Mar 3, 2018

Black Panther inapowasuta wazungu kuhusu Afrika



TANGU filamu ya Black Panther itoke, kwa kweli imenifikirisha sana kwa jinsi ilivyojaribu kuiweka Afrika katika nafasi chanya, ikiionesha Wakanda (Afrika) kuwa nchi bora sana.
Kwa jinsi Wakanda ilivyoonekana, maana yake ni kuwa kama Afrika isingetawaliwa na wakoloni na kuachwa kukua yenyewe, ingekuwa mbali sana.

Ukiangalia filamu nyingi za watu weusi, mazingira ya Afrika yanaonekana kuwa ni mabaya sana na machafu, lakini tofauti katika filamu hii, nchi ya kufikirika ya Wakanda ina teknolojia za hali ya juu kuliko hata nchi kubwa za ulaya na Marekani.

Pia inaonesha kukatwa mawasiliano kati ya Wamarekani weusi na Waafrika wa bara la Afrika.

Ikiwa imetokana na hadithi ya michoro, Marvel Comic Black Panther, shujaa katika filamu ni T'Challa (Chadwick Boseman), ambaye anarudi nyumbani kwao baada ya kifo cha baba yake, Mfalme wa Wakanda.

Anapochukua madaraka ya kuwa mfalme, T'Challa anakabiliwa na mgogoro unaoelezea uongozi wake na hatima ya taifa la Afrika.


Akizungukwa na wanawake katika maisha yake, ikiwa ni pamoja na mama yake (Angela Basset), mpenzi wake (Lupita Nyong'o), dada (Letitia Wright) na mkuu (Danai Gurira), T'Challa anapigania kati ya kuwa Mfalme na kurekebisha makosa ya zamani.

Kinachofurahisha mno, filamu hii ina maudhui ya kiafrika, kwani hata matatizo ya kiutawala ambayo alikuwa anapambana nayo Tchalla yanaonesha kabisa kuwa ni ya kiutamaduni wa Afrika.

Kwa mfano ili uchaguliwe kuwa mfalme inabidi upambane na mpiganaji katika kila kabila katika nchi ya Wakanda na ukishinda ndipo unachaguliwa kuwa mfalme wa nchi hio, utamaduni wa namna hii ulikuwa unafanyika huko zamani katika nchi za Afrika na kuuweka katika filamu hii kunaonesha ni jinsi gani filamu ilipania kuakisi utamaduni wa kiafrika.

Katika suala la mavazi (costumes) yaliyotumika, filamu hii imefanikiwa kwa kiasi kikubwa sana, ukiangalia mavazi anayovaa mfalme wa Wakanda, pia mavazi wanayovaa watu waliopo kwenye baraza la serikali ya nchi hiyo ni ya kiafrika.

Kwa ujumla mavazi yana nafasi kubwa sana katika filamu kuonesha utamaduni fulani au kupeleka aina fulani ya ujumbe kwa hadhira iliyokusudiwa.

Hivyo, katika filamu hii licha ya kuwa Wakanda ni nchi iliyoendelea sana kiteknolojia lakini bado inakumbatia asili yake ya kiafrika katika mavazi na utamaduni wake kiujumla.
Ingawa Black Panther siyo kwamba ni filamu bora kuliko zote za Marvel la, ila ni filamu yenye upekee sana na huwezi kuifananisha na filamu kama Thor Ragnarock au Guardians Of The Galaxy 2, ingawa zote ni nzuri.

Filamu hii ina umuhimu mkubwa kwa jamii ya watu weusi kwa sababu: ndiyo filamu ya kwanza ya kueleweka ya Superhero mweusi.

Negros wa Marekani hawakuamini macho yao kuona mhusika mweusi anapewa heshima na thamani kubwa hadi kufikia kutengenezewa filamu iliyosubiriwa kwa hamu ulimwenguni kote.

Hasa ikizingatiwa kuwa Negros wametoka mbali sana, toka enzi za mwanamama Rosa Parks kunyimwa kiti katika basi, kisa ni mtu mweusi hadi zama hizi mwanadada Lupita Nyong’o anapewa uhusika mkubwa katika filamu ya kampuni kubwa ya wazungu.

Zimekuwepo filamu nyingi za watu weusi kama Superheroes zilizofanyika huko nyuma, lakini Black Panther inaonekana ndiyo ya kueleweka zaidi.

Filamu hii itaongeza umoja na mshikimano kati ya wazungu na jamii ya watu weusi, pia itapunguza ubaguzi kidogo kwa sababu imempa nafasi mtu mweusi kuwa nyota wa mchezo tofauti na filamu nyingine ambazo watu weusi wanakuwa kama wasaidizi katika filamu za ki-Superheroes, mfano Falcon ni msaidizi wa Captain America na War Machine ni msaidizi wa Iron man.

Filamu ya Black Panther inafungua milango kuachiwa kwa filamu nyingine zinazohusu Superheroes weusi katika ulimwengu wa Marvel.

Ukitoa series ya Empire iliyofanikiwa kuwainua sana watu weusi katika ulimwengu wa sinema licha ya kukosolewa kukosa maadili ya kiafrika kutokana na ushoga ulioonekana, filamu ya Black Panther itainua sana jamii ya watu weusi katika ulimwengu wa sinema, kwa kuwa Marvel wamepania kuona filamu hii ikifanya vizuri na inasemekana ndiyo filamu yao muhimu sana kuwahi kufanya tangu waanze kuachia filamu mwaka 2001.

Tayari filamu hii imevunja rekodi kwenye wiki yake ya kwanza ya uzinduzi ikitajwa kuingiza kiasi cha dola za Marekani milioni 192 nchini Marekani, ambazo ni zaidi ya shilingi bilioni 432 za Tanzania.

Kiasi hicho kimevunja rekodi zilizowahi kuwekwa na filamu kibao kwenye ‘box office’, ikiwemo ile iliyowahi kuwekwa Aprili mwaka jana na The Fate of the Furious.

Filamu hii pia imeingiza zaidi ya dola milioni 361 kutoka sehemu zingine duniani. Pia imekuwa filamu ya pili kutoka kwenye kampuni ya Marvel kuwa na ufunguzi mkubwa zaidi ikiongozwa na filamu ya The Avengers ya mwaka 2012.

No comments: