Aug 12, 2018

Tuitumie fursa ya burudani kukuza uchumi na kuongeza ajira

Diamond Platnumz akitumbuiza


“HATUPO katika kizazi cha taarifa na maarifa. Tupo katika kizazi cha BURUDANI na STAREHE.” Tony Robbins.

Tony Robbins ni mwandishi wa Marekani, mjasiriamali, mwalimu na anajulikana kwa matangazo yake kwenye runinga, semina na vitabu, ikiwa ni pamoja na ‘Unlimited Power’ na ‘Awaken the Giant Within’.

Burudani ni biashara inayokua kwa kasi sana barani Afrika zaidi ya kawaida. Sekta ya burudani imejaa fursa nyingi sana kupita kawaida. Yeyote atakayeamua kuichunguza sekta hii kwa makini atashangaa fursa zilizojaa.

Kila siku mamilioni ya watu duniani wanahangaika kutafuta sehemu za kustarehe, vitu vya kujistarehesha na kujiburudisha, michezo na matamasha ya kufurahisha.

King Majuto katika sinema ya Daladala

Sekta ya burudani inatengeneza zaidi ya dola  billioni 50 za Marekani kila mwaka. Sekta hii inaongoza katika kutengeneza ajira kuliko sekta zote barani Afrika.

Afrika ikiwa kama sehemu ya kivutio cha utalii, vipaji vya filamu na muziki bado vibichi. Dunia nzima inahamia Afrika kwa sababu Afrika inaendelea kukua na kukua katika sekta ya burudani.

Sekta za Filamu na muziki zimekua kwa kasi zaidi ya kawaida. Zimejaa vipaji visivyo na kikomo. Hii fursa bado mbichi sana Tanzania. Japo watu wanafanya muziki au kutengeneza filamu lakini sekta hii bado haijaguswa vya kutosha.

Pamoja na matatizo yake lukuki lakini ukichunguza waigizaji au waimbaji, kama akina Joti, Masanja Mkandamizaji, Diamond Platnumz, Ali Kiba n.k. wanaingiza pesa nyingi kwa mwezi kuliko hata wakurugenzi wa kampuni Afrika.

Wasanii katika burudani ni zaidi ya watu wa kawaida. Wapo juu ya kilele. Msanii katika burudani anaweza kuingiza pesa nyingi ndani ya dakika tano pesa ambayo mtu mwingine anaweza kuipata kama akikusanya pesa hizo tokea anapojitambua mpaka uzeeni.

Wao wanaweza kutengeneza ndani ya dakika tano na serikali inaweza kujipatia kodi kubwa hapa ikiangalia kwa jicho la kiuchumi.

Sekta hii imejaa pesa nje nje kuliko kawaida, lakini ukikutana na waigizaji wengi maarufu utasikitika kwa kuwa bado hawajagusa kabisa sekta hii.

Kuna uzembe fulani wa kufikiri hapa na wanajua hivyo. Hakuna malengo hapa. Kuna ubabaishaji uliopindukia. Hii ndiyo sababu tunawasikia wanatumika na wanasiasa.

Msanii wa filamu ni mtu mkubwa sana duniani, siyo mtu wa mchezo mchezo lakini wasanii wetu Mungu awasaidie maana hawajaamka, ndiyo maana hata soko la filamu ni kama limeparaganyika.

Wako wapi wafanyabiashara wajanja Afrika waweze kuichangamkia fursa ya filamu Tanzania? Watanzania wanatamani kuona filamu zilizobamba lakini hazipo sokoni.

Hakuna filamu nzuri sasa. Wasanii waseme wenyewe, mauzo ya filamu za Kibongo yakoje kwa sasa? Yameshuka kuliko kawaida. Hii haimaanishi kuwa Watanzania hawapendi filamu, ila ni kwamba filamu za maana ni chache mno kuliko maahitaji ya soko.

Hii ndiyo sababu filamu na series za nje, hasa za Kikorea, China na India zilizotafsiriwa zinabamba… hebu fikiria kama badala ya umaarufu wa series hizo, tufanye ingekuwa ni filamu mpya ya JB ni kiasi gani cha kodi serikali ingekusanya?

Lakini hao wanaotafsiri hizo filamu wanalipa kodi? Mnajua wanaharibu kwa kiasi gani sekta ya filamu Tanzania? Lakini tujiulize, kwanini hivi sasa filamu hizo zinatamba na kupata umaarufu? Ni kwa sababu wasanii katika tasnia ya filamu nchini walibweteka.

Walibweteka na kusahau kuwa sanaa ndiyo inayoweza kutengeneza pesa nyingi sana kuliko hata kazi za kuvaa tai posta.

Lakini hali hii si kwa Tanzania pekee, hata Nigeria (Nollywood) ambao mchango wa sekta ya filamu kwa Taifa ni Naira bilioni 853.9 (Dola bilioni 2.37 za Marekani) wamegusa kiasi kidogo sana katika sekta hii ya filamu Afrika.

Katika nchi kama Nigeria yenye matatizo ya ukosefu wa ajira, Nollywood peke yake imefanikiwa kuajiri zaidi ya watu milioni 1 (bila maharamia) na kuifanya sekta hii ya filamu kuongoza baada ya sekta ya kilimo.

Hii ni ishara ya jinsi gani sekta ya filamu inavyoweza kukuza na kubadili uchumi wa nchi yoyote, kwa njia ya utoaji wa ajira kama itachukuliwa kwa umakini mkubwa. Matokeo ya kukubalika kwa sinema pia huwafanya watayarishaji wa sinema, waigizaji na watendaji wengine kuwa na heshima kwenye jamii na hata kisiasa.

Mwanzoni Nollywood ilianza kama aina fulani ya wazimu wa kutengeneza ‘home video’ za bajeti ndogo.

Filamu zilitengenezwa na wafanyabiashara zaidi kuliko wanataaluma, na baadaye soko la ushindani likaanza kudai ubora na ndipo tulipoanza kuona filamu nzuri zikiibuka baadaye, kama ile ya Kunle Afolayan ya ‘The Figurine’.

Swali ni kwamba tupo serious au suala lilikuwa ni kupata umaarufu tu ili uweze kuwasaidia kwenye mambo mengine yasiyo ya kisanii, kama kukimbilia kwenye siasa? Nini kimetusibu jamani? Siasa?

Wapo wasomi wengi mitaani wamefungwa na vyeti vyao wakati wana vipaji lukuki na wana uwezo wa kuanzisha projekti za filamu Tanzania lakini wamebaki kukosoa tu na wengine kulala fofofo. Siku wakija kuamka watakuta kila kitu kimekwisha haribika.

Nimekutana na vijana wa kawaida sana hawajaenda hata shule, hawajui hata kuandika lakini waliweza kujiajiri kupitia filamu na walikuwa wanaingiza pesa kimchezo mchezo kuliko hata mameneja na wengi wao walimiliki kampuni tena nyingi zikiwa hata hazijasajiliwa.

Hebu fikiria, kama kungekuwa ana utaratibu wenye kueleweka nchi hii ingeingiza pato kiaso gani kupitia filamu pekee?

Waafrika wengi wanapenda starehe, Waafrika wengi tunapenda kuburudishwa na hii ni fursa kwa wasanii.

Fursa katika filamu na muziki ni zaidi ya kawaida hapa Afrika na hasa Tanzania. Waulize wazee wa fursa, wamiliki wa CMG, utashangaa pesa wanazoingiza.

Milango iliyofunguliwa na fursa hii ni mingi, cha ajabu watu ni wagumu kuingia: fursa hii imefungua milango mingine zaidi ya fursa nyingine.

No comments: