Jul 1, 2015

Filamu zinaweza kutumika kama tiba

·         Lakini pia zinaweza kuacha athari ya kisaikolojia

Wapenzi wa sinema wakisubiri kuangalia sinema katika moja ya
maonesho ya sinema kwenye viwanja vya Tangamano, jijini Tanga
TUPENDE tusipende, nyakati hizi za karne ya 21 tunalazimika kutumia vyombo mbalimbali vya mawasiliano, kama magazeti, simu, redio, vinasa sauti, televisheni, filamu, mtandao, n.k. Vyombo hivi vimechangia kwa kiasi kikubwa sana katika kuifanya dunia yetu kuwa ndogo sana. Tunaweza kuvitumia vyombo hivi kwa ajili ya kujielimisha na kujiburudisha ingawa kwa walio wengi, maendeleo ya vyombo hivi ni kama kitendawili. Kila wakati vyombo hivi vinakuwa vya teknolojia mpya na vya rahisi kutumia.

Dunia ya mawasiliano inaweza kuchochea ubunifu wa vijana, na katika njia zote za mawasiliano njia iliyo na ushawishi mkubwa ni sekta ya filamu. Katika zama zetu hizi, sinema ni chombo muhimu sana kinachotumiwa kueneza utambulisho, utamaduni na fikra. Filamu zinaweza kusaidia katika kujielimisha na kujiburudisha. Aidha, zinaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa kuleta mabadiliko ya kiutamaduni na kifikra, hasa kati ya vijana. Lakini uzuri au ubaya wa vyombo vya mawasiliano hutegemea na matumizi yake.

Filamu zina uwezo mkubwa wa kutengeneza hisia kuliko maneno ya moja kwa moja, ndiyo maana upo utofauti mkubwa kati ya ujumbe unaotumwa kwa njia ya wimbo na ule unaoweza kutolewa kwa njia ya sinema. Kama hilo halitoshi, kusahau maneno ni rahisi zaidi kuliko kusahau sinema, hivyo kutumia njia ya filamu kama chombo cha mawasiliano kunatajwa kuwa ni njia bora zaidi ya kutolea maelekezo.

Napenda filamu. Napenda jinsi zinavyoleta pamoja mambo mengi ya sanaa-fasihi, michezo ya kuigiza, upigaji picha, muziki nk. Ninapoangalia filamu, huwa najikuta natoka kwenye dunia yangu inayojulikana na kuingia kwenye dunia nyingine kabisa, napotelea katika sehemu tofauti; najikuta mimi ni kama mtu anayefurahia kuchungulia wengine (voyeur), nakuwa msafiri na shahidi wa kile ninachokishuhudia. 

Matukio ya kipicha (scenes) na misemo huniingia hadi chini ya ngozi yangu, hujizungusha katika ubongo wangu, na kujaa katika sehemu kubwa ya akili yangu kwa siku kadhaa—na hata kwa miaka mingi. Katika dakika 90 au 100 au 180 za sinema, naweza kuondolewa, kusafirishwa, au hata kubadilishwa kidogo katika maisha yangu yote. Nipe filamu yenye mazungumzo yaliyoandikwa na kupangiliwa vizuri, iliyohaririwa kiufundi zaidi, na picha zilizopigwa katika kiwango cha hali ya juu, huwezi kuamini nitajikuta nipo mbinguni.

Nilipokwenda kusomea tiba (medical), nilidhani ningepoteza hamu ya kuandika na kufuatilia filamu; Nilidhani nisingekuwa tena na muda wa kuandika au kufuatilia filamu. Kwa kiasi fulani, nilikuwa sahihi kwenye suala la kukosa muda; lakini vitabu na sinema vikawa kimbilio langu, riziki yangu na mtandao (connection) wangu katika ulimwengu kipindi hicho cha miaka yangu ya masomo. 

Filamu kama ‘The Thin Blue Line’, ‘Crimes and Misdemeanors’, ‘Cinema Paradiso’, ‘Lorenzo’s Oil’, na ‘Do the Right Thing’ zilinifundisha mambo mengi kuhusu haki, maadili, shauku, upendo, na kuhusu ubaguzi wa rangi kwa njia ambazo mafunzo yangu ya kawaida ya udaktari yasingeweza kunipa taarifa hizo. Tangu wakati huo nimetambua kuwa filamu hazikuwa tu kimbilio langu, bali zimeweza kuyajaza maisha yangu maarifa na taarifa nyingi wakati wa udaktari wangu. Nahisi imekuwa hivyo hata kwa wengine.

Sekta ya filamu nchini imefikia ilipo kutokana na msukumo mkubwa wa filamu za mwanzo zilizokuwa zinazogusa maisha halisi. Wavulana walio wengi hupenda kuangalia filamu za mapigano, na wasichana hupendelea zile za hadithi za mikasa halisi ya kimaisha. Kwenye televisheni, wavulana wanapenda kuangalia spoti, wasichana wanapenda sana tamthilia, hasa zinazohusu mahusiano ya watu wa jinsia tofauti. Ajabu ni kwamba, tamthilia za Kiingereza zinaonekana kupendwa zaidi kuliko zile za Kiswahili.

Pia filamu ndiyo aina ya mawasiliano inayochangia kwa kiwango kikubwa katika kuendeleza utandawazi, na katika usambazaji wa utamaduni wa kimagharibi. Hali hii imekuwa ikifanya familia nyingi na hasa watoto wamekuwa wakikatazwa na wazazi wao kuangalia sinema kwa fikra kwamba zinapumbaza na kupoteza muda, jambo ambalo wanasaikolojia wanapingana nalo.

Wakati nasoma tiba, nilipata kujifunza pia saikolojia. Ukisoma katika baadhi ya machapisho, wanasaikolojia wanabainisha kuwa kuna kitu tofauti na mtazamo wa walio wengi kuwa: kazi ya filamu si burudani pekee, bali ni njia yenye mafanikio makubwa katika kujifunza mambo na kutibu baadhi ya matatizo yanayowakabili wanadamu.

Japo kuna ukweli kuwa zipo baadhi ya sinema (zinazoonesha mauaji ya kikatili, unyanyasaji wa watoto au wa kijinsia) zinaweza kuwaharibu watoto, lakini dhamira kubwa ya sinema ni kufundisha na kutatua shida zetu. Kwani ndani ya filamu (iliyofuata misingi inayotakiwa) uanadamu wetu unakamilishwa kwa kujifunza kupitia kusikia, kuhisi na kutafakari, mambo ambayo yanapatikana ndani ya filamu.

Hakuna ubishi kwamba uchaguzi wa simulizi, visa na tungo zinazopatikana kwenye filamu ndiyo jambo pekee linalohitajika kuzingatiwa, hii ikiwa na maana kwamba kujifunza na kujitibu matatizo yetu kunaanzia kwenye kile tunachotaka kukitazama ndani ya filamu.

Upo ushahidi wa kutosha kuhusu watu wenye matatizo ya hisia za kimapenzi kumaliza ugonjwa wao kwa kutazama sinema za ngono huku wengine wakitajwa kujengwa kiimani, ujasiri na uvumilivu kupitia michezo ya kuigiza. Kwa msingi huo hatuwezi kupuuza utazamaji wa sinema kwani inawezekana kuihamasisha jamii yetu kuwa hodari katika mambo wanayoyaona yakitendwa na waigizaji.

Kupitia filamu tunaweza kuwapatia watoto wetu moyo wa kishujaa mithili ya michezo inayoigizwa na wasanii. Katika hali hiyo, si ajabu kusikia watoto wakijisifia mtaani: “Mimi Jack Chain”, “Mimi Rambo” au “Mimi ni Schwarzenegger”. Hii ina maana kwamba, filamu za waigizaji hao zimesaidia kwa kiwango kikubwa kuwajenga watoto katika ujasiri.

Kama hilo halitoshi wanasaikolojia wanaamini kwamba, mtu anaweza kujitibu mwenyewe tatizo la msongo wa mawazo kwa kuangalia filamu zenye ujumbe unaohusiana na tatizo lake na hivyo kujiongezea moyo wa ushindi kupitia waigizaji anaowatazama kwenye sinema.

Kwa mfano, mtu anaweza kuwa mgonjwa miaka sita na akawa katika hali ya kukata tamaa lakini akiletewa filamu inayomuonesha mtu mwenye ugonjwa kama wake akihangaika na hatimaye kupona, hata yeye atafarijika na kuamini kuwa ipo siku atapona kama yule muigizaji,s na hivyo kupata imani ambayo itamsaidia kuishi.

Jambo muhimu la kuzingatia ni kuwa makini na uchaguzi wa filamu tunazotaka kuziangalia. Ndiyo maana huwa zinawekewa madaraja na Bodi za Ukaguzi (Censorship Boards). Hakuna ubishi kwamba mtoto akizoezwa kuangalia filamu za kikatili atabadilika na kuiga tabia ya ugomvi, vivyo hivyo wanaopendelea sinema za ngono zitawashawishi kufanya kitendo hicho, lakini sinema za kuelimisha ni msaada mkubwa wa kukuza ufahamu wa watu.

Pia tusisahau kuwa zipo athari walau chache za matumizi ya vyombo vya mawasiliano, hasa kati ya vijana. Vyombo vya mawasiliano vimekuwa kama walimu wa kisasa. Kwa vile vijana wanashinda muda mwingi pamoja na vyombo hivi, vina uwezo mkubwa wa kuathiri fikra na tabia zao. Vyombo hivi vinaendelea kurusha mifano ya kuiga ambayo vijana wengi wanavutiwa kufuata, hivyo, kujifunza taarifa mbalimbali kirahisi na kupanua akili, lakini pia wanaweza kujifunza mambo mabaya.

Licha ya athari ya kijamii na kimaadili, filamu kama moja ya vyombo vya mawasiliano endapo haitatumika vizuri basi inaweza kuleta matokeo ya ajabu. Wataalam wanasema kwamba watoto ambao hawajaanza kwenda shule wakiona picha za televisheni uwezo wao wa kumsikiliza mwalimu darasani hupunguwa. Watoto siku zote wanatazamia vitu vinavyowavutia, wasipovipata wanakataa kujifunza.

Lakini kikubwa ni kuwa, filamu hutengeza ndoto za maisha, huleta ubunifu na kuamsha hamasa ya kufikia malengo yetu, hivyo si busara kuipuuza sekta ya filamu kwa mtazamo kuwa inawapotezea watu muda wa kutafuta mafanikio.

Alamsiki.

No comments: