Jul 18, 2017

Soko la filamu Tanzania halijafa bali mfumo ndiyo mbovu (2)

Filamu ya Chalii wa Ngarenaro

KIGEZO cha pili cha kusaidia soko la filamu ni jukwaa la uwasilishaji; watazamaji wanahitaji majukwaa ya habari. Falsafa hii ni muhimu wakati unaposhughulikia maudhui yanayowafaa watazamaji. Maudhui ya jukwaa la uwasilishaji katika dunia ya kisasa ya filamu hayaishii tu kwenye kazi ya usambazaji, yanakwenda ndani zaidi ya soko la filamu lilivyo. Jukwaa husaidia kuwasilisha mawazo kwa watu katika njia itakayojumuisha mitazamo yao. 

Jukwaa muafaka litampa urahisi mtengenezaji wa filamu kuendana na ushindani wa soko. Watoaji filamu wanatakiwa kuandaa takwimu ya watazamaji na kukutana nao katika dunia yao iliyostawi kwenye kundi la teknolojia ya digitali. 

Filamu ni bidhaa kama zilivyo bidhaa nyingine, kuzitangaza na kuzisambaza ni vitu vyenye umuhimu sawa. Lazima kuwe na mkakati wa kujitangaza kwenye mitandao ya intaneti. Hii itaongeza mipaka katika utekelezaji wa kampeni ya kuzitangaza. 


Filamu wa Hollywood ya The Notebook

Lakini Tanzania bado tuna tatizo kubwa, Tanzania bado ina kiwango cha chini cha watu wanaotumia intaneti ukilinganisha na nchi zingine katika Afrika.

Taasisi ya Mawasiliano ya Kimataifa (ITU) katika ripoti yake inaonesha kuwa kati ya watu 56,877,529 waliopo nchini, watumiaji wa intaneti ni 3,700,000. Watumiaji wa facebook 3,700,000. Idadi hii inaifanya Tanzania kuwa nchi ya nne katika Afrika Mashariki nyuma ya Rwanda yenye watu milioni 12,159,586 lakini ina watumiaji wa intaneti 3,724,678, watumiaji wa facebook 490,000.

Kenya yenye watu milioni 48,466,928 ina watumiaji wa intaneti 39,664,377, watumiaji wa facebook 5,500,000. Uganda yenye watu 41,652,938 ina watumiaji wa intaneti 13,023,114, na watumiaji wa facebook 2,200,000

Sudan Kusini yenye watu 13,096,190 ina watumaji 2,179,963, na facebook 180,000. Na Burundi yenye watu 11,936,481 ina watumaji 526,372, facebook 450,000. Takwimu hizi ni za Machi 31, 2017 na zinapatikana www.internetworldstats.com.

Ili tuweze kupiga hatua kwenye biashara ya filamu tunahitaji nguvu kubwa kuwaelimisha wasanii na jamii faida za kutumia mitandao ya jamii inayoweza kusaidia utoaji habari za filamu na kujenga jamii yenye wafuasi, na humo, mijadala inaweza kujadilika, kipengele muhimu kabisa cha kuleta ufahamu au kampeni ya kujitangaza.

Jumuiya hizi ni maeneo ambayo watu wanaotembelea wanaweza kupata habari zaidi, kushiriki katika mijadala, kujiunga na majarida, na kubadilishana ujuzi na mawazo na watu wengine, kwa lengo la kupanua wigo mkubwa wa watazamaji. 

Katika miaka michache iliyopita, mitandao imesaidia sana kufanya uwepo wa gharama nafuu katika kutangaza na kuuza kazi kwa watengeneza filamu na hata kwa studio.

Katika baadhi ya tasnia za filamu za nchi zilizoendelea, ni nadra na kosa kubwa kutokuwa na tovuti ya kutangaza filamu kabla haijaoneshwa. 
Kwa takwimu za ITU ni ishara kuwa tunahitaji kuelekeza namna nzuri mitandao ya jamii inavyoweza kusaidia na kufanya kampeni yenye kuleta mwamko wa namna ya kujitangaza.

Njia ya haraka na madhubuti ya kujenga jamii ya watazamaji kupitia vyombo vya habari za mtandao ni kutengeneza tovuti za filamu ili kutoa makala, vipande vifupi vya filamu, kupakua picha, miziki, sauti (soundtrack), mabango (wallpapers), n.k. 

Pia kuwapa mashabiki fursa ya kupata habari kuhusu stori, wasifu wa waigizaji, kuchangia maoni yao na hata kuonesha interest zao katika filamu kwa jumla kutasaidia kuenea kwa taarifa au tetesi za filamu. 

Kuhodhi mitandao ya intaneti kama Facebook, Myspace, Youtube, Vimeo n.k., wadau wanaweza kuwa na mawasiliano na watumiaji. Siku hizi, facebook-Twitter-youtube ni njia za kujitangaza kwa haraka, watayarishaji lazima waangalie namna ya kuongeza tovuti zao na kuongeza matangazo na taarifa zao muhimu. 

Matangazo ya kulipia kwenye televisheni, radio, magazeti, majarida, na majarida ya kitaaluma ni muhimu pia.

Mtayalishaji wa filamu anaweza kuwa na ukurasa wake wa uchapishaji kwa habari za filamu, ambapo taarifa mbalimbali kuhusiana na filamu na maendeleo yake zitapatikana kwa wasomaji kwa kipindi cha muda fulani.

Kutokana na uwezo wake wa kuonesha filamu kwa watazamaji wengi kwa haraka, kutoa habari za nyota wa filamu, vipande vya filamu (trailers), mahojiano na muongozaji wa filamu na kadhalika, vinaweza kuwekwa kwenye maonesho ya televisheni, au vipindi vya habari za burudani.

Matangazo ya filamu yaliyoandaliwa vizuri (Advance trailers) na picha zinazoonesha yaliyofanyika nyuma ya Kamera (behind-the-scene footage) pia vinaweza kuwekwa kwenye vipindi maalum (documentary) kwa ajili ya vituo vya televisheni na kuvutia watazamaji kuitafuta sinema husika. 

Katika jitihada za kibiashara, kutafuta masoko ni kama uwanja wa vita, na biashara ya filamu haiwezi kukwepa hili. Baadhi ya njia makini zinaweza kutafsiri upya mfumo na kuweka kiwango kipya.

Kwa mfano, filamu inaweza kutolewa kwenye vyombo vyote vya habari kwa wakati huohuo, ikiruhusu watazamaji tofauti kuchagua lipi jukwaa linalowafaa.


Naomba kuwasilisha.

No comments: