SANAA ni hazina muhimu sana inayohifadhi kazi ya
uumbaji, ina lugha pana ambayo hakuna lugha yoyote nyingine yenye upana kama
huo.
Hii si lugha ya sayansi, wala lugha ya kawaida,
wala lugha ya mawaidha yenye upana kama wa lugha ya sanaa. Inapaswa ipewe
umuhimu na pafanyike juhudi za kuhakikisha muundo wa kujivunia wa sanaa
unatumiwa.
Bila ya kuwepo sanaa, matamshi ya kawaida hayawezi
kupata nafasi yake katika akili ya mtu yeyote yule. Sanaa ni ala na nyenzo nzuri
sana ya kufikisha na kupanua fikra sahihi.
Sanaa ni ala, ni zana, ni chombo; naam chombo
muhimu mno. Hivyo si sahihi kuipuuza sanaa na kudharau wajibu wa kuiendeleza na
kuipanua, na si sahihi kudhani kwamba sanaa ni dhambi au kufikiri ni makosa
kuwa msanii na vitu kama hivyo.
Kila msanii peke
yake ni kama dunia nzima na sifa hiyo maalumu ya msanii imo ndani ya nafsi
yake. Kama mtu angelipata fursa ya kudiriki dhati ya wasanii angeliweza kuona
shani za dunia na maajabu yake.
Pia wasanii wana dhamana ya kutibu na kuganga
madonda yaliyomo ndani ya moyo wa binadamu na hivyo kumkirimia tena: imani na
matumaini, hasa kwa wale wanaoishi katika mazingira magumu, ili kwa njia ya
kazi ya wasanii, watu hawa waweze kutambua uzuri wa kazi ya uumbaji.
Katika dunia iliyojaa
furaha na majonzi, matumaini na wasiwasi ndani yake ni sanaa inayoweza kuvutia
nyoyo na macho, kwa sababu sanaa ni kipawa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Mtaalamu wa sanaa ambaye pia alikuwa Mkurugenzi wa
Tume ya Utamaduni na Sanaa (NCCA) nchini Philippines, Malou Jacob aliwahi
kuliambia kongamano la kimataifa la sanaa lililofanyika Australia kuwa, pamoja
na faida nyingi zinazoletwa na sanaa, pia sanaa ni tiba yenye njia nyingi.
Alitolea mfano kwamba kuna wakati aliwatumia
ipasavyo wasanii wa Philippines kuitibu jamii iliyokumbwa na mafuriko nchini
humo na kufanikiwa kwa kiwango kikubwa.
Anasema kuwa jamii hiyo ilipona majeraha ya dhiki
baada ya mapinduzi mwanzoni mwa miaka ya 2000 kupitia wasanii.
Hapa tunakubaliana bila shaka kuwa wasanii ni
nguvu kubwa. Jambo muhimu ni kuwafanya wao wenyewe wajitambue na wajiamini,
kisha na jamii yenyewe iwaamini kwamba wakitumika inavyotakiwa katika mambo ya
maana, wanaweza kuchagiza matokeo chanya.
Jamii inapaswa
kuwatumia wasanii katika kutibu majeraha yaliyopo kwenye jamii hiyo, na msanii kwa
upande wake anapaswa kujua kuwa ana jukumu mbele ya uhakika maalumu.
Kuna baadhi ya
watu wanasema kwamba kuna ukinzani na mgongano katika maneno yanayounda
istilahi ya Sanaa ya Uwajibikaji.
Neno sanaa lina
maana ya kile kitu ambacho kinatokana na mawazo huru ya mwanaadamu, wakati neno
uwajibikaji lina maana ya mtu kujifunga (commitment) na kile ambacho anapaswa
kukitenda.
Sasa maneno hayo
mawili yanaweza kuwa na uhusiano gani baina yake? Wako watu wenye mawazo hayo
na wanaoona haiwezekani maneno hayo mawili kukutana.
Lakini ni wazi
kwamba mawazo hayo si sahihi na ni makosa kufikiria hivyo. Jukumu la kuwajibika
msanii liko juu ya mabega yake kwa kuwa kwake tu mwanaadamu hata kabla ya
kufikiria kipaji chake cha kisanii.
Ni wazi kuwa kabla
ya msanii kuwa msanii, yeye kabla ya yote ni mwanadamu. Mwanadamu naye hawezi
kusema kuwa hana majukumu wala ulazima wa kuwajibika.
Jukumu la kwanza
kabisa alilo nalo mwanaadamu linahusiana na wanadamu wenzake, japo kuna
majukumu yanayomuhusu mwanadamu kuhusiana na maumbile, ardhi na mbingu, lakini
jukumu lake kubwa ni kuhusiana na wanaadamu wenzake.
Msanii ana majukumu katika pande zote, na
hapaswi kutosheka na daraja ya chini. Hilo ni jukumu na ni jambo la wajibu.
Msanii mvivu na
asiyewajibika na ambaye hafanyi bidii ya kukuza kipaji na kazi zake za kisanii,
bila ya shaka yoyote atakuwa hakutekeleza wajibu wake wa kisanii katika kazi
yake.
Ni jukumu la
msanii kuwajibika na kufanya juhudi bila kuchoka katika kazi zake. Inawezekana
baadhi ya wakati mtu akafanikiwa kufikia katika hatua ambayo hawezi kwenda
mbele zaidi ya hapo wala kufanya juhudi zaidi ya hizo zilizo nje ya uwezo wake
– hilo si neno – lakini mtu anapaswa kuwajibika na kutimiza wajibu wake.
Lakini
imekuwa inasikitisha sana kuona kwamba wasanii walio wengi wala hawatambui
nguvu kubwa waliyokuwa nayo na hawajiamini zaidi ya kutumika kwa maslahi ya
wachache.
Inasikitisha
pale unapoyaona maisha ya wasanii yanapokuwa ya kuigiza, wanaonekana kama ni
wenye neema, kumbe wanaongoza kwa kuwa na maisha mabaya.
Na
hata pale inapojitokeza neema basi huwa ni kwa muda fulani tu, hasa pale
wanapotumiwa na baadhi ya wanasiasa kwa maslahi ya wanasiasa katika kufanikisha
jambo lisilowahakikishia uhakika wa soko la kazi zao.
Hii
inatokana na kwamba wamekuwa wakipewa mipango mingi isiyotekelezeka na kwa
sababu wao wenyewe na hata viongozi wa vyama vyao hawajui nini wanachokihitaji
na kwa muda upi, hivyo hujikuta wakinasa kwenye mtego wa kutumika.
Hata
zile harakati na ajenda ya ukombozi wa wasanii zimekwisha, na sasa kilicho
akilini mwao ni jinsi gani wanavyoweza kutumika au kutumia umaarufu wao
kuhakikisha mwanasiasa fulani anapata madaraka, kwa kigezo kuwa anajali
maendeleo ya vijana.
Inashangaza
kuona wasanii wanaacha kupigania haki zao ikiwa ni pamoja na soko la bidhaa zao
na kujiingiza kwenye masuala tofauti kama siasa.
Tumefikia
hatua mbaya, wasanii wanaunda timu kulingana na wagombea (wakati wa uchaguzi) ili
kutumika kuwapigia kampeni wagombea fulani.
Kufuatia
mikakati na harakati walizonazo sasa – za kutumika – utatambua kuwa si wao tu
hata viongozi wao wanaowaongoza pia hawajui kwanini walianzisha umoja? Hawajui
lengo hasa lilikuwa nini? Na hawajui wanahitaji nini?
Hadi
leo hawana dira, na malengo yao ni ya muda mfupi tu (kuganga njaa), matokeo yake
wamejikuta wakiishia kuilalamikia serikali kwa kukosa fursa za kupata mikopo
kwenye asasi za kifedha, na kutothaminiwa.
No comments:
Post a Comment