MICHEZO si tu kwamba ina faida kubwa sana kwa
mwanadamu na nchi, pia ni chombo cha kuwasilisha tunu msingi katika kuboresha
ubinadamu na katika ujenzi wa jamii ya amani na ya kindugu.
Kwa kauli hiyo yatari tunapata wazo kuu juu ya
michezo kwa ujumla ya kwamba michezo imekuwa na lengo kuu msingi tangu zamani
za kale la kujenga undugu na amani.
Kama mchezo ni chombo cha kuwasilisha tunu ya
binadamu mwenyewe, kujieleza mwenyewe, kukubalika mwenyewe na kujikubali,
inamaana kwamba nchi yoyote haiwezi kutambulikana na utaifa wake bila kuwa na
utamaduni wao, na mojawapo ya viungo vya utamaduni huo vinavyounganisha katika
dunia hii ni michezo.
Mfano, kuna baadhi ya mataifa mbalimbali ambayo
wameweza kujitambulisha kwa mavazi na alama mbalimbali… ukiona ‘vazi’ fulani
tayari unajua ni kutoka nchi gani, hivyo basi hata michezo ni chombo muhimu
sana katika kuendeleza jamiii.
Moja ya vitu muhimu sana vinavyoweza kuitambulisha
nchi yoyote mbele ya jumuiya ya kimataifa ni michezo.
Aidha michezo huweza kuwa kielelezo kikubwa na
utambulisho wa taifa katika kutoa burudani, kujenga nidhamu, kujitangaza
kiuwezo na kukomaza afya, ya mwili na akili.
Uzuri wa michezo ni kwamba katika kufanikiwa
inakuwa furaha ya wote, tuzo zinatoka za kimataifa, jina la nchi linang’aa na
ndiyo inakuwa njia ya moja kwa moja ya kujitangaza kwenye utalii.
Faida ya michezo siyo kwa wachezaji tu bali hata
mashabiki ambao kufurahi kwao huwa ni kinga dhidi ya maradhi, hasa inapokuwa
michezo ya ushindani, kama soka, mpira wa kikapu, mpira wa pete, riadha, mbio
za baiskeli, tenisi n.k.
Michezo ni mizuri kwa afya ya ubongo, ni njia ya
pekee ya kuufanya ubongo kuchangamka na kufanya kazi vizuri, mwanadamu anapaswa
kutenga angalau muda mchache wa mazoezi.
Kucheza inatufundisha kutumia mawazo yetu na tunakuwa
wabunifu wa mambo, kwa kutumia fikra zetu katika maisha.
Mara ngapi nchi fulani inatangaza vipaji vya
wachezaji wake inaposhiriki michezo ya kitaifa na kimataifa, mifano ipo mingi, siku
za karibuni tumesikia jinsi wachezaji wa soka wakihama kutoka timu moja hadi
nyingine mara baada ya kombe la dunia, maana michezo imewaweka sokoni.
Kutokana na umuhimu wa michezo katika jamii kila
kipindi cha kihistoria, binadamu amekuwa akishiriki michezo katika tamaduni,
mila na sanaa. Tunajua michezo ya mila na desturi ilikuweko tangu zamani,
imekuwepo mieleka, kuruka, kukimbia kulenga shaba ya mishale, kuogelea n.k.
Michezo hii ililenga kujiamini na kuwa na
utambulisho wa kila jamii ambayo iliitwa michezo ya jadi, hata ndugu zetu
waliopelekwa kwenye utumwa na kukutana na watu wa mataifa mbalimbali walieneza
jadi zao katika michezo hiyo, iliyowasaidia sana kukabiliana na matatizo
yaliyokuwa yanawakumba katika utumwa huo.
Lakini baada ya michezo ya kisasa kuingia kama
mpira wa miguu, mpira wa meza, ndondi, mbio, baiskeli, magari ya mashindano,
mashindano ya farasi na michezo mingine mingi, historia ya jadi ikalegeza
thamani yake na kuanza kutawaliwa na mambo mawili: fedha na ushindani.
Si vibaya endapo michezo itatumika kama chanzo
kikubwa cha kuingiza fedha na nchi zikaweka mikakati kwa kutumia mabilioni ya pesa
kuweka msingi wa michezo, lakini hatupaswi kuuweka kapuni ubinadamu wetu kwa kuitupa
historia ya jadi na kuegemea kwenye fedha na ushindani tu.
Hatupaswi kusahau kwamba michezo ya jadi kwanza
ilikuwa inalenga undugu zaidi, urafiki zaidi, burudani zaidi, katika
kushirikiana kwa pamoja na kuishi kwa amani.
Leo hii katika viwanja mbalimbali vya mipira (si
tu uswahilini bali hata viwanja vikubwa), kuna uwoga wa kurudi salama au
kutokurudi salama, hii ni hatari kubwa!
Karne hii inazo changamoto nyingi ambazo
zimejitokeza kwenye michezo kama vile, kinachotangulizwa ni fedha na ushindani,
au kuwepo na dharau na ubaguzi wa rangi, kutaka kushinda kwa kila njia, wakati
mwingine hata watu wanaofanya michezo hiyo kupenda kutumia dawa za kuongeza
nguvu ili washinde.
Changamoto ni nyingi kwani mabadiliko ya jamii
yetu wazazi wengi hawawafundishi tena watoto umuhimu wa michezo ni nini, kwa sababu
watoto walio wengi ukiongelea mchezo, kitu cha kwanza kichwani ni kufikiria
kushinda kabla ya burudani na furaha ya kushiriki na wengine.
Watoto walio wengi wanapokwenda kwenye michezo
tayari wana wazo lazima washinde tu, na kumbe uwajibikaji wa jamii zetu kuanzia
katika familia ni muhimu sana kuwafundisha tangu utoto umuhimu wa michezo ya
pamoja kwanza ni kufurahi, kunyoosha viuongo kwa ajili ya kutunza afya bora na
siyo tu kushinda na kupokea zawadi.
Maana katika mchezo lazima mmoja tu ashinde, mfano
wa hivi karibuni tumeona machozi, masikitiko na majonzi kwenye fainali za kombe
la dunia nchini Urusi.
Tukisimama katika misingi yake tutaweza kuifanya michezo
kusimama katika kusudi lake ili baadaye ikuze uchumi, kwa sababu itakuwa imejengewa
miundombinu mizuri, nchi ikawa na wachezaji wengi katika michezo tofauti, na kuwa
chanzo kikubwa cha ajira.
Michezo ina utajiri mkubwa kwa binadamu si katika
biashara au malumbano, bali utajiri wa kuunganisha watu, kabila, jamii, taifa
na mataifa, nikitoa mfano wa changamoto zinazokabili nchi za Ulaya, ukimbizi na
uhamiaji kupitia njia ya baharini.
Tumeshuhudia watu wengi, hasa vijana, wakipokelewa
katika vituo mbalimbali katika nchi za Ulaya, wengine hata hawajui lugha ya
mahali hapo, lakini kinachowaunganisha ni zile talanta zao walizo nazo za kucheza
michezo mbalimbali.
Michezo izidi kuboreshwa katika tamaduni zetu ili
iweze kutuunganisha badala ya kututenganisha, iboreshe utu kwanza kuliko kujali
mali, ndipo tutaweza kujenga jamii ya utu yenye kupendana kama ndugu.
No comments:
Post a Comment