Oct 31, 2012

Tujifunze kutoka Sekta ya filamu ya Afrika Kusini

 Hii ni sehemu ya sinema ya Blood Diamond 
iliyotengenezwa Afrika Kusini

TASNIA ya filamu nchini haiwezi kukua kama tutaishia kusema bila kutekeleza tunayoyasema huku kukiwa na mambo mengi yanayoirudisha nyuma. Nimekuwa nikisisitiza kuhusu uanzishwaji wa chombo maalum kitakachosimamia utoaji wa mafunzo ya weledi kwa watengenezaji filamu kiwe kipaumbele cha kwanza.

Ni muda mchache umebakia kufika tarehe 1 Januari, 2913 ambapo ule mpango wa Serikali kama ulivyoainishwa na Waziri wa Fedha, William Mgimwa, kuhusu Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, Sura 147, ambapo Mamlaka ya Mapato Tanzania itaanza kuweka stampu kwenye bidhaa za sanaa ili uuzaji wa kazi hizo uwe rasmi na kuwawezesha wasanii kupata kipato stahili kutokana na kazi zao.

Ni katika kipindi hicho Serikali itaanza kurasimisha biashara ya muziki na filamu kwa nia ya kuhakikisha kwamba uasili wake unatambulika na hivyo kuzuia vitendo vya kurudufu kazi za sanaa (piracy of artists work) hali ambayo inadumaza ukuaji wa sanaa na vipaji hapa nchini.

Narudia tena, kama kweli tumedhamiria kuiokoa tasnia hii na wasanii, tunapaswa kuelekeza nguvu nyingi katika suala la utoaji wa mafunzo kwa wasanii na watengeneza filamu. Serikali inapaswa kwanza kutafuta gharama za mafunzo katika kuutambua mchango wa sekta ya filamu kabla ya mambo mengine yote.

Pili, iangalie uwezekano wa kuanzisha chombo kitakachokuwa na uwezo wa kuzitangaza filamu zetu kitakachoitwa, ambacho kitakuwa na idara tano: ya utoaji wa taarifa za upatikanaji wa pesa (funding information) na kutoa fursa kwa watengeneza sinema, ya kuandaa takwimu za kina na kutoa fursa ya kuzitangaza kazi zetu katika masoko mengine ya Afrika, na duniani na hivyo kuongeza uwezekano wa kuuza kazi zetu kimataifa na kuigiza pesa za kigeni.

Nyingine ni idara itakayowalazimisha wadau katika sekta ya filamu kupata mafunzo ya weledi (professionalism), itakayosimamia mapato (revenue generation) yatokanayo na filamu, na itakayosimamia kwa ukamilifu sheria za uharamia/wizi (piracy) wa kazi za sanaa na hivyo kuwafanya watengenezaji wa kazi hizi kutokuwa na hofu ya kupoteza mapato (economic reward) yatokanayo na kazi zao.

Ili kufanikisha haya tunapaswa kujifunza kutoka sekta ya filamu ya Afrika Kusini ambayo inakua na kuzidisha ushindani katika anga za kimataifa. Watengenezaji wa filamu wa nchi hiyo wanatumia fursa mbalimbali zilizopo ambazo hazitofautiani sana na hapa kwetu.

Sekta hiyo imeweza kuwa na hazina ya kujivunia ambayo ni filamu ya ‘Tsotsi’ iliyoshinda tuzo ya Academy (Oscar) katika kipengele cha filamu bora za lugha ya kigeni mwaka 2006. Filamu nyingine zilizofanya vizuri kimataifa ni ‘Yesterday’ iliyoshiriki tuzo za Oscar na imewahi kushinda katika tuzo mbalimbali za kimataifa, na ‘U Carmen E Khayalitsha’, iliyoshinda tuzo ya Golden Bear mwaka 2005 katika Tamasha la Filamu la Berlin.

Hivi sasa sinema nyingi zenye mafanikio makubwa za kimataifa zimekuwa zikipigwa nchini humo, ikiwa ni pamoja na ‘Blood Diamond’ iliyomshirikisha Leonardo DiCaprio na ‘Lord of War’, iliyomshirikisha Nicholas Cage akicheza kama muuza silaha duniani, Lord of War imesaidia kutangaza maeneo tajiri nchini Afrika Kusini - huku eneo la Cape Town likionekana kama maeneo tofauti 57 yaliyofanywa kuonekana kama meneo katika Mashariki ya Kati, Afghanistan, Bolivia, Sierra Leone na kwingineko.

Afrika Kusini imetambua kuwa sekta ya filamu ni sekta yenye nguvu na inayochangia kwa kiwango kikubwa ukuaji wa uchumi. Ingawa mchango wa Afrika Kusini kwa pato kimataifa unasimama katika asilimia 0.4 tu, sekta ya filamu kwa ndani ya Afrika Kusini inazidi kupata nguvu wakati wote.

Mwaka 1995, wakati nchi hiyo ilipoanza kutumika kama eneo muhimu kwa ajili ya uzalishaji wa filamu na televisheni, sekta hiyo ilitoa ajira nchini kote kwa watu 4 000. Imepanda hadi kufikia watu wapatao 30,000, pamoja na ajira zaidi - na mapato - vikitengenezwa katika filamu - ikihusisha usafiri, malazi na chakula.

Kwa mujibu wa Idara ya Biashara na Viwanda, sekta ya burudani nchini Afrika Kusini ina thamani ya karibu Randi bilioni 7.4, huku filamu na televisheni zikichangia zaidi ya Randi bilioni 5.8 katika shughuli za kiuchumi kila mwaka. Na kulingana na matokeo ya utafiti wa tathmini ya kiuchumi ya hivi karibuni uliosimamiwa na Tume ya Filamu ya Cape, sekta hiyo ina mapato ya moja kwa moja kila mwaka ya zaidi ya Randi bilioni 2.65 na huchangia mapato ya moja kwa moja kila mwaka ya zaidi ya Randi bilioni 3.5 ya pato la taifa la nchi hiyo (GDP).

Faida za ukuaji haraka wa sekta ya filamu ziko wazi, hasa linapokuja suala la kuingiza fedha za kigeni. Ushiriki katika uzalishaji na matokeo ya makampuni ya kimataifa katika uwekezaji wa moja kwa moja wa mamilioni ya randi katika uchumi.

Afrika Kusini imetiliana saini mikataba ya ushirikiano katika uzalishaji filamu wa pamoja na nchi nne: Canada, Italia, Ujerumani na Uingereza. Hii inamaanisha kwamba ushirikiano katika uzalishaji filamu wowote rasmi unachukuliwa kama uzalishaji wa kitaifa kwa kila nchi mwenza iliyohusika katika uzalishaji, hufanya hivyo kwa faida au mipango ya kwa msaada wa kila nchi inayohusika. Afrika Kusini pia ina mkataba wa makubaliano kuhusiana na filamu na nchi ya India.

Serikali ya Afrika Kusini imekuwa ikisisitiza umuhimu wa filamu katika kujenga urithi wa nchi hiyo kwa kuwasimulia watu hadithi zao wenyewe, na imejiweka katika “kuwezesha udhibiti” kwa kuhimiza uzalishaji wa bidhaa za ndani. Vyombo vya utangazaji vya Afrika Kusini vimekusudia kufikia lengo la kutoa kipaumbele kwa kazi huru za ndani, ambazo zimesababisha kuongezeka kwa mahitaji ya vipindi vya ndani. Zaidi ya tamthilia saba zinazorushwa kila siku Afrika Kusini zinazalishwa nchini Afrika Kusini.

"Ni maadili muhimu ya taifa ya kujenga majukwaa ya Waafrika Kusini wa kawaida kuwa na uwezo wa kubeba ushawishi katika maelezo ya picha zao wenyewe," anasema Eddie Mbalo, mtendaji mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Filamu na Video (NFVF). "Kwa njia hii, kama sekta, tunaweza kuchangia kuendeleza maadili yetu ya kidemokrasia na kuleta mafanikio."

Serikali, kupitia Taasisi ya Taifa ya Filamu na Video (NFVF), Shirika la Maendeleo ya Viwanda na Idara ya Biashara na Viwanda, ni mwekezaji mkuu katika sekta ya filamu. Taasisi ya Taifa ya Filamu na Video husaidia katika upatikanaji wa fedha katika tasnia, kupromoti maendeleo ya watazamaji wa filamu na televisheni wa Afrika Kusini, kuendeleza vipaji na ujuzi katika nchi - kwa msisitizo maalum kwa makundi maalum - na kuwasaidia watengeneza filamu kuwakilisha na kuuza kazi zao kimataifa.

NFVF hutoa fedha kwa ajili ya uzalishaji wa filamu na makala (documentaries) kwa njia ya mikopo au ruzuku. Husaidia makampuni ya uzalishaji yanayomilikiwa na Waafrika Kusini, na hutoa kipaumbele kwa miradi au mashirika yanayoweka umuhimu wa kitaifa na mapendekezo ambayo yanasisitiza kazi za ndani na ambayo yana uwezeshaji au mafunzo.

Pia inagharimia fedha za elimu na mafunzo kwa njia ya masomo mbalimbali; kutoa tuzo za maendeleo; na misaada ya maombi ya fedha kwa ajili ya uuzaji na usambazaji, inaruhusu wazalishaji filamu wa kujitegemea na wasambazaji upatikanaji wa maeneo ya kuoneshea filamu na uzinduzi wa filamu. Mnamo Machi 2007, NFVF ilitoa kiasi cha Randi milioni 26 katika ruzuku.

Taasisi ya maendeleo ya fedha inayomilikiwa na serikali, Shirika la Maendeleo ya Viwanda (IDC) imekusudia kujenga sekta endelevu ya filamu ambayo ujuzi utasambaa kwa watu kutoka makundi yaliyokuwa chini ya ubaguzi wa rangi na "kazi za ndani" za filamu zinatengenezwa na kuangaliwa na Waafrika Kusini.

Kituo cha utoaji fedha cha Mkakati wa Biashara ya Filamu na Habari cha IDC, mradi wa utangazaji na uhariri. Msaada ya fedha kwa kawaida hutolewa katika mfumo wa mkopo. Ushiriki wake wa chini ni Randi million 1 na si zaidi ya asilimia 49 ya mradi. Mnamo Juni, 2008, IDC imewekeza zaidi ya Randi milioni 500 na kufadhili filamu zaidi ya 30 nchini humo.

Idara ya Biashara na Viwanda (DTI) inatoa motisha maalum katika sekta ili kuhamasisha kazi za ndani pamoja na kuvutia uzalishaji wa kimataifa. DTI imetangaza marekebisho ya motisha za uzalishaji filamu na vipindi vya televisheni mnamo Machi 2008, ikiondoa kizingiti na kufungua mlango kwa ajili ya filamu za bajeti ndogo kutoka kwa watengeneza filamu wanaoibukia.

Kwa nini na sisi tusifikirie kufuata njia waliyoipita Afrika Kusini kama kweli tumedhamiria kuinua sekta ya filamu? Ni wakati sasa tuache blah blah na tujikite katika kutekeleza tunayoyahubiri.

Alamsiki.

Oct 24, 2012

Tunahitaji mabadiliko ya kweli na si blah blah


Watanzania wana mapenzi na sinema au michezo ya TV 
kama inavyoonekana kwenye picha hii

NI Jumapili tulivu inayoambatana na mvua ya rasharasha. Watu kadhaa wamejazana kwenye chumba kimoja katika nyumba moja wakiangalia filamu ya kusisimua ya Kitanzania. Tukio (scene) katika filamu hiyo linaanzia pale sebuleni. Ni tukio ambalo linaonekana kuvutia kiasi; linaikamata dunia ya wapenda sinema na kuwafanya watazamaji hawa waamini kuwa wanachokiona ni cha kweli.

Oct 17, 2012

Wasanii, tumieni Jukwaa la Sanaa kutatua matatizo yenu


Katibu Mtendaji wa Basata, Ghonche Materego, akisisitiza
jambo kwenye moja ya midahalo ya Jukwaa la Sanaa

NI ajabu, wasanii kulia kilio cha kuilalamikia Serikali kuwa haisaidii juhudi za wasanii katika masoko na usambazaji kwa ajili ya filamu ambazo ni kwa maslahi kwa watazamaji wa Tanzania, kilio cha kuibiwa kazi za sanaa ingawa kuna uwezekano mkubwa wanaolia kutojua wanaibiwaje kazi zao, lakini wanakwepa majukwaa ya upashanaji habari ambayo yangetumika kufikisha kilio chao na kwenda kusemea pembeni.

Hili ni jambo la ajabu sana! Ni kwewli mfumo wa usambazaji ni mbovu, lakini wasanii wanadharau majukwaa muhimu ya habari na hata vyama na mashirikisho yao wakisahau kuwa umoja ni nguvu. Ikumbukwe kuwa utengenezaji sinema ni jambo linalohitaji sana mgawanyo wa kazi. Kuna waongozaji, waigizaji, waandishi wa miswaada na kadhalika, huku msingi mkuu wa sinema yoyote ukiwa ni mwongozo (script).

Oct 10, 2012

Mtalalamika na kuponda kazi zetu hadi lini?


Cover ya filamu ya handsome wa Kijiji

WIMBI la wanaojiita wakosoaji wa filamu nchini limeibuka kiwa kasi ya ajabu, wengi wamecharuka kuandika maoni na ujumbe mbalimbali kupitia mitandao ya kijamii wakiponda sinema za Kitanzania kila kukicha pasipo hata kutoa ufumbuzi wa nini kifanyike ili kuboresha kazi zetu.

Mojawapo ya ujumbe maaruf unaotumika kuponda sinema za Kibongo katika mitandao kama facebook, Jamii Forums na twitter ni huu:

Oct 9, 2012

Nafasi muhimu kwa Watanzania kujitangaza kupitia Tuzo za Filamu Afrika (AMVCA)


Meneja Uhusiano wa Multichoice Tanzania, Barbara Kambogi, akizungumza katika semina fupi ya wadau wa Tasnia ya Filamu nchini pamoja na waandishi wa habari

Mashindano ya Tuzo za Filamu Afrika (AMVCA) yatakayofanyika jijini Lagos, Nigeria Machi 9 mwakani na kushirikisha wasanii na watengenezaji wa filamu barani Afrika yalizinduliwa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam katika hafla iliyoshirikisha makundi mengi ya filamu nchini.

Hafla hii imekuja kufuatia matukio mengine mawili yaliyofanyika mjini Lagos na Nairobi, ambapo AfricaMagic na Multichoice Africa walitangaza mpango wao mpya unaojulikana kama ‘Tuzo za Chaguo la Watazamaji wa AfricaMagic’.

Oct 8, 2012

Filamu ya Chungu ni somo kwa waandaaji filamu nchini

Dk. Vicensia Shule, mtayarishaji wa filamu ya Chungu

Filamu ya Kitanzania iliyoandaliwa na Mtanzania na kuongozwa na Mtanzania mwaka huu imeibuka na tuzo ya filamu bora Tanzania katika tuzo zilizotolewa na waandaaji wa tamasha la 15 la maonesho ya Kimataifa ya Filamu kwa Nchi za Majahazi (ZIFF).

Filamu hiyo ya Chungu iliibuka kidedea katika tuzo hizo baada ya kufanikiwa kuwa filamu bora huku pia ikitoa mwigizaji bora wa Tanzania, Richard Mshanga, maarufu kama Masinde ambaye katika filamu hiyo alitumia jina la She Mdoe.

Oct 3, 2012

Baraza la Sanaa la Taifa latoa tamko zito


Katibu Mtendaji wa Basata, Ghonche Materego

Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) limewaagiza viongozi wa Mashirikisho ya sanaa hapa nchini kufuatilia kwa karibu matukio ya ukiukwaji wa maadili yanayoendelea katika Sanaa hivi sasa na kuchukua hatua kwa wanaobainika kufanya hivyo.  

Mbali na Basata kuwakemea vikali wasanii wanaotumia majukwaa kwa kuidhalilisha Sanaa wao wenyewe na Watazamaji pia limeyataka mashirikisho kushirikiana na vyama vyao kuwaita wale wote watakaohusika na uvunjwaji wa maadili ili kuwakanya katika hatua ya kwanza na kama wasipoacha tabia hizo Baraza litawafungia kujishughulisha na kazi ya Sanaa hapa nchini.

Skendo ya picha chafu, hivi Watanzania tumeingiwa nini?


Wasanii wa filamu Aunt Ezekiel na Wema Sepetu wakiwa jukwaani

INASHANGAZA sana! Katika kipindi cha miaka michache tu iliyopita taratibu kumeingia mdudu mbaya sana katika tasnia nzima ya burudani, huku tasnia ya filamu ikionekana kuongoza. Tumekuwa tukishuhudia jinsi wasanii wa kike wanavyokuwa nusu watupu kitu kinachosemwa eti ndiyo maendeleo (kupiga hatua), na pengine inabainishwa kuwa hiyo ndiyo dalili ya kuwepo kwa mafanikio katika tasnia hii.