Feb 21, 2011

Serikali yasitisha usambazaji wa filamu ya Shoga


 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 Poster ya filamu ya Shoga

Hisani Muya (Tino), mtunzi na mhusika mkuu wa filamu ya Shoga

Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo imeiagiza Kampuni ya kutengeneza filamu ya 'Al-Riyamy Production Company' kuwasilisha Filamu ya 'Shoga' kwa Bodi ya Taifa ya Ukaguzi wa Filamu kwa ajili ya ukaguzi.

Aidha Kampuni hiyo pia imeagizwa kutoisambaza Filamu ya 'Shoga' na kusitisha hatua nyingine yoyote kuhusiana na filamu hiyo hadi hapo Bodi ya Taifa ya Ukaguzi wa Filamu itakapojiridhisha kuwa filamu hiyo inakidhi kuonyeshwa hadharani kama ilivyoainshwa katika Sheria ya Filamu na Michezo ya Jukwani Namba 4 ya mwaka 1976.

Kampuni hiyo inatakiwa kuwasilisha kanda hiyo kabla ya tarehe 17 februari, 2011.Kwa mujibu wa Sheria hiyo hairuhusiwi kutengeneza filamu bila kupata kibali cha kutengeneza filamu.
Aidha kifungu cha 4 (1) inaelekezwa bayana kuwa kila anayetengeneza filamu anatakiwa kuwasilisha maombi kwa maandishi kwa Waziri chini ya Sheria hii yakiambatana na mswaada na maelezo ya filamu inayotarajiwa kutengenezwa.

Pamoja na mambo mengine katika kifungu cha 14 (2) Sheria inaipa Bodi ya Filamu mamlaka ya kukagua filamu, picha ya matangazo au maelezo yake kwa makusudi ya kuamua kuonyesha na ikiwa rushusu itatolewa maonyesho yawe kwa namna gani.

Katika Sheria hiyo kifungu cha 15 (1) kinapiga marufuku kwa mtu yoyote kuongoza,kusaidia , kuruhusu au kushiriki katika maonyesho ya filamu bila kuwa na kibali cha Bodi.
Sheria hii ilipitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa waraka Namba 22 wa mwaka 1974.

Imetolewa na Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano,
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.
Tarehe 14 februari, 2011.

No comments: