Rais Jakaya M. Kikwete
KWANZA napenda kukupongeza, Rais Jakaya Kikwete kwa kuchaguliwa tena kuliongoza taifa hili kwa kipindi kingine cha miaka mitano. Pia nakushukuru angalau kwa kuonesha kuutambua mchango wa sekta ya filamu Tanzania. Katika hotuba yako ya kuvunja bunge la tisa uliyoitoa huko Dodoma tarehe 20 Julai 2010, chini ya kipengele cha “Michezo, Burudani na Utamaduni”, ulinukuliwa ukisema, pamoja na mambo mengine kwamba: “...Hivi sasa tumelipia mtaalamu mshauri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam asaidie kutengeneza njia bora ya kusambaza kazi za wasanii wa muziki na filamu ili wapate malipo halali kwa jasho lao. Mafanikio ya zoezi hili yatatufundisha namna ya kuwasaidia wasanii wa fani nyingine pia...”
Ikumbukwe kuwa kwa miaka mingi sasa, wasanii na watengenezaji wa sinema miongoni mwa wadau wengine wa sanaa wameendelea kutoa sinema hapaTanzania ili kujipatia riziki kutokana na kazi yao bila mafanikio. Ingawaje sekta ya filamu ni sekta yenye thamani ya mabilioni ya fedha, wengi wameishi na kufa maskini.
Rais, serikali yako inapaswa ibadilishe mtazamo wake kuhusu wizi wa sanaa na nakala zisizo halali (pirated copies). Mambo haya lazima iyaone kama wizi na ipinge wizi kwa nguvu zote kama inatarajia kuona taaluma hii ikinawili na kuwaajili vijana wengi na hivyo kuchangia katika kuinua uchumi wa taifa letu. Ieleweke kuwa ni kosa la jinai kuuza au kununua kazi feki, kama ilivyo kwa nchi nyingi zilizofanikiwa katika tasnia hii.
Cover ya sinema ya Miss Bongo
Taaluma hii haiwezi kukua kama viongozi wataishia kusema tu bila kutekeleza huku kukiwa na mambo mengi yanayoirudisha nyuma. Binafsi nimetumia miaka kadhaa kujifunza na kufanya tafiti mbalimbali kuhusu historia ya filamu, matatizo makubwa katika tasnia hii, mfumo unaofaa kutumika katika tasnia ya filamu na mambo mengine mengi, kutoka na na haya, naweza kukuhakikishia kwamba sekta ya filamu Tanzania ina thamani ya bilioni 200 ya pesa za Tanzania katika biashara, kama tu serikali yako itatilia mkazo na kutoa msaada unaohitajika.