, Jacqueline Wolper, Irene Uwoya, Jacob Steven 'JB' na Vicent Kigosi 'Ray' kwa mara ya kwanza wamepanda kwenye jukwaa moja la tamasha la filamu linalofanyika jijini Tanga lililoanza Jumamosi hadi Julai 6 mwaka huu.

Katika tamasha hilo kumekuwa na burudani mbalimbali kutoka kwa wasanii wa Tanga wanaoimba ngoma za asili kama baikoko, mdumange na msanga.

Jun 20, 2012

Dk. Mgimwa, hili la stampu za TRA na kuirasimisha tasnia ya filamu ni sawa, lakini…

 Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa

“MHESHIMIWA Spika, napendekeza kufanya marekebisho katika Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, SURA 147 kama ifuatavyo:-

“Mheshimiwa Spika, kumekuwa na kilio cha muda mrefu cha wasanii kudurufiwa kazi zao za sanaa na kukosa maslahi kwa kazi wanazofanya. Ili kutatua tatizo hili, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato itaanza kurasimisha biashara ya bidhaa za muziki na filamu kwa nia ya kuhakikisha kwamba uasili wake unatambulika na hivyo kuzuia vitendo vya kudurufu kazi za sanaa (piracy of artists work) hali ambayo inadumaza ukuaji wa sanaa na vipaji hapa nchini.

Gaba Arts Centre na Basata watoa somo kwa wasanii wa filamu


Mkurugenzi wa asasi ya Gaba Arts Centre, James Gayo, akisisitiza jambo wakati akitoa mafunzo kwa wasanii wa filamu juu ya Stadi za Uandishi wa Miswada ya Sinema (Script) kwenye Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila wiki makao ya Baraza la Sanaa la Taifa (Basata)

Asasi ya Gaba Arts Centre na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) Jumatatu ya wiki hii 18, Juni 2012, saa 4 kamili kwenye jukwaa la sanaa waliendesha semina fupi kwa Wadau/wasanii wa filamu ili kuwajengea weledi katika eneo la uandishi bora wa miswada ya sinema (scriptwriting).

Warsha hiyo ya saa mbili ilihusu zaidi Stadi za uandishi wa miswada ya Sinema (Script writing skills), baadhi ya mambo yaliyojadiliwa ni:

Jun 17, 2012

Tamasha la filamu la wazi kufanyika Tanga Juni 2012


Tamasha kubwa la filamu la wazi linatarajiwa kuanza tarehe 30 mwezi huu, tamasha hilo linajulikana kwa jina la Grand Malt Tanzania Open Film Festival (TOFF) na litafanyika jijini Tanga kwa mara ya nne katika viwanja vya Tangamano, ambapo litadumu kwa muda wa siku saba, na kwa kila siku zitaonyeshwa filamu tatu.

Mkurugenzi wa kampuni ya Sofia Production ya Jijini Dar es Salaam, Mussa Kisoki, amesema kuwa kila kitu kimekamilika kwa ajili ya tamasha hilo ambalo linafanyika kwa mwaka wa nne toka kuasisiwa kwake.

Jun 6, 2012

Filamu za Nigeria zinapotumika kama kipimo cha filamu zetu!


Desmond Elliot, muigizaji wa Nollywood ambaye alikuwa 
akiigwa na Steven Kanumba katika uigizaji wake

Marehemu Steven Kanumba

SEKTA ya filamu Tanzania kwa sasa inajulikana duniani licha ya matatizo yake, licha ya mtayarishaji wa filamu wa Tanzania kuendelea kuishi maisha ya chini yasiyo tofauti na mtu mwingine wa kawaida! Sekta ya filamu Tanzania inakua, lakini hali halisi ya soko la filamu nchini inabana sana uwezekano wa kuibuka kwa wasanii, watayarishaji au waongozaji wapya...

Sidhani kama kuna mtu atakayebisha kuwa filamu za kibongo ‘hazitesi’ katika ukanda wa Afrika Mashariki na maeneo ya Maziwa Makuu. Filamu hizi zimesaidia kwa kiwango fulani kuitangaza nchi hii, kuwatangaza wasanii wa nchi hii, lakini vipi kuhusu maisha ya wasanii hawa? Je, wanapata stahili yao na wanaishi kwa kutegemea filamu pekee?

Jun 4, 2012

Wasanii Bongo Movie na madai ya ukahaba, kupiga picha chafu




Ni muda mrefu imekuwa ikisemwa kuwa wasanii wanaoendesha maisha yao kwa ‘kuuza nyago’ kwenye filamu za Kibongo ni watu wanaojiuza, kufanya ufuska na kupiga picha za utupu, ambapo imeshawahi kutolea orodha ndefu ya wasanii hao, huku wengine wakiondoka nchini na kwenda kufanya ufuska huo nje ya Tanzania.


Madai ya kufanya ufuska yaliwahi kuthibitishwa na msanii wa filamu Bongo, Coletha Raymond ‘Koleta" aliyesema kuwa “Kiukweli sanaa inatufanya wasanii wa kike tuingie kwenye vitendo vya umalaya. Sanaa ya Bongo ni vigumu sana kutoka, hailipi kabisa... yaani inatakiwa mtu ufanye kazi nyingine tofauti ndiyo uweze kufanikiwa. Wasanii unaowaona wamefanikiwa si kwa filamu pekee, wana mambo mengine,” alisema na kuongeza:

May 30, 2012

Ubora ndiyo suluhisho kwa kazi zetu kung’ara kimataifa


Filamu ya Senior Bachelor iliyopata tuzo katika
tamasha la filamu la Zanzibar (ZIFF) kupitia
kipengele maalum cha filamu za Tanzania.

Filamu ya Fake Pregnant

CHANGAMOTO kubwa ambayo imekuwa midomoni mwa wengi katika soko la filamu za Tanzania na hata Afrika kwa ujumla ni ile ya kuzalisha sinema zisizo na ubora unaoridhisha. Changamoto hii ambayo ni sehemu ya mambo ambayo yameonekana kuwa magumu kutatuliwa (crux) na ndiyo mjadala wangu wa leo, ni suala ambalo tuko nalo kwa muda mrefu sasa tangu sekta hii ya filamu nchini (Bongo movies) iwepo. 

Katika hatua hii, ni muhimu kutambua kuwa nakusudia kuelezea kwa kiasi kikubwa kutokana na mtazamo wa wangu kuhusu sekta ya filamu ya Tanzania, ambalo ndilo soko la filamu ninalolijua vizuri na nililolifanyia utafiti wa kutosha.

May 24, 2012

Soko huria na filamu za Bongo


Men's Day Out

Aching Heart

Glamour

Uchumi wa soko huria Bongo karibuni umechangia kukua kwa sinema  za Kiswahili. Ukipita mitaani Bongo unakutana na filamu kila kona. Si kama miaka ileeee… tukililia sinema hatuzioni… Imekuwa kama mchezo  bila refa, mkutano bila mwenyekiti, darasa bila mwalimu, nyumba bila mzazi…

Wafanyabiashara wanaahidi milioni kumi hadi ishirini kwa sinema; watoaji wanalipua; waigizaji hawalipwi vizuri; utengenezaji sinema unafanywa haraka haraka.  Sinema zinatolewa ndani ya mwezi mmoja. Haraka haraka…

May 22, 2012

Kwanini tuelendelee kuwa sekta ya 'kuganga njaa' tu?




Picha zote kwa hisani ya Mwewe

NILIANDIKA wakati wa msiba wa Kanumba kuwa umati wa watu waliojitokeza siku ya msiba wake ni ishara tosha kuwa sekta ya filamu nchini ni kubwa na yenye nguvu kubwa lakini iliyotelekezwa na serikali. Kama serikali itaamua kuzichukulia filamu kwa umakini mkubwa, ikaandaa sera na kuunda chombo maalum kitakachoshughulikia filamu mfano wa kile cha Afrika Kusini cha National Film and Video Foundation (NFVF), naamini kabisa zinaweza kuwa chanzo kikubwa na muhimu sana katika kujenga taifa na zinaweza kutumika kama jukwaa la kuchochea mijadala nchini kote.

Kupitia chombo chao cha NFVF Afrika Kusini wanajivunia ‘hazina’ za sekta ya filamu ya nchi hiyo kama Tsotsi, iliyoshinda tuzo ya Academy mwaka 2006, Yesterday, filamu nyingine iliyoshiriki tuzo za Oscar na iliyowahi kushinda katika tuzo mbalimbali za kimataifa, na U Carmen E Khayalitsha, iliyoshinda tuzo ya Golden Bear mwaka 2005 katika Tamasha la Filamu la Kimataifa la Berlin.

Muigizaji wa filamu ya Yesterday, Leleti Khumalo

Filamu ya Yesterday

Filamu ya Tsotsi iliyopata tuzo ya Oscar

Filamu hizi zimekuwa zikitia chachu na hamasa kwa watengenezaji wa filamu wa Afrika Kusini kuwa wabunifu na wenye kujali ubora. Vipi kuhusu sisi? Hivi serikali haidhani kuwa kuanzisha chombo cha aina hii kutasaidia kutufanya tuwe na kazi nzuri ambazo siku moja zinaweza kushinda tuzo katika matamasha makubwa na yanayoheshimika duniani?

Mbona hatujiulizi, sekta ya filamu Tanzania inatengeneza sinema nyingi mno zinazoifanya kushika nafasi ya tatu katika bara la Afrika, nyuma ya Nollywood (Nigeria na Ghana), lakini ni Afrika Kusini ambayo ina mafanikio makubwa kwenye sekta ya filamu. Kwa nini hatujiulizi kuwa sinema nyingi za bajeti kubwa na zenye mafanikio makubwa za kimataifa zimekuwa zikitengenezewa Afrika Kusini.

May 16, 2012

Tuache malumbano, tuunganishe nguvu kuikomboa sekta ya filamu


Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Simon Mwakifwamba

Baadhi ya wasanii wanaosemwa kuwa 
wanafanya vizuri kwenye soko la filamu nchini

SEKTA ya filamu ni moja ya sekta ambazo zimezongwa na matatizo makubwa. Tathmini nyingi zilizofanyika na zinazoendelea kufanyika zinabaini kuwa chanzo kikuu cha matatizo haya ni kutoeleweka kwa dhana nzima ya burudani hususan filamu, kutothaminiwa kwa filamu na kwa serikali kutokuwa na kipaumbele katika tasnia ya filamu katika mipango ya maendeleo ya nchi yetu.

Ingawa jamii na viogozi wa nchi yetu hawawezi kukwepa lawama kwa maendeleo hafifu ya sekta ya filamu na burudani kwa ujumla wake, wasanii, waandaaji na watendaji wengine katika sekta hii wanastahili kulaumiwa zaidi kwa kuwa hawafanyi jitihada za kutosha katika kuelimisha na kuwaelewesha wananchi juu ya dhana ya burudani (filamu), mchango wake katika uchumi, ajira na umuhimu wake katika kusimulia hadithi zetu.

May 11, 2012

Bila sera nzuri ya filamu hatufiki kokote


Dk. Fenella Mukangara, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo

NANI anaweza kunihakikishia kuwa tuna sera ya filamu? Je, sera ya filamu nchini ni ipi? Kama kweli tunaamini kuwa tasnia ya filamu ni moja ya sekta zenye nguvu na yenye kuchangia kwa kiwango kikubwa katika ajira kwa vijana, kwa nini hatuna sera inayotuongoza? Tutaendelea kuongozwa na matamko ya viongozi hadi lini? Ieleweke matamko si sheria, ndiyo maana kila kiongozi anayeingia anakuwa na matamko yake ambayo atakayefuata baada yake halazimiki kuyafuata.

Hivi hatuoni kama huu ni muda muafaka wa kuwa na sera ya filamu itakayotuongoza katika kutenda kazi zetu? Mbona kuna sera ya utamaduni japo hata huo utamaduni wenyewe unapuuzwa? Lakini ipo! Vipi kuhusu filamu?

May 8, 2012

Sajuki kwenda India leo


 Sadiki Juma Kilowoko (Sajuki) alivyo sasa

Sajuki wakati akiwa na afya njema

Msanii wa filamu nchini, Sadiki Juma Kilowoko (Sajuki) leo anasafirishwa kuelekea India kwa ajili ya matibabu baada ya kukamilika kwa asilimia kubwa ya michango iliyotolewa na wasanii na wadau mbalimbali wa tasnia ya filamu.

Msanii huyo ataongozana na watu wengine wawili katika safari yake hiyo. Zaidi ya Shilingi milioni 25 zilikuwa zikihitajika kwa ajili ya kumtibu msanii huyo ambapo pesa iliyopatikana ni milioni 16 pamoja na tiketi tatu za ndege. Hata hivyo michango mingine inazidi kuchangishwa na zitatumwa kwa ajili ya kuendelea na matibabu zaidi.

May 4, 2012

Zitto Kabwe, Halima Mdee na wasanii kibao ndani ya wimbo wa Sajuki


Sadik Juma Kilowoko Sajuki katika picha tofauti.
Kushoto alivyo sasa na kulia wakati akiwa mzima


Picha hizi zinawaonyesha Sajuki na mke wake
Wastara Juma katika hali ya furaha

Waheshimiwa wabunge wametoa track inayoenda kwa jina la "Nimepoteza Mboni Yangu" kwa ajili ya kuhamasisha kumchangia pesa za matibabu msanii Sadiki Juma Kilowoko maarufu kama Sajuki wimbo huu utaanza kusikika katika kituo cha Clouds FM.

Watu wamekuwa wakihamasishwa kuchangia kwa kutuma pesa kwenye Account No. 050000003047 AKIBA BANK, jina la mwenye account ni Wastara Juma ambaye ndiye mke wa Sajuki au watume pesa kupitia MPESA No. 0762189592.

May 2, 2012

Tujifunze kutoka sekta ya filamu ya Afrika Kusini


Mtendaji Mkuu mpya wa Taasisi ya Taifa ya Filamu na Video 
(NFVF) nchini Afrika Kusini, Zamantungwa (Zama) Mkosi

Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo nchini
Tanzania, Dk. Emmanuel Nchimbi

SIKU zote nimekuwa nikiwasihi wale wote wanaopenda maendeleo ya tasnia ya filamu nchini kuuangalia mfumo unaotumiwa na nchi ya Afrika Kusini ili kuiboresha sekta ya filamu nchini. Nadhani sasa ni muda muafaka kuliangalia kwa mapana yake, hasa kipindi hiki tunapojiandaa kuandika katiba mpya.

Sekta ya filamu ya Afrika Kusini ni moja ya sekta za filamu mahiri duniani, ni sekta inayokua na kuzidisha ushindani katika anga za kimataifa. Watengenezaji wa filamu wa ndani na wa nje wanatumia fursa mbalimbali zilizopo; maeneo ya kipekee - na gharama nafuu za uzalishaji kutokana na kiwango kizuri cha pesa ya nchi hiyo dhidi ya dola ya Kimarekani, ambacho hufanya kuwepo unafuu wa hadi asilimia 40 katika kutengeneza filamu Afrika Kusini kuliko Ulaya au Marekani na unafuu wa hadi asilimia 20 zaidi kuliko Australia.

Apr 25, 2012

Ni nini kitatusaidia kufikia mafanikio ya soko la filamu?


Ukurasa wa facebook unaweza kutumika kutangaza sinema

Pia unaweza kutumia ukurasa katika mtandao wa Youtube

TASNIA ya filamu nchini ni sawa na mtoto yatima lakini hali hii isiwe sababu ya kutufanya kulipua kazi zetu, bali tunapaswa kuangalia namna iliyo nzuri itakayotuwezesha kuboresha kazi zetu na kufanikiwa katika soko la ndani na hata nje ya Tanzania. Nimewahi kudokeza katika siku za nyuma kuhusu vigezo muhimu viwili vinavyoweza kutuongoza katika dhana nzima ya mafanikio hasa tunapolifikiria soko la filamu: Maudhui/Mahitaji ya Watazamaji na Jukwaa la Uwasilishaji.

Tunapaswa kwanza kuwaelewa watazamaji wetu kabla ya kufanya chochote, kwani ni hatua muhimu sana katika mchakato wa biashara ya filamu.