Jul 18, 2017

SRIDEVI KAPOOR: Supastaa wa kwanza mwanamke Bollywood

Sridevi Kapoor
TASNIA ya filamu ya India maarufu kwa jina la ‘Bollywood’ hadi sasa imekwisha tengeneza mastaa wengi wakubwa waliojulikana duniani, wakatengeneza pesa nyingi na kupata heshima kubwa ndani ya India na hadi nje ya mipaka ya India. Kwa mpenzi yeyote wa sinema, iwe ni sinema za Hollywood (tasnia ya sinema ya Marekani), au Nollywood (tasnia ya sinema ya Nigeria) bado atakuwa amekwishaziona filamu za India.

Nollywood mara nyingi wamekuwa wakiiga kutoka Bollywood, tasnia ambayo imewatengeneza waigizaji maarufu duniani kama Amitabh Bachchan, Shahrukh Khan, Aamir Khan, Salman Khan, Dilip Kumar, Raj Kapoor, Dharmendra, Hrithik Roshan, Rish Kapoor na wengine wengi kwa upande wa wanaume.


Filamu ya English Vinglish

Unapoongea na wapenzi wa sinema za Bollywood, mara nyingi watakwambia kuwa Amitabh Bachchan ndiye supastaa wa kwanza halisi na baba wa sinema za Bollywood, jambo ambalo japo si kweli lakini haliko mbali na ukweli.

Hadi sasa, ni Dhundiraj Govind Phalke (aliyejulikana pia kwa jina la utani la Dadasaheb Phalke) ndiye ‘baba halisi wa sinema za Kihindi’.

unapoongelea masupastaa wa Bollywood, kuna mtu anaitwa Rajesh Khanna (1942-2012) ndiye anaaminika kuwa supastaa wa kwanza halisi wa Filamu za Bollywood, akipata hadhi hiyo kutokana na kazi zake zilizokubalika sana kwa wakosoaji wa filamu (film critics) na kufanya vizuri sana sokoni kiasi cha kuweka rekodi kadhaa ambazo nyingine mpaka leo bado hazijavunjwa.

Hata Amitabh Bachchan aliwahi kukiri waziwazi kuwa Rajesh Khanna ni funga kazi. Mastaa wengine wa sasa wa Bollywood na hata wanaochipukia mara nyingi humtaja Rajesh kama muigizaji aliyewapa msukumo kuwa waigizaji.

Ila unapoongelea waigizaji wanawake wa Bollywood, muigizaji Sridevi Kapoor (53) ndiye supastaa halisi wa kwanza wa kike wa filamu za Bollywood kutokana na kuacha historia kubwa katika filamu hizo.

Hivi karibuni Sridevi alikaririwa akisema kuwa ukiwa mtu wa watu (msanii maarufu) hupaswi kuishi kama mtawa, kwa maana ya maisha ya kujifichaficha, bali unapaswa kuwa kioo cha jamii kwelikweli.

Kabla ya Sridevi alitanguliwa na waigizaji wa kike wengi waliopata mafanikio makubwa: kama Madhubala, Waheeda Rehman, Sharmila Tagore, Rekha, Hema Malini, Jaya Bachchan, Nargis, Mumtaz na wengineo lakini ujio wa Sridevi aliyekuwa mrembo na msanii mwenye kipaji cha pekee, ikawa stori mpya katika ulingo wa filamu za Bollywood. Umaarufu wake ulitokana na kazi na siyo skendo.

Wandishi kibao walijaribu kutunga stori huku akilini mwao wakimfikiria Sridev katika husika hizo. Sridevi amecheza filamu nyingi sana za lugha mbalimbali na kufanikiwa sana kimauzo lakini lugha nyingine alizotumia kucheza filamu hizo hazijui mpaka leo.

Baadhi ya filamu zilizompa umaarufu mkubwa ni pamoja na Sadma, Chandni, Gumrah, Judaai, Lamhe, Khudah Gawah, Nagina na English Vinglish iliyotoka mwaka 2012.

Sridevi alianza kuigiza tangu akiwa mtoto mwaka 1967 na ndiye mwigizaji wa kike aliyekuwa namba moja miaka ya 1980.

Sridev Kapoor katika filamu ya English Vinglish

Anaaminika kuwa mmoja wa waigizaji waliotamba sana katika sinema za kihindi kwa muda mrefu na kuwa na mfanikio makubwa hata baada ya umri kuanza kumtupa. Na aliporudi tena kwenye ulingo wa sinema mwaka 2012 kama muigizaji mkuu katika filamu ya English Vinglish alifanikiwa sana kuliteka soko la filamu za Bollywood japokuwa alikuwa nje ya ulingo wa filamu kwa miaka 15 mfululizo. 

Leo hii wapo masupastaa wakubwa wa kike wa Bollywood, waigizaji kama Aishwarya Rai, Kajol, Kareena Kapoor, Rani Mukerjee na wengineo, lakini wote hawa walitanguliwa na Sridevi ambaye ameendelea kuwa juu, wengine wengi wameshindwa kufika level yake licha ya kupata umaarufu mkubwa sana kwa kazi zao.


Hivi karibuni, Sridevi alikaririwa akiwaasa waigizaji kuwa siri kubwa ya wao kufanikiwa si kujaribu kuishi maisha ya ‘kuigiza’ na kuvikwepa vyombo vya habari, maana unapokuwa mtu wa watu (kwa maana ya msanii staa) huwezi kuishi kitawa.

No comments: