KILA mtu aliyezaliwa na
mwanamke anacho kitu cha pekee alichojaaliwa kuwa nacho. Kitu hiki si umbile
lake, elimu yake, umaarufu wake, usomi wake, cheo chake katika jamii, au
utajiri wake wa vitu na fedha; la hasha, bali ni kipaji chake.
Kipaji ni uwezo wa kiasili
ulio ndani ya mtu katika maumbile, nafsi na roho yake. Kipaji kinatoka ndani
yake. Ni tunu au zawadi toka kwa Mungu ambayo hakuna anayeweza kutunyang’anya
au kutuibia mpaka tutakapokufa.
Fedha na magari vyaweza
kuibiwa, nyumba inaweza kuanguka, kubomoka, kubomolewa au hata kuungua, lakini
vipaji hubakia kuwa nasi daima.
Kipaji ni karama. Ni zawadi anayokirimiwa mtu kutoka kwa
Mungu. Kipaji hiki hukua katika ufanisi na matumizi ikiwa kitakuzwa na
kuendelezwa na kimenuiwa kutumika kwa niaba ya vingine, si kwa ajili ya
ubinafsi bali kwa faida ya wengine na si yake wenyewe.
Kwa kawaida kila mtu ameletwa
duniani kwa kusudi maalumu na la kipekee. Ili kutekeleza kusudi hilo, Mungu katujaalia
vipaji mbalimbali, wengine wamepewa vipaji vya uimbaji, uigizaji, ufundi,
uchoraji, uchongaji, ususi, uchezaji muziki, uchekeshaji, uchezaji michezo
mbalimbali, ujasiriamali, utabibu, ualimu, uongozi katika jamii, ugunduzi, uandishi
n.k.
Wapo watu wanaolalamikiwa
au kulaumiwa kuwa hawana ubunifu. Lakini kila mtu ana upekee katika jamii
kupitia kipaji chake. Hakuna mtu yeyote yule mwenye afya njema asiye na kipaji,
ni kwa vile tumeshindwa kukitambua kipaji chake.
Kwa kifupi, wengi wetu
tunashindwa kabisa kuvitambua, kuviendeleza na kuvitunza vipaji vyetu. Unaweza
ukawa unazunguka kila kona kutafuta ajira, kumbe unatembea na ajira au mtaji
wako ambao labda ni sauti yako nzuri kwa kuimba.
Ni muhimu sana kutambua
kipaji chako ambacho ni mtaji wa kukupa ajira. Ukitambua kipaji chako na
kukitumia ipasavyo utakuja kuwa mtu muhimu sana katika jamii. Hebu fikiria mtu
kama Nasib Abdul almaarufu Diamond Platnumz
au Ali Kiba, hivi wangebaki kulalamika kwa kuwa hawajafika chuo kikuu au wangetegemea
kuajiriwa ingekuwaje leo!
Wengi tunaojiona tumesoma
au tuna utaalamu hatuufikii utajiri wa Diamond Platinumz, kwani kipaji chake
cha kuimba kimemfanya amiliki miradi ya maana.
Leo hii watu kama Diamond,
vipaji vyao vimekuwa msaada hata kwa watu wengine wakiwemo jamaa zao na watu
wanaowazunguka. Ni vipaji ambavyo tunazaliwa navyo kwa ajili ya faida ya mwenye
kipaji na jamii nzima.
Mtu anapewa kipawa cha asili kama matokeo ya mchanganyiko wa
jenetiki (huweza kurithiwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine), baadhi wakiwa na
uwezo wa asili katika muziki, sanaa, au hisabati.
Pia kinaweza kutokana na mazingira (endapo utakulia katika
familia ya muziki itachangia katika kuendeleza kipaji cha muziki). Lakini ili
kipaji kifanye kazi yake sawasawa kwa kusudi la Mungu ni lazima mtu atumie kipaji
chake kwa lengo la kuisaidia jamii yake.
Ni kama nyuki
wanavyotengeneza asali tamu na ya ubora wa viwango vya hali ya juu, lakini
hawafundishwi na yeyote wala kusomea popote. Hawana cheti wala shahada ya chuo
kikuu bali ni uwezo wa asili ulio ndani yao.
Ndivyo vipaji vyetu
vilivyo, ni kama uwezo wa nyuki ulivyo katika kuzalisha asali tamu. Lakini vipaji
hivi vinatofautiana kati ya mtu na mtu, kutokana na jinsi vilivyokuzwa na
kuendelezwa.
Watu wanapewa vipawa ili waweze kusaidia kuchangia maendeleo
kwenye jamii zao, na kama kipaji alichopewa mtu hakitumiki ipasavyo ni sawa na
kumiliki bunduki bila risasi halafu utegemee utaitumia bunduki hiyo kuwindia au
kujilinda.
Kwa kutumia vipaji vyetu ipasavyo, sisi pia hupata ukamilifu
katika maisha kupitia kwa kazi zetu. Kwa mfano, mimi kama mwandishi ili niweze
kuwa mkamilifu ni lazima niandike mambo yanayoigusa na kuisaidia jamii yangu
badala ya kujifikiria kibinafsi.
Hilo ndilo kusudi la Mungu
la kutujaalia vipaji au uwezo tofauti kwa ajili ya kutufaidisha wenyewe,
kufaidiana na kuifaidisha jamii.
Ndiyo,
uandishi ni kipaji, mwandishi mzuri lazima kwanza awe na kipaji na uwezo wa
kuandika kabla hajasomea. Hapo utagundua kuwa kipaji mtu huzaliwa nacho au
hukipata katika umri mdogo, hasa kutokana na mazingira anayokulia.
Lakini
kipaji hiki kinapaswa kuendelezwa kwa mafunzo au kutumika kwa muda mrefu ili
aliyejaaliwa kipaji hicho aweze kufanikiwa, na ukifuatilia historia ya
waandishi wengi waliofanikiwa utagundua kuwa wameviendeleza vipaji vyao na kuishi
muda wao mwingi katika maisha yao wakifanya kazi ya kuandika bila kuchoka.
Hivyo, ni kazi ya jamii kusaidia kuwajenga vijana wenye
vipaji ili waweze kuimarika zaidi na kutumia vipaji vyao kwa ajili ya kuleta
maendeleo katika nchi. Matokeo yawe kwamba vipawa hivi vitumike kulifanya taifa
kuwa na nguvu za kiuchumi na kukuza ajira.
Mwezi Juni mwaka huu, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alipofungua
rasmi Mashindano ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Sekondari Tanzania
(UMISETA) kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza aliwataka viongozi wa
Mikoa na Wilaya zote nchini wahakikishe kuwa masomo ya haiba, michezo na stadi
za kazi yanafundishwa kikamilifu kwenye shule zote za msingi.
Pia Waziri Mkuu alitaka somo la elimu ya michezo kwa
Shule za Sekondari lifundishwe kikamilifu na vyuo vya michezo kama Malya
viendelee kuwaendeleza walimu wa michezo, huku akiwaagiza Maofisa Elimu wa
Mikoa na Wilaya kuhakikisha maeneo ya michezo na burudani yanapimwa na yasiingiliwe
na vitengo vya michezo kwenye ofisi za Halmashauri na Mikoa vitengewe fedha za
kuendeshea michezo.
Kwa kauli hii na nyingine
kutoka kwa Waziri Mkuu, ni vyema jamii ikaviendeleza vipaji ipasavyo ili viweze
kuitangaza vyema nchi kimataifa na kuongeza fursa ya ajira kwa Watanzania.
Jamii ni kama mwili, una
watu tofauti wenye uwezo au vipaji tofauti kama ambavyo mwili una viungo
tofauti vyenye uwezo tofuati. Watu, kama viungo vya jamii tunapaswa kutumia
vipaji vyetu tofauti kwa faida ya watu wote na jamii nzima.
No comments:
Post a Comment