Apr 13, 2018

Tuwafundishe watoto umuhimu wa michezo ya pamoja



MICHEZO ni chombo cha kuwasilisha tunu msingi katika kuboresha ubinadamu na katika ujenzi wa jamii ya amani na ya kindugu.

Michezo ina faida kubwa sana kwa mwanadamu, siyo kwa wachezaji tu bali hata kwa wanaoshabikia ambao kufurahi kwao huwa ni kinga dhidi ya maradhi, hasa inapokuwa michezo ya ushindani.

Ni wazi kuwa matatizo mengi ya kiafya kwa wanadamu yanaongezeka siku hizi kutoka na mfumo mpya wa maisha tunayoishi ukilinganisha na miaka ya nyuma. Ingawa kwa wale wanaoshiriki michezo mbalimbali mara nyingi imewasaidia kuepuka matatizo hayo.


Miongoni mwa wanamichezo siyo rahisi kupata magonjwa ya kisukari, shinikizo la juu la damu n.k., na pia hujengeka katika hali ya afya njema ya viungo mbalimbali vya mwili, afya ya akili huimarika, ambapo yote hayo husababisha kuwa na jamii ya watu wenye afya na furaha.

Michezo pia imesaidia watu kufahamiana, kuwaepusha (hasa watoto na vijana) wanaoshiriki katika michezo mbalimbali katika shule za msingi, za sekondari na hata vyuo vikuu, kutojihusisha kwa wingi katika matumizi ya dawa za kulevya, pombe, sigara na vitendo vya ngono ikilinganishwa na wale ambao hawajihusishi au kushiri katika michezo mbalimbali.

Kwa kauli hiyo tunapata wazo kuu juu ya michezo kwa ujumla ya kwamba michezo imekuwa na lengo kuu msingi tangu zamani za kale la kujenga undugu na amani.

Kama mchezo ni chombo cha kuwasilisha tunu ya binadamu mwenyewe, kujieleza mwenyewe, kukubalika mwenyewe na kujikubali, inamaana kwamba nchi yoyote haiwezakani kutambulika na utaifa wake bila kuwa na utamaduni wao, na mojawapo ya viungo vya tamaduni hiyo vinavyounganisha katika duniani hii ni michezo.

Mfano, kuna baadhi ya mataifa ambayo wameweza kujitambulisha kwa mavazi, na ishara mbalimbali kiasi kwamba ukiona vazi fulani tayari unajua ni kutoka nchi fulani.

Hivyo basi, michezo ni chommbo muhimu sana katika kuendeleza jamiii. Aidha, michezo huweza kuwa kielelezo kikubwa na utambulisho wa taifa katika kutoa burudani, kujenga nidhamu, kujitangaza kiuwezo na kukomaza afya, ya mwili na akili.

Mara ngapi nchi majirani zetu wameonekana kujivunia vipaji vya wachezaji wao kila wanaposhiriki michezo ya kitaifa na kimataifa?

Mifano ipo mingi, mfano wa karibu zaidi katika Michezo ya Jumuiya ya Madoa inayotarajia kumalizika kesho Jumapili huko Gold Coast, Australia, tunasikia ni jinsi gani wanamichezo wan chi jirani wameng’aa wakati wanamichezo wetu wamebung’aa.

Pia tumekuwa tukisikia jinsi wachezaji wa mipira wanahama kutoka timu moja hadi nyingine mara baada ya kombe la dunia, maana sasa hivi wako katika soko.

Kutokana na umuhimu wa michezo katika jamii kila kipindi cha kihistoria, binadamu amekuwa akishiriki michezo katika tamaduni, mila na sanaa, tunajua michezo ya mila na desturi tangu zamani imekuwepo; mieleka, kuruka, kukimbia kulenga shaba ya mishale, kuogelea nk.

Ni michezo iliyokuwa inalenga kujiamini na kuwa na utambulisho wa kila jamii ambayo iliitwa ya jadi, hata ndugu zetu waliopelekwa kwenye utumwa na kukutana na watu wa mataifa mbalimbali walieneza jadi zao katika michezo hiyo, iliyowasaidia sana kukabiliana na matatizo yaliyokuwa yanawakumba katika utumwa huo.

Lakini baada ya michezo ya kisasa kuingia kama mipira ya miguu, mipira ya meza, ndondi, mbio, baiskeli, magari ya mashindano, mashindano ya farasi na michezo mingine mingi historia ya jadi ikalegeza thamani yake, na kuanza kutawaliwa kwanza fedha na ushindani.

Hatuwezi kusahau kwamba michezo ya jadi kwanza ilikuwa inalenga undugu zaidi, urafiki zaidi, burudani zaidi, katika kushirikiana kwa pamoja na kuishi kwa amani.

Leo hii katika viwanja mbalimbali vya mipira, kuna uwoga wa kurudi salama au kutokurudi salama, ni hatari kubwa.

Karne ya leo inazo changamoto nyingi ambazo zimejitokeza kwenye michezo kama vile, kinachotangulia ni fedha, na ushindani, au kuwepo na dharau, kutaka kushinda kwa kila njia, wakati mwingine hata watu wanaofanya michezo hiyo kupenda kutumia hata dawa za kujiharibu mwili hili wawe na guvu za kushinda.

Hata hivyo, changamoto ni nyingi kwani mabadiliko ya jamii yetu wazazi wengi kutowafundisha watoto umuhimu wa michezo ni nini, kwa sababu watoto walio wengi ukisema mchezo kitu cha kwanza kichwani ni kufikiria kushinda kabla ya burudani na furaha ya kushiriki na wengine.

Ndiyo maana utakuta watoto wengine hawapendi kushiriki michezo kama ngoma au muziki wakisema mimi siwezi maana mwenzangu ndiyo aliye na uwezo.

Watoto walio wengi wanapokwenda kwenye michezo tayari wana wazo kuwa lazima washinde tu, na kumbe uwajibikaji wa jamii zetu kuanzia katika familia muhimu sana kuwafundisha tangu utoto umuhimu wa michezo ya pamoja kwanza ni kufurahi, kunyoosha viuongo kwa ajili ya kutunza afya bora na siyo tu kushinda na kupokea zawadi.

Ili tupige hatua, michezo ifundishwe kwa watoto wetu na iboreshwe katika tamaduni zetu, ili iweze kutuunganisha badala ya kututenganisha, iboreshe utu kwanza kuliko kujali mali, ndipo tutajenga jamii ya utu wa kweli na yenye kupendana kama ndugu. Baada ya hapo tutaweza kupiga hatua kimichezo kama taifa.

No comments: