Sep 4, 2018

Je, unajua kuwa kila msanii ni wa kipekee?



KAMA wewe ni msanii, iwe wa uimbaji, uigizaji, uchoraji, uchezaji muziki, uchekeshaji, uandishi n.k., amini usiamini hakuna mtu ambaye ana kila kitu ulicho nacho wewe.

Hata kama binadamu ni wawili wawili, basi anaweza akatokea mtu mmoja tu kati ya watu maelfu ndiyo akakufanana kwa vitu vingi: sura, rangi, uzungumzaji, uwezo wa sanaa, mvuto n.k.

Kitu ambacho pengine hukijui ni kwamba mamilioni ya watu duniani wametafuta msanii kama wewe, mwenye sifa kama zako ili wamtumie kwenye matangazo, kwenye video za muziki, kwenye filamu, kwenye mfululizo wa sinema au michezo ya kuigiza maarufu kama series n.k.


Au pengine wamekutafuta ili watumie kazi zako za sanaa unazoziandaa, watumie script zako, ubunifu wako na hata kipaji chako ulicho nacho, na walikuwa tayari kukulipa kiasi kizuri cha pesa, lakini walikosa mtu kama wewe (kwa kuwa hukujionesha ukafahamika), hivyo wakampachika mtu tu ilimradi wafanikishe kazi yao.

Kwa kuwa unacho kitu cha pekee ulichojaaliwa kuwa nacho, usije ukafanya kosa kubwa la kujaribu kuwa mtu mwingine, kwa maana ya kutaka kumuiga mtu mwingine ambaye ana vitu tofauti na wewe, na usiruhusu kulalamikiwa au kulaumiwa kuwa huna ubunifu.

Kila mtu ana upekee katika jamii kupitia kipaji chake, na kila mtu ameletwa duniani kwa kusudi maalumu na la kipekee.

Suala ni kwamba kama kipaji unacho kwanini ubaki unakufa na njaa? Fahamu kuwa unaweza kufanya biashara ya kipaji ulicho nacho kwa kujiweka sokoni wewe mwenyewe uonekane na wale wanaokuhitaji.

Kama msanii unapaswa kufanya juhudi za kukuza kipaji chako cha usanii ndani ya nafsi yako. Msanii ni yule aliyejaaliwa kipaji cha sanaa, na neno sanaa lina maana ya kile kitu ambacho kinatokana na mawazo huru ya mwanadamu.

Kwa kuwa kiini cha sanaa ni “ubunifu” nina kila sababu ya kuamini kuwa kila binadamu ni msanii.

Tofauti huwa iko katika aina za sanaa anazohusika nazo mtu mmoja na mwingine kwani hakuna binadamu anayeweza kujihusisha na sanaa za aina zote.

Japo ubunifu mwingine huegemea katika baiolojia na teknolojia, yaani sayansi, lakini ili ukamilike lazima uhusishe sanaa.

Sanaa ni dhana pana inayohusisha mambo mengi. Zaidi ya asilimia 60 ya maisha ya kila binadamu huhusishwa na sanaa kwani hata ubunifu anaoufanya mwanandoa katika ulaji wa ‘chakula cha usiku’ ni sehemu ya sanaa na hata ubunifu anaoufanya mpishi katika chakula anachopika ni sanaa pia.

Katika muktadha rahisi tunaiweka sanaa katika mambo kadhaa yaliyozoeleka kuitwa sanaa ambayo ni pamoja na: Michezo; Utunzi; Uandishi; Kuimba; Kuigiza; Ushonaji; Uchongaji; Uchoraji; Ufinyanzi; Ususi; Kupaka rangi na mengine mengi.

Lengo kuu la sanaa ni kuelimisha, kuburudisha, kuonya na malengo mengine ni pamoja na kutoa ajirakuhamasisha na kuendeleza tamaduni.

Sanaa huboreshwa na ubunifu pamoja na viungo vya sanaa ili iwe sanaa bora. Viungo vikuu vya sanaa ni taaluma na kipaji, kwa maana kwamba sanaa huanzia kwenye kipaji, kisha mafunzo hufuatia.

Japo mtu anaweza kutumia kimoja kati ya viungo hivi katika kutekeleza kazi za sanaa akafanikiwa lakini inakuwa bora zaidi pale vinapohusika vyote viwili kwa pamoja.

Kipaji na taaluma katika sanaa hufanya kazi sambamba sawa na nguzo mbili zilizobeba nyumba moja kila moja kona yake kiasi kwamba hauwezi kuondoa moja kati ya nguzo hizo na bado nyumba ikabaki salama.

Japo katika hili naweza kutofautiana na baadhi ya watu wenye dhana kwamba kipaji pekee kinatosha kukufanya kuwa bora, lakini vyote viwili ni lazima vifanye kazi sambamba.

Ni kweli, sanaa ni kipaji na kama kuna mtu atabisha kuwa si kipaji atakuwa na matatizo ya kufikiri. Lakini sanaa ni zaidi ya kipaji, sanaa ni taaluma. Kwa maana kuwa inasomewa.

Ni vigumu kwa fani yoyote kubakia katika kundi lisilokuwa na vigezo vya upimaji wa ubora. Kusipokuwepo vigezo vya kupima utaalamu wa fani, sanaa zetu zitaendelea kuwa duni, zisizothaminika.

Hata hivyo, kila msanii peke yake ni kama dunia nzima na sifa hiyo maalumu ya msanii imo ndani ya nafsi yake. Kama mtu angelipata fursa ya kudiriki dhati ya wasanii angeliweza kuona shani za dunia na maajabu yake.

Kwa kifupi, wasanii wengi wanashindwa kabisa kuvitambua vitu vya kipekee walivyo navyo ndani yao, wanashindwa kuviendeleza na kuvitunza vitu hivyo.

Unaweza ukawa unazunguka kila kona kutafuta ajira, kumbe unatembea na ajira au mtaji wako ambao labda ni kipaji cha uchekeshaji, uchoraji, uandishi au ni sauti yako nzuri kwa kuimba.

Kama msanii mwenye upekee, hupaswi kutosheka na daraja ya chini. Msanii mvivu na asiyewajibika ambaye hafanyi bidii ya kukuza kipaji na kazi zake za kisanii, bila ya shaka yoyote atakuwa hakutekeleza wajibu wake wa kisanii.

Ni jukumu la msanii kuwajibika na kufanya juhudi bila kuchoka katika kazi zake.

Inawezekana baadhi ya wakati mtu akafanikiwa kufikia katika hatua ambayo hawezi kwenda mbele zaidi ya hapo wala kufanya juhudi zaidi ya hizo zilizo nje ya uwezo wake – hilo si neno – lakini bado anapaswa kuwajibika na kutimiza wajibu wake.

Uwajibikaji huo hauwezi kupatikana bila ya kuweko shauku, msukumo na hisia za kuwajibika ndani yake.

No comments: