Feb 17, 2011

Waziri Nchimbi, ni lini sekta ya filamu itakuwa rasmi?

 Waziri wa Habari, Maendeleo ya Vijana, 
Utamaduni na Michezo, Emmanuel Nchimbi

KWANZA kabisa napenda nikupongeze kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Habari Vijana na Michezo, nikitumaini kuwa Rais Jakaya Kikwete amekuona unafaa zaidi kuiongoza wizara hii nyeti inayohusu mustakabali wa utamaduni wa Watanzania.

Nakubaliana na wanaosema kuwa uteuzi wako kuiongoza wizara hii umewapa wanahabari na wasanii tumaini jipya kwa sababu tangu nchi yetu ipate uhuru miaka 49 iliyopita, wizara hiyo ilimpata waziri mmoja tu, Marehemu Ahmed Hassan Diria, aliyesimamia kwa dhati maendeleo ya wanahabari/ wasanii na ustawi wa tasnia nzima.
 
Nakuhakikishia kuwa wizara unayoiongoza imesheheni utajiri mkubwa sana wa utamaduni na uchumi kupitia filamu za Kibongo. Tatizo ni kwamba hadi sasa tasnia ya filamu bado haijawa rasmi.

Sekta ya filamu na burudani kwa sasa inakua kwa kasi, hivyo, nguvu kubwa lazima iwekezwe ili kuhakikisha kuwa sekta hii inakuwa chanzo kikubwa cha ajira na mapato miongoni mwa Watanzania ikiwa ni pamoja na kulitambulisha taifa katika ngazi mbalimbali za kimataifa.

Waziri, sina hakika kama wizara yako inaielewa nguvu ya soko letu na umuhimu wa utamaduni na uchumi kupitia filamu za Kibongo, na iwapo itasimamia vyema basi tasnia hii itasaidia kupanuka kwa ajira hapa nchini.

Mbali na hilo, nakusihi ujaribu kuangalia suala zima la wizi wa kazi za wasanii kwa kuzitazama upya sheria dhaifu za hakimiliki, na kutusaidia kupigana na wezi hawa kwa kushiriki kutunga sheria kali au kutoa hoja kuhusu tatizo hili ambalo kwa sasa limekuwa sugu.

Vilevile nakuomba ujaribu kuangalia uwezekano wa kuanzisha mfuko maalum kwa ajili ya kuwawezesha watengenezaji wa filamu, ili kuondoa mfumo uliopo kwa baadhi ya wafanyabiashara wachache kushikilia biashara hiyo, wapo wanaodhani tuwe na Tume ya Filamu (
Tanzania Film Commission) itakayotoa misaada kwa watengenezaji wa filamu ikiwa na jukumu la kuongeza ujuzi katika uandishi wa miswada na utayarishaji wa filamu.

Nimewahi kumshauri Rais ajaribu kuwaagiza watendaji wake kuutazama mfumo unaotumiwa nchini Afrika Kusini kupitia chombo chao kinachojulikana kama National Film & Video Foundation (VFVF), na uwezekano wa kuwa na chombo cha aina hii kwa maendeleo ya tasnia yetu.

Katika kufanikisha jambo hili ni lazima kiundwe chombo kitakachoongozwa na Baraza linalojumuisha wanataaluma wanaoheshimika sana katika filamu na utaalamu wa aina mbalimbali katika sekta ya filamu na televisheni, wasanii waliobobea na wenye uelewa mkubwa na wasambazaji ili kuweza kuwakilisha vyema mbinu na mikakati sahihi kwa niaba ya serikali.
Chombo hiki lazima kijue tatizo la msingi linalowakabili wahusika, na kiangalie maslahi kwa pande zote zinazohusika na biashara hii. 
 
Chombo hiki kiwe chombo cha kisheria kitakachopewa mamlaka na bunge kuongoza maendeleo ya sekta ya filamu na video hapa nchini. Visheni ya chombo hiki iwe kuhakikisha kunakuwepo ubora wa filamu katika tasnia ya filamu na video Tanzania zinazowakilisha taifa, kibiashara na kuhamasisha maendeleo.

Kama ilivyo kwa Afrika Kusini, chombo hiki kiundwe ili kusaidia kujenga mazingira ambayo yanaendelea na kudumisha sekta ya filamu na video, ndani ya nchi na kimataifa.

Waziri, najua unajua kuwa tasnia ya filamu lazima iongozwe na maadili, vivyo hivyo chombo hiki kiwe na maadili muhimu ya kujenga mazingira kwa ajili ya Watanzania wa kawaida, kubeba ushawishi katika kazi zao wenyewe, na hivyo kuimarisha demokrasia na kujenga mafanikio.

Chombo hiki kiwe na malengo makuu kumi yanayotokana na mpango wa biashara yake kama vile mamlaka yake kutoka kwa serikali:
-Kuendeleza uhusiano bora kati ya serikali, sekta ya filamu na taasisi za udhibiti.
-Kupata fedha kwa njia ya fedha za umma, uwekezaji binafsi, bahati nasibu na njia nyingine.
-Kuchochea na kuendeleza maendeleo ya ujuzi, elimu ya filamu na mafunzo.
-Kufuatilia, kupima na kupanga mikakati ya kitaifa kwa ajili ya tasnia, na kutoa ushauri kwa serikali juu ya sera zifaazo.
-Kuendeleza bidhaa za ndani na uzalishaji.
-Kuwaendeleza watazamaji wa filamu na televisheni wa Tanzania ili kuthamini mchango wao kwa kununua kazi zinazozalishwa ndani ya nchi.
-Kukuza mauzo ya filamu nje ya nchi, na kuvutia uwekezaji na uzalishaji wa kimataifa.
-Kurekebisha usawa katika sekta ya filamu na kuendeleza biashara ndogondogo na za kati kwa ajili ya ukuaji wa ufanisi katika sekta hii.
-Kusaidia kutafakari utamaduni na lugha ya Watanzania kwa watazamaji wa ndani na wa kimataifa.
-Kutoa fursa na fedha kwa ajili ya maendeleo ya filamu, uzalishaji, maonesho na mafunzo.

Lakini huwa napata shida kidogo kutokana na ukweli kwamba watengenezaji wa filamu waliopo kwenye soko letu wamekosa mfumo mzuri wa kuwawezesha kupata msaada wa mitaji kwa kazi zao. Hata hivyo, kwa mtazamo wangu, nakushauri ujaribu kuangalia kwa makini jinsi watengenezaji filamu wanavyoandaa miundo ya kihazina (funding structure) katika kampuni zao kabla haujaelekeza nguvu zako katika kusaidia sekta hii.

Waziri, najua unaelewa fika kuwa sekta ya filamu ni nguvukazi kubwa na hivyo ni moja ya sekta muhimu, ikiwa itaungwa mkono na serikali, inaweza kuchangia sana upatikanaji wa ajira. Wizara yako inapaswa kuelekeza nguvu nyingi katika suala la utoaji wa mafunzo kwa wasanii na watengeneza filamu. 
 
Kama nilivyowahi kumwandikia rais, suala la kutafuta gharama za mafunzo kwa watengeneza filamu linapaswa kuwa jambo la kwanza kabisa kwa wizara yako katika kuutambua mchango wa sekta ya filamu. 
 
Elimu na mafunzo ni ufunguo muhimu sana kwa ukuaji na uendelevu wa sekta ya filamu na video, na hata mafanikio ya tasnia hii hasa kama sekta itafaidika kutokana na mahitaji ya kimataifa ya burudani ya filamu ambayo inakua sambamba na teknolojia ya digitali inayofanya kuongezeka kwa idadi na aina ya vyombo vya utoaji wa filamu. Tasnia ya filamu, kwa asili yake, inaendeshwa na mambo makuu mawili; vipaji na ujuzi. 
 
Waziri, lengo la msingi la chombo ninachopendekeza liwe kutoa mkakati wa kitaifa na uongozi wa maendeleo ya kimitaji katika Sekta ya Filamu na Video ndani ya mfumo kwa niaba ya serikali na kutangaza sera ya kazi kwa njia ya Mkakati wa Taifa wa Stadi na Maendeleo, na hivyo kuchangia kuboresha uzalishaji na ushindani wa sekta, na kukabiliana na changamoto za maendeleo ya kijamii na kuondokana na umaskini. 
 
Pia chombo hiki kiweze kutoa na kuhimiza utoaji wa nafasi kwa ajili ya watu, hasa wanaotoka katika jamii yenye matatizo kushirikishwa katika sekta ya filamu na video.

Kuwepo uthamini katika kupeana mrejesho kutoka kwa mtunzi wa wazo kupitia awamu zote za uzalishaji, usambazaji, utoaji na njia ambayo watazamaji watapokea na mwitikio wa bidhaa (Filamu, vipindi vya televisheni, Video, nk.) ambayo kwa upande wake, hujazwa katika hadithi iliyoandikwa na utafiti na huishia kwenye muongozo (scripts) au majarida ya filamu na makala (documentaries). 
 
Chombo hiki kiweze kutoa takwimu za kina na za kuaminika, utafiti unaoendelea juu ya mahitaji ya ujuzi uliopo, elimu na utoaji wa mafunzo pamoja na kubaini mapungufu. Kufanya uratibu wa pamoja na mbinu ya kutoa elimu na mafunzo kulingana na mahitaji ya tasnia.

Pia kiweze kusimamia elimu ya filamu na mafunzo bora ya uhakika, manunuzi kutoka sekta ya filamu kwa ajili ya Mkakati wa Taifa wa Stadi na Maendeleo na mifumo yake ya kutekeleza.
Kiwe na mkakati madhubuti wa mawasiliano kwa ajili ya elimu na mafunzo ya filamu, mkakati imara wa ushirikiano na wadau wa umma na sekta binafsi kutoa uratibu na ufanisi wa kifedha kwa ajili ya elimu ya filamu na mafunzo.

Pia uwepo uratibu na usimamizi wa mgao wa ruzuku kwa ajili ya maendeleo ya ujuzi kuendana na mahitaji ya ujuzi na malengo ya chombo hiki ikiwa ni pamoja na utoaji wa huduma ya elimu ya filamu na mafunzo.

Chombo hiki kizingatie kusaidia uzalishaji wa filamu na makala (documentaries) ama kwa njia ya mikopo yenye riba nafuu au ruzuku. Chombo kichukulie utoaji pesa za uzalishaji kama uwekezaji na kitafidia matumizi yake wakati wa utoaji wa bidhaa iliyokamilika kupitia usambazaji wa ndani wa kibiashara na njia ya maonesho. Pia chombo hiki kitaamua kwa hiari yake ni aina gani ya msaada kiutoe. 
 
Naamini kuwa mafanikio ya filamu yoyote iliyokamilika au uzalishaji wa video hutegemea masoko na kukuza ubunifu. Chombo hiki kitoe mikopo ipasavyo kwa ajili ya matangazo na masoko ili kuhakikisha uzalishaji wa filamu na video za Tanzania kwa watazamaji wa ndani na wa kimataifa unakua.

Mwisho, chombo hiki kitoe msaada kwa watengeneza filamu na wasambazaji kwa ajili ya kukuza ufanisi wa bidhaa zao katika masoko ya filamu na matamasha.
Naomba kuwasilisha...

No comments: