Aug 17, 2018

Aretha Franklin: Malkia wa Soul aliyeishi maisha ya ‘mateso ya kimyakimya’



MUZIKI ni chombo ambacho kimewavutia wanadamu. Katika kutumia nyimbo, waimbaji wameweza kuhifadhi historia na utamaduni wa jamii zao.

Muziki umekuwa ukitumika kama njia mojawapo ya kujifundisha utamaduni na aghalabu hutumiwa katika kumwelezea mtu, mazingira yake na jinsi anavyoweza kuyatumia na kuyatunza vilivyo.

Kama chombo ambacho hutumiwa kuelezea historia ya jamii, muziki hutumiwa kupasha ujumbe maalumu kwa wanajamii hasa kutoka kizazi kimoja hadi kingine na hutumiwa hasa kuelezea historia, imani, itikadi na kaida zajamii.

Nyimbo kama zao la mazingira ya jamii, zinaweza kufananishwa na mtoto ambaye hufinyangwa na mambo mengi katika historia ya jamii yake.
Hata hivyo, muziki ni zaidi ya taaluma kama zilivyo taaluma zingine za sheria, uhandisi, udaktari, usimamizi wa fedha, biashara na kadhalika. muziki ni kipawa ambacho mtu hutunukiwa na Mungu.


Kipawa hiki ni uwezo wa kiasili ulio ndani ya mtu katika maumbile, nafsi na roho yake. Kipawa hiki kinatoka ndani yake. Ni tunu au zawadi mahsusi kutoka kwa Mungu, ambayo hakuna anayeweza kumnyang’anya au kumuibia mpaka anapokufa.

Kwa kawaida kila mtu ameletwa duniani kwa kusudi maalumu na la kipekee. Ili kutekeleza kusudi hilo, Mungu kamjaalia kila mmoja kipawa chake, wengine wamepewa vipawa vya uimbaji, uigizaji, ufundi, uchoraji, uchongaji, ususi, uchezaji muziki, uchekeshaji, uchezaji michezo mbalimbali, ujasiriamali, utabibu, ualimu, uongozi katika jamii, ugunduzi, uandishi n.k.

Unapovamia kipawa ambacho si cako kwa vyovyote hutoweza kufika mbali, utakwama tu. Ndiyo maana wapo wanamuziki wengi ambao wamewahi kutamba kwa muda mfupi kisha wakapotea, wapo walioimba wimbo mmoja tu au nyimbo mbili na kupotea na wengine wakafanikiwa kutoa albamu moja tu kisha wakapotea kwenye gemu.

Ila wengine wameweza kudumu kwenye gemu kwa muda wote bila kuchuja, na wengine wanawika hadi leo hata baada ya vifo vyao miaka mingi iliyopita.

Mmoja wa wanamuziki mashuhuri ambao wameweza kudumu kwenye gemu la muziki ni Aretha Franklin, aliyejulikana kama ‘Malkia wa muziki wa taratibu Soul’, ambaye amefariki dunia siku ya Alhamisi.

Aretha Franklin alikuwa mwanamke wa kwanza kuchaguliwa katika Rock na Hall of Fame amefariki dunia huko Detroit akiwa na umri wa miaka 76.

Mwanamuziki huyo alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa saratani ya kongosho tangu mwaka 2010 na alitangazwa kuwa anaumwa mwaka jana wakati alipoamua kustaafu rasmi muziki.

Muziki wake ambao ulijulikana zaidi ulikuwa ni 'Respect and Think' ambao ulikuwa katika nyimbo 20 bora zilizopendwa zaidi nchini Marekani kwa miongo saba.

Aretha aliweza onesho lake la mwisho mwezi Novemba mwaaka jana katika gala iliyoko mjini New York akiwa amesaidiwa na taasisi ya Elton John ya ‘Elton John Aids Foundation’.

Hata hivyo, Aretha Franklin aliishi maisha ya ‘mateso ya kimya kimya’ na miongoni mwa siri za maisha ya Franklin zilizomfanya kupenda kuishi maisha ya “faragha sana,” ni jukumu lake kama mama, jambo lililokuwa moja ya mambo yaliyomfanya nyota huyo kuwa na maisha ya faragha sana.

Malkia huyu wa Soul alikuwa na watoto wanne, huku mtoto wake wa kwanza  akiwa amempata akiwa katika umri wa miaka 12 tu.

“Alikuwa na maisha magumu sana utotoni,” David Ritz, mwandishi ambaye aliandika wasifu mara nyingi juu ya maisha ya Aretha Franklin alibainisha hayo kabla ya kifo cha nyota huyo.

Maisha magumu ya utotoni ya mwimbaji huyo wa “(You Make Me Feel Like) A Natural Woman” yalisababishwa na kutengana kwa wazazi wake, mama yake Barbara na baba yake Clarence LaVaughn, jina ambalo aliamua kumpa mtoto wake wa kwanza, hii ni kwa mujibu Respect, kitabu cha Ritz kinachohusu maisha ya Franklin.

Mama yake Franklin aliondoka nyumbani akiiacha familia wakati mwimbaji huyo alipokuwa na umri wa miaka 6 tu kwa sababu ya kuchukizwa na mumewe aliyekosa uaminifu.

“Alijaribu sana kuonesha kuwa aliishi maisha ya furaha na watoto wenye furaha na kila kitu kilikuwa kizuri, na hadithi nyingine zozote kinyume cha hayo ziliweza kumkasirisha sana,” alibainisha Ritz kwenye kitabu hicho cha Respect.

Franklin alikuwa hajawahi kuthibitisha hadharani kuhusu baba wa mtoto wake mkubwa aitwaye Clarence mwenye umri wa miaka 63, lakini Ritz aliweza kufichua siri hiyo katika kitabu chake kwamba baba wa Clarence, aliitwa Donald Burke, ambaye walijuana na Franklin tangu shule.

“Aretha alirudi shuleni baada ya kumzaa Clarence,” dada ya nyota huyo wa muziki, Erma alibainisha kwenye kitabu cha Respect. “Alikuwa mwanafunzi mzuri ambaye alifanya vizuri katika madarasa yake yote.”

Miaka miwili tu baada ya kumzaa Clarence, Franklin alimpata mtoto wake wa pili, Edward, ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 61.

Franklin hatimaye akaamua kuacha shule ili azingatie kipaji chake cha muziki, kilichomfanya kuishi maisha ya “mateso ya kimya kimya,” kama ambavyo dada yake Erma anaelezea kwenye kitabu hicho.

“Tulikuwa sehemu ya kizazi hicho cha waimbaji wadogo wa kike ambao kwa hakika walijitolea muda wao pamoja na watoto wetu kuhudhuria kwenye kazi zetu. Tulifanya hivyo kwa kufahamu,” dada mkubwa wa Franklin alinukuliwa kwenye kitabu hicho. "Pia tulifanya hivyo tukiwa na hatia.”

Kuwatunza watoto wake wawili ilikuwa ni kazi ngumu sana kwa “Mama Mkubwa,” yaani bibi wa Franklin, kwa mujibu wa biografia ya mwaka 2015 ya maisha ya Franklin.

“Nilitamani sana kutoka na kwenda matembezi na rafiki zangu,” Franklin aliwahi kuliambia jarida la Ebony mwaka 1995 kuhusu umama wake katika umri mdogo.

“Nilitaka kuwa katika sehemu mbili kwa wakati mmoja. Lakini bibi yangu alinisaidia sana, na dada yangu na binamu yangu. Walijitahidi kuwalea watoto wangu ili nipate nafasi ya kutoka mara kwa mara.”

Akiwa na umri wa miaka 19, Franklin aliolewa na Ted White, na waakapata mtoto wa kiume aliyempa jina la Ted “Teddy” White, Jr., ambaye sasa ana umri wa miaka 54.

Ted na mwimbaji huyo wa soul waliachana mwaka 1969 baada ya taarifa za unyanyasaji wa ndani kufichuka, kwani mwaka 1968 makala ya jarida la Time ilielezea jinsi ambavyo Ted “alimtendea visivyo” mwanamuziki huyo zaidi ya mara moja.

Ted White, Jr. alijiingiza kwenye muziki na kumpigia gitaa mama yake, Franklin, kabla ya kuamua kuanzisha muziki wake kwa jina la Teddy Richards.

Mtoto mdogo zaidi wa Franklin, aitwaye Kecalf mwenye umri wa miaka 48, alizaliwa mwaka 1970. Jina lake linawakilisha kifupi cha majina kamili ya baba yake na mama yake - Ken E. Cunningham na Aretha Louise Franklin.

“Tumempoteza bibi, malkia na mwamba wa familia yetu,” familia ya mwimbaji huyo iliandika katika taarifa rasmi. “Upendo aliokuwa nao kwa watoto wake, wajukuu, wapwa, na binamu zake haukuwa na mfano.

“Tumeguswa sana na upendo wa ajabu na sapoti ambayo tumeipata kutoka kwa marafiki wa karibu, wafuasi na mashabiki duniani kote,” familia yake iliendelea kuandika.

"Asanteni kwa upendo na sala zenu. Tumeuona upendo wenu kwa Aretha na inatuletea faraja kujua kwamba alama yake itadumu. Tunapohuzunika, tunawaomba muheshimu faragha yetu katika wakati huu mgumu.”

Aretha alizaliwa Memphis na alianza kuimba kama muimbaji wa nyimbo za dini na mpiga kinanda na alikuwa muhubiri katika sherehe za ubatizo.
Franklin alianza kufundishwa katika umri mdogo kuwa nyota wa muziki wa dini kama ilivyokuwa kwa Mahalia Jackson na Clara Ward.

Alihangaika sana kupata umaarufu katika umri mdogo akiwa chini ya rekodi za Columbia ambazo zilijitahidi kuondoa aibu aliyokuwa nayo na kuiweka sauti yake inayovutia kuweza kung'ara duniani.

Mwanamuziki Elton Jon ameandika salamu zake za pole katika ukurasa wa instagram na kusema kuwa kifo cha Aretha Franklin kimeshtua kila mmoja anayependa muziki wa kweli.

“Sauti yake ilikuwa ya kipekee, jinsi alivyokuwa anapiga piano kwa ufanisi... nilimpenda na nilikithamini kipawa chake. Mungu ambariki na salamu zangu za pole kwa familia," aliandika Elton Jon.

No comments: