Jan 23, 2013

Kwanini tuendelee kufuata nyayo badala ya kuongoza?


Ousmane Sembène, gwiji wa filamu barani Afrika

MAMBO ni tofauti kabisa, kile kinachotokea Nigeria ni tofauti na kile kinachotokea Afrika Kusini, Tasnia ya filamu ya Misri inaonekana kuwa na kiwango cha mbali mno ukilinganisha na ile ya Kenya, na nikijaribu kufupisha mambo, ni kweli soko la filamu barani Afrika ni soko tata kidogo. 

Nchini Nigeria, nadhani kilichoanza kutokea kinaweza kuwa mfano kwa hali ya soko hapo baadaye: Nollywood ilianza kama aina fulani hivi ya watu mfano wa wazimu/mhemko wa video za bajeti ndogo, zilizotengenezwa na wafanyabiashara zaidi kuliko watengenezaji wa filamu, na baadaye soko la ushindani likaanza kudai ubora na ndipo tulipoweza kuona filamu nzuri sana zilizokuja kuibuka baadaye kama ile ya Kunle Afolayan ya ‘The Figurine’.

Watayarishaji wa filamu Afrika wameanza taratibu kuelewa haja ya kufanya vizuri zaidi. Nchi za Afrika zinazozungumza Kifaransa (Francophone) bado zinaonekana kutembeza bakuli hata kama filamu zinazotengenezwa katika nchi hizo zinavutia, na za kisanii. Ni nani analipa gharama za kuziandaa (sanaa hizi za hali ya juu) filamu hizi kutoka nchi makoloni ya Ufaransa? Ni nani anaziangalia?

Nadhani kwa sasa watayarishaji wa filamu hizi wanaanza kufikiria kuhusu hadithi wanazotaka kuelezea kwa watu wao, namna gani wataweza kuendelea kugharamia utengenezwaji wake, na kadhalika. Nimeanza kuiona hatua hii ya Afrika kama ni kipindi cha ‘mwamko wa kweli’. Sijui, au labda najaribu kuota ndoto ya mchana!

Tukiachana na filamu za Francophone, hali ya tasnia ya filamu nchini kwa sasa ni ya kusisimua sana. Kuna aina tofauti za watengenezaji wa filamu na aina mbalimbali za filamu zinazotengenezwa, ambayo ni kubwa. Nimeanza kuona watu wengi zaidi wakifanya majaribio kwa kutengeneza filamu fupi, filamu za makala (documentary) na filamu ndefu (feature films).

Tofauti ya maadili ya uzalishaji wa filamu, tasnia ya filamu nchini, ambayo ni kama majibu ya Watanzania kwa tasnia iliyokuwa imeshika kasi nchini mwanzoni mwa miaka ya 2000 - tasnia ya filamu ya Nigeria (Nollywood) – imeanza kuwa mahiri lakini kama ilivyo kwa Nollywood, tasnia ya filamu nchini bado inaendeshwa na wafanyabiashara.

Wafanyabiashara hao ndiyo wenye kudhibiti mfumo mzima wa usambazaji wa filamu zetu. Wanalielewa soko lao na wamekuja na mbinu zao za kukabiliana na uharamia wa kazi za sanaa na kwa namna fulani, wamekuwa wakiwafanya watazamaji wao kuelewa kwamba wanahitaji kununua kazi halisi – ambazo zinapatikana madukani kwao au kwa mawakala wao.

Wafanyabiashara hao wameigeuza sekta ya filamu nchini kuwa kitu kingine kabisa. Hawataki kuturuhusu sisi kama wajasiriamali kuamua hatma na mwelekeo wetu wa kwenda. Siku zote wanataka sisi tufuate nyayo tu!

Filamu hizi zinatengenezwa kwa bajeti ya chini mno ingawa zimefanikiwa kwa kiasi chake kuliteka soko la filamu katika nchi za Maziwa Makuu. Kwa upande mwingine, pia kuna filamu za bajeti kubwa, filamu ambazo hutengenezwa na kupelekwa kwenye matamasha ya filamu ya kimataifa – kama ‘Tumaini’ ya Beatrix Mugishagwe, ‘Chungu’ ya Vicensia Shule, ‘Chumo’ ya Jordan Riber na kadhalika.

Filamu hizi zinapaswa kuoneshwa kwenye majumba ya sinema, zimetengenezwa kisinema zaidi, zimetengenezwa kwa kuzingatia maadili ya utengenezaji filamu, lakini bado ukweli unabaki palepale kuwa watengenezaji wa filamu hizi hawalielewi soko lao au kuwa na mifumo ya usambazaji inayoweza kusaidia.

Nadhani soko filamu la kimataifa siku zote linahitaji filamu mpya zenye kujali masimulizi kutoka Afrika, Asia, India, Korea, na Ulaya ya Mashariki au kwingineko. Na hii imekuwa ikileta shida kidogo kati ya watazamaji wa ndani na wa nje, kwani soko la kimataifa linataka ladha tofauti kidogo na ile iliyozoeleka ndani. Ni mtengenezaji wa filamu wa Tanzania ambaye anapaswa kuangalia namna nzuri ya kuzalisha filamu zeenye kuzingatia maudhui mara kwa mara ili tuweze kuliteka soko la filamu ambalo litatusaidia kupata watazamaji wetu wenyewe wa ndani watakaonunua na kutuunga mkono kwenye filamu zetu.

Tunapaswa kuwa makini zaidi kwa kuangalia mahitaji yetu halisi na si mahitaji ya wengine, kwani hatuwezi kujenga sekta ya filamu kwa kulenga kutosheleza hitaji dogo la kimataifa, kwa kujifurahisha na kutaka kutambuliwa kimataifa bila kwanza kuanzia nyumbani. Hii imeleta shida kama ilivyokuwa kwa gwiji wa filamu barani Afrika, Ousmane Sembene, wa Senegal ambaye filamu zake zimesifiwa sana Ulaya na Marekani lakini zimekosa mvuto kabisa nchini kwake na kwa mataifa ya Afrika.

Mfano mwingine katika filamu za Kiafrika ni filamu iliyoshinda tuzo za Oscar ya Tsotsi ambayo pamoja na kukubalika nje ya nchi haikuweza kufanya vizuri na kufikia kiwango kizuri cha mauzo ya tiketi nchini Afrika Kusini, ukilinganisha na filamu ya Jerusalema ya Ralph Zimman, ambayo haikuwahi kupata tuzo ya Oscar lakini iliweza kufidia gharama ya uzalishaji wake kwa kutumia soko lake la ndani ya nchi.

Filamu ya Kunle Afolyan wa Nigeria, ya Figurine ilifanikiwa kurudisha nusu ya gharama ilizotumia za dola 400,000 kwa kutumia soko la ndani nchini Nigeria katika wiki chache tu. Filamu za aina hii zinapoingizwa kwenye mfumo wa DVD, mtengeneza filamu anakuwa katika wakati wa kutarajia kuingiza milioni chache, kwa sababu Wanigeria wanapenda sinema zao na wana idadi kubwa ya watu ndani ya nchi na hata ugenini ambayo hununua filamu.

Tatizo kubwa kwa nchi hizi za Kiafrika bado lipo kwenye upatikanaji wa fedha na usambazaji, mambo haya mawili ni changamoto kubwa sana kwa watengenezaji wa filamu Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Afrika Kusini imetuonesha yote jinsi tume ya filamu imara ilivyo muhimu kwa afya ya sekta imara ya filamu. Mamlaka yao ya filamu inajumuisha pamoja na upatikanaji wa fedha na mafunzo na watayarishaji wa filamu nchini Afrika Kusini wana fursa nyingi wakiishukuru tume na sekta ya filamu ambayo imefanya ushawishi mkubwa serikalini na ninaamini pia sekta binafsi za kibenki zinaitazama sekta ya filamu kama muwekezaji pamoja na uwezekano wa kutengeneza faida kubwa.

Unapoangalia filamu ndefu na fupi zilizoshinda tuzo zinazotoka Ulaya, Marekani na Canada mara moja utafahamu jinsi fedha nyingi zinavyopatikana kwa watengenezaji wa filamu katika nchi zao, hata kwa nchi zenye tasnia isiyo mahiri.
Hivyo serikali bila shaka ina jukumu na kufanya mara tu watakapotambua fursa kubwa ya kiuchumi kupitia sekta ya filamu kwa faida ya nchi na Hazina pia.

Lakini bado tatizo lipo, hata pale inapotokea fursa ya upatikanaji wa fedha za kutengenezea filamu kama ilivyokuwa kwa Mfuko wa Utamaduni, mfano inapoelezwa kuwa ni asilimia chache tu ya maombi yote yaliyotumwa yaliyobahatika kuchaguliwa, utatambua kuwa inaweza isiwe wale waliopata wamepata kutokana na ujuzi wao kama watengenezaji wa filamu, lakini imesababishwa na fursa ya upatikanaji wa fedha.

Lakini hebu pia tujichunguze wenyewe na kipi tunaweza kufanya. Sisi pia, kama watengenezaji wa filamu tuna jukumu la kufanya kujiunga na kusaidia vyama vya filamu ili kusimamia na kutetea kila aina ya msaada tunaouhitaji. Serikali zetu hapa Afrika zinatakiwa kubadilika kutoka kwenye usingizi wa pono na kuamka. 

Tunahitaji kuhakikisha kama nchi tunajiamini na kutambua kuwa hatuhitaji tena kuwa wafuata nyayo, bali tunatakiwa kuongoza pia harakati za kujikomboa. Ili kuongoza, tunapaswa kusoma machapisho mbalimbali ili kujua njia walizopitia wengine katika kuelekea kwenye mafanikio ya kweli ya tasnia ya filamu.

Baadhi ya wasomaji wazuri ulimwenguni ni waandishi na watunzi wa vitabu, na pia watengenezaji wa filamu, labda tunahitaji kuunda klabu ya filamu kwa ajili ya kubadilishana mawazo na DVD chache tulizonazo ili tuanze kufurahia kuzungumza pamoja kuhusu filamu na mwelekeo wa filamu kimataifa, hivyo kuwa sehemu ya udugu wa watengenezaji wa filamu. Lakini tusisahau kuwa tunahitaji kusoma zaidi pia.

Kusoma kutatuwezesha kupata taarifa ya mambo mengi - filamu, muundo na kadhalika. Tuna haja pia ya kuwa na ufahamu zaidi wa dunia na upekee wa hadithi zetu. Tunahitaji kuwa na imani katika mazingira au juu ya mchezo wetu.

No comments: