Jul 20, 2015

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuiunga mkono ZIFF

Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuunga mkono  juhudi zinazochukuliwa na Uongozi wa Tamasha la Kimataifa la Filamu la Nchi za Jahazi  Zanzibar (ZIFF) katika azma yake ya kuijengea nguvu tasnia ya Filamu Nchini inayoonekana kusaidia ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya Utalii.

Kauli hiyo imetolewa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, katika Hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, wakati  akilizindua Tamasha la 18 la Kimataifa la Filamu la Nchi za Jahazi Zanzibar (ZIFF) hafla iliyofanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Double Tree By Hilton Shangani Mjini Zanzibar.


Wageni waalikwa wakimsikiliza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi (hayupo pichani), wakati wa ufunguzi wa Tamashala

Dk. Shein  alisema kwamba Tamasha la Nchi za jahazi limekuwa na mchango mkubwa katika kuitangaza Zanzibar Kimataifa hali ambayo imetoa ushawishi kwa wageni na watalii wengi kuamua kuvitembelea Visiwa vya Zanzibar kujionea mazingira na rasilmali zilizopo.

Alisema kupitia Tasnia ya filamu zinazotayarishwa na wasanii mbalimbali kwa kushirikiana na wadau wa Fani hiyo chini ya Wataalamu wa Ziff wageni na watalii mbalimbali Duniani wamekuwa wakivutiwa na fukwe pamoja na Utamaduni uliojaa ukarimu wa Watu wa Visiwa vya Zanzibar.

Rais wa Zanzibar aliushauri Uongozi wa ZIFF kuendelea kufanya juhudi zaidi za kuwashawishi wasanii wa Kimataifa kuzitumia Fukwe na Tamaduni za Zanzibar katika kutengeneza Filamu mbalimbali kwa lengo la kuitangaza zaidi Zanzibar Kimataifa.

“Zanzibar  ni Visiwa vya maumbile ya Utamaduni ya Ukarimu pamoja na fukwe za kuvutia mambo ambayo yakitangazwa vyema wasanii wa Kimataifa wanaweza kushawishika kuyatumia katika kutengeneza Filamu zao”. Alifafanua Dk. Shein.

Alifahamisha kwamba Tamasha la Kimataifa la Filamu la Nchi za Jahazi, Tamasha la Iddi, Tamasha la Mzanzibari pamoja na Sherehe za Mwaka Kogwa zinazofanyika Makunduchi ni Mambo muhimu yanayopaswa kuimarishwa katika kukuza na kusimamia Utamaduni na Historia ya Zanzibar na Watu wake.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi amewapongeza Wasanii wa Maigizo pamoja na Filamu Nchini kutokana na kazi kubwa wanayoendelea kuifanya ya kuelimisha Jamii sambamba na kuwapatia Burudani.

Alisema mbali ya Tasnia hiyo kutoa ajira pana kwa kundi kubwa hasa Vijana Nchini lakini pia imepanua soko la filam za nyumbani na kuleta unafuu kwa kila mtu kumudu kununua na kuangalia kazi za wasanii wa hapa Nchini hali iliyopelekea kufikia asilimia 80 ya filamu za Kiswahili zinazoangaliwa tofauti na miaka iliyopita nyuma.

Mapema Meneja wa Taasisi ya Kimataifa inayosimamia kukuza vipaji vya wasanii katika ukanda wa Afrika Mashariki (ZUKU), Bibi Maud Roger, aliahidi kwamba Taasisi yake itaendelea kukuza vipaji vya wasanii kwa lengo la kufikia kiwango kinachokubalika Kimataifa.

Bibi Roger alisema hatua hiyo muhimu itaweza kuwajengea uwezo wa kiajira badala ya kusubiri kutegemea zile za Serikali ambazo kwa sasa upo upungufu mkubwa hata katika Mataifa yaliyoendelea.

Meneja wa Taasisi hiyo ya Zuku alifahamisha kwamba mpango maalum umeandaliwa na Uongozi wa Taasisi hiyo baina ya miaka sita na kumi kwa kuwadhamini Vijana wapatao Kumi wanaopata Mafunzo ya msingi kuweza kutengeneza Filamu zitazokubalika Kimataifa.

Wakitoa salamu zao kwenye uzinduzi wa Tamasha hilo la 18 la Kimataifa la Filamu la Nchi za Jahazi Msanii Gwiji  Duniani kutoka Nchini Afrika Kusini, Leleti Kumalo, aliyeigiza filamu maarufu ya Sarafina pamoja na msanii mkongwe wa nchi hiyo, Doroth Masuka, wameelezea faraja yao kutokana na Serikali kupitia taasisi za kijamii zilivyojikita katika kusaidia vijana kwenye fani ya sanaa.

Akimkaribisha mgeni rasmi katika uzinduzi wa Tamasha la 18 la Ziff, Mwenyekiti wa Bodi ya Tamasha hilo, Mahmoud Thabit Kombo, alisema Ziff itaendelea kushirikiana na wadau wote wa ndani na nje ya nchi katika kuona Taasisi hiyo muhimu inazidi kuimarika.

Mahmoud Thabit Kombo alisema uimarikaji huo utawapa nguvu na ari Vijana walioamua kujiajiri kupitia Tasnia ya Filamu inayoonekana kupata umaarufu siku hadi siku hapa Duniani.

Uzinduzi wa Tamasha hilo la 18 la Kimataifa la Filam la Nchi  za Jahazi Zanzibar (ZIFF) limekwenda sambamba na siku yake lililoasisiwa rasmi Tarehe 18 Julai Mwaka 1997 likitimiza umri wa miaka 18 sasa.


No comments: