Oct 21, 2015

Je, unajua kuwa Filamu ya Yesu imerudiwa upya?

Muigizaji wa filamu ya Yesu, Brian Deacon

TAKRIBAN baada ya miaka 35 tokea sinema ya Yesu iliyoigizwa na Brian Deacon, muigizaji ambaye watu wengi wa kizazi cha siku hizi huamini kuwa ndiye Yesu, imerudiwa tena katika mfumo wa hali ya juu, kuanzia picha na hata uchanganyaji wa sauti.

Jesus, filamu ambayo ndiyo imevunja rekodi na inaongoza duniani kwa kutafsiriwa kwenda lugha nyingi, kwani kwa mujibu wa kitabu cha kumbukumbu cha Guiness, (Guiness World Record) filamu hiyo imetafsiriwa kwenda lugha 1,197 tofauti duniani kote, na kutazamwa na zaidi ya mara bilioni moja, huku watu zaidi ya milioni mbili wakiokoka kutokana na kutazama sinema hiyo.


Utengenezaji upya wa filamu hiyo umehusisha kupitia 'frame' moja baada ya nyingine. Sekunde moja ina takriban fremu 24, yaani kwa lugha rahisi, picha 24 ndani ya sekunde moja ambazo zinatengeneza mtiririko wa muondoko, na hivyo kufanya jumla ya fremu 173,000 kupitiwa moja baada ya nyingine na kisha kuihariri upya na kusawazisha rangi ili iendane na mfumo wa kisasa.

Kwa upande wa sauti, mfumo wa 5.1 Surround system ndiyo ambao umetumika, huku maeneo mengine yakiongezewa sauti kulingana na utayarishaji wa kisasa ulivyo kwa kizazi cha sasa.

Filamu hiyo ambayo imepewa jina la 'The Jesus Film', inakuwa ya kipekee kama ambavyo wakati inatengenezwa miaka 36 iliyopita, ilikuwa na mashiko kwa ulimwengu, kutokana na namna ilivyoandaliwa, kutayarishwa na kuongozwa.

Filamu hii ilipotoka miaka 36 iliyopita, kwa kweli ilikuwa mbele, yaani imeendelea kuliko sisi. Mkurugenzi mtendaji wa Jesus Film Project ameeleza, akisifia namna ilivyosukwa ikasukika, ambapo kila kilichoigizwa, kimetoka kwenye Biblia, na kupitia na wachungaji na wanazuoni zaidi ya 450 ili kujiridhisha dhidi ya upotoshaji.

Brian Deacon, muigizaji ambaye katu hatosahaulika kwa wasifu aliouonesha, mara nyingi alikuwa akichanganywa na Yesu, hasa kwa watu ambao wanatazama filamu hiyo bila kuwa na rejea ya mafundisho.

Na licha ya kwamba filamu hii imetazamwa na wengi ulimwenguni, ni watu wachache tu nchini Marekani ambao wameiona, ila kwa kuwa imetengenezwa upya kwa namna ya kisasa zaidi katika kuadhimisha miaka 35 tokea kupikwa mnamo mwaka 1979, inaaminiwa kuwa watu wengi zaidi wameiona, ikizingatiwa kuwa nakala moja ya DVD itajumuisha lugha za Kiingereza, Kispanish, Kikorea, Kiarabu, Kifaransa, Kijerumani, Kivietnam, na Kimandarin.


Machi 2014 ndiyo mwezi ambao filamu hiyo ilianza kutazamwa kwenye majumba ya sinema ulimwenguni, ambapo kufikia mwezi Aprili, filamu hiyo ilikuwa imewekwa pia kwenye mfumo wa DVD na Blu-Ray.

No comments: