Mar 16, 2018

Zi wapi zama za vikundi vya sanaa?

Kikundi cha Sanaa cha TaSUBa wakifanya vitu jukwaani


DAH! Ama kweli siku hazigandi na maisha hayarudi nyuma! Maisha yakipita yamepita, japo historia ndiyo inayoweza kuturudisha nyuma tupendavyo. Enzi za uongozi wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na baadaye Ali Hassan Mwinyi kulikuwa na vikundi vingi vya sanaa, hasa vya sarakasi, maigizo, ngoma, mazingaombwe na kadhalika.

Vikundi hivi vilitoa burudani ya aina yake katika jamii husika, na watu walikuwa wakienda kwenye kumbi mbalimbali, hasa jijini Dar es Salaam na miji mikubwa mwisho wa wiki kupata burudani ya aina yake.

Nakumbuka kulikuwa na vikundi vya sanaa vya DDC Kibisa, Muungano Culture Troup, Makutano Dancing Troup, Ujamaa Ngoma Troup, Mandela Theatre, Bima Modern Taarab, Super Fanaka, Reli Kiboko Yao, JWTZ, Tancut Almasi, UDA, Urafiki n.k.

Pamoja na kutumbuiza kwenye kumbi mbalimbali, vipo vilivyokonga nyoyo kwa burudani na vichekesho vya papo kwa papo jukwaani na maigizo yaliyorushwa kwenye kituo pekee cha redio cha wakati huo, Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD).

Nakumbuka tukiwa wadogo tulizoea kusikiliza vipindi vya Mahoka au Pwagu na Pwaguzi vikirushwa na RTD, bila kusahau vipindi vya Twende na Wakati, Mzee Jangala n.k.


Kwa kweli hawa jamaa walikuwa vinara wa burudani kwa jinsi walivyoweza kupangilia vituko vyao japo tulisikia sauti tu bila kuwaona.

Pamoja na kutoa burudani murua vikundi hivi vilijenga uzalendo kwa vijana wa wakati ule. Hakika uzalendo kwa wakati huo ulikuwa juu, ila kwa sasa tunashuhudia anguko kubwa linalosababisha janga kubwa kwa Taifa.

Kwa kipindi kirefu tumekosa vionjo vya sanaa kutoka kwa vikundi kama hivyo... vikundi vingi kwa sasa ni vya kwenye runinga na si ukumbini ama stejini.

Watu wengi siku hizi wamekuwa wanaanzisha vikundi vya sanaa pasipo kuwa na malengo, wanakaa kutegemea runinga zirushe kazi zao, jambo linalowafanya wasanii kuhama vikundi mara kwa mara kila wanapoona hakuna uhakika wa kuonekana kwenye runinga.

Baraza la Sanaa la Taifa limekuwa linasajili vikundi vya sanaa kila kukicha lakini vikundi vingi vinakufa kwa muda mfupi pasipo kutimiza malengo waliyojiwekea kutokana na kukosa maono.

Kutokana na kukosa maono, imewapenyeza wenzetu Wachina na wa Mataifa ya Magharibi kwa kasi kubwa na sasa wamejizatiti katika kutangaza utamaduni wao. Kwa mfano, Wachina wana vikundi vingi vya sanaa na ndivyo vinawachangamsha wao.

Laiti tungejua umuhimu wa vikundi hivi, tungerudisha misingi ya utamaduni na sanaa (hili nitaliongelea vizuri siku nyingine), kwani wanasayansi wamekadiria kwamba kufurahi humuongezea mtu afya bora na maisha marefu.

Yapo manufaa mengi ya kufurahi ikiwa ni pamoja na kuongezeka mara tatu kwa kiasi cha hewa kinachovutwa ndani ya mapafu na vile vile kuboreshwa kwa mzunguko wa damu, umeng'enyaji na uyeyushwaji wa chakula, utendaji wa ubongo na kuondolewa kwa vitu vyenye kudhuru.

Hata baada ya kuanzishwa vituo vya televisheni miaka ya 1990, tulikuwa na vikundi vya sanaa vya kina Mzee Small, Mzee Majuto na kina Onyango na wenzake vilivyotuburudisha sana.

Mara wakaibuka Max na Zembwela na 'Mizengwe' yao na kutoa burudani kulingana na wakati. Kisha ikawa zamu ya Ze Comedy (EATV) ya kina Masanja, Joti, Mpoki na wenzao, kuuteka umma wa Watanzania kwa burudani ya aina yao.

Nchini Kenya bado wana utamaduni wa vikundi vya sanaa kuburudisha katika kumbi mbalimbali kila mwisho wa wiki.

Mchekeshaji maarufu wa Kenya, Daniel Ndambuki "Churchill"

Kwa mfano mchekeshaji Daniel Ndambuki, maarufu kama Churchill, huandaa vipindi vya runinga kama Churchill Show ambavyo kabla ya kurushwa kwenye runinga, ucheshi wa papo kwa papo jukwaani hufanyika kwenye ukumbi wa Carnivore jijini Nairobi.

Churchill Show imekusanya wachekeshaji wakongwe na wachanga, kwa ucheshi wa papo kwa papo jukwaani (stand-up comedy). Aina hii ya ucheshi Wakenya wamefanikiwa sana, tofauti na Tanzania.

Daniel Ndambuki kabla hajaanzisha Churchill Show alikuwa katika kundi la Ridiculous lililojulikana zaidi kama “Red Corna”, ambalo kundi la Ze Comedy waliiga ucheshi wa papo kwa papo lakini wakashindwa kabla hawajarukia kuigiza taarifa ya habari ambayo pia waliiga kutoka Red Corna ya Kenya.

Niliwahi kushuhudia jinsi Ze Comedy walivyokuwa wanahangaika kuchekesha papo kwa papo pale kwenye ukumbi wa Starlight!

Aina hii ya ucheshi wa papo kwa papo inahitaji uelewa mkubwa sana wa jambo unalotaka kuliigiza ili lichekeshe, kwani kichekesho kinategemeana sana na tukio la papo kwa papo au lililotokea!

Hii ni kwa sababu sisi Waafrika kwa sehemu kubwa hutumia ishara, mifano katika hadithi na matukio ya kuchekesha. Ucheshi kwa kawaida huwa na mwisho wenye kufurahisha, ingawa wakati mwingine unaweza kuegemea mambo yanayosisimua au mabaya.

Tanzania tunao wasanii wazuri lakini wamekosa mwongozo mzuri wa kuwafanikishia kazi zao.

Wasanii wetu wanatakiwa kuongeza wigo wa ubunifu na kujifunza zaidi kama wanataka kuendelea kutusisimua, aidha wanapaswa kufuatilia sanaa za wenzetu ikiwa ni pamoja na kununua kazi hizo, wawashirikishe wengine, wabadili mfumo, watafute maoni, watumie lugha sanifu, wazame ndani ya akili za watazamaji wao kujua mahitaji yao na wasome alama za nyakati.

Kila jamii ina utamaduni wa kipekee sana wa kuchekesha. Bahati mbaya Watanzania tumeathiriwa na mifano ya nje.

Vijana wa Tanzania wameshindwa kuelewa kwamba tunatazama vipindi vya nje kwa ajili ya kuangalia wenzetu wanafanyaje kazi zao lakini si kuiga, kwani si mwalimu mzuri kwetu.

Ndiyo maana natamani sana enzi za vikundi vya sanaa vya DDC Kibisa, Muungano, Makutano, Ujamaa, Mandela, Bima, Super Fanaka, na kadhalika zirudi.

No comments: