Katibu Mtendaji wa Basata, Ghonche Materego, akisisitiza
jambo kwenye moja ya midahalo ya Jukwaa la Sanaa
NI ajabu, wasanii kulia kilio
cha kuilalamikia Serikali kuwa haisaidii juhudi za wasanii katika masoko na
usambazaji kwa ajili ya filamu ambazo ni kwa maslahi kwa watazamaji wa Tanzania ,
kilio cha kuibiwa kazi za sanaa ingawa kuna uwezekano mkubwa wanaolia kutojua
wanaibiwaje kazi zao, lakini wanakwepa majukwaa ya upashanaji habari ambayo
yangetumika kufikisha kilio chao na kwenda kusemea pembeni.
Hili ni jambo la ajabu sana ! Ni kwewli mfumo wa
usambazaji ni mbovu, lakini wasanii wanadharau majukwaa muhimu ya habari na
hata vyama na mashirikisho yao
wakisahau kuwa umoja ni nguvu. Ikumbukwe kuwa utengenezaji sinema ni jambo
linalohitaji sana
mgawanyo wa kazi. Kuna waongozaji, waigizaji, waandishi wa miswaada na
kadhalika, huku msingi mkuu wa sinema yoyote ukiwa ni mwongozo (script).
Hakuna kisa kinachoweza
kuifanya sinema ipendeze bila kuwepo 'storyline' nzuri. Hii inamaanisha kwamba
endapo waandishi wa miongozo watafanya utafiti wa kina kwa kuwahusisha
watazamaji wa kazi zao kupitia majukwaa ya habari, basi soko letu litaweza
kukua zaidi na kuleta tija.
Majukwaa ya habari kama
lilivyo Jukwaa la Sanaa linaloendeshwa na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata)
kila Jumatatu ni jambo la kujivunia, na ni chachu ya kukua kwa Sanaa, kwani
Jukwaa la Sanaa ni programu inayomfanya mtu awe na upeo wa kusema, kwa kuwa
hapo hutolewa elimu, uratibu na mwongozo, hivyo wasanii wanatakiwa waitumie
fursa hiyo badala ya kuikwepa.
Waandaaji wa sinema pia
wataweza kujua ni nini hasa kinachoendelea katika hali halisi ya maisha ya
jamii kuhusiana na hadithi wanayohitaji. Hii itatokana na midahalo na mahojiano
na wadau wa sanaa na watu wengine kuhusiana na hadithi zenye kuakisi maisha
halisi ya jamii ambapo pia wataweza kuandaa takwimu ya watazamaji wanapokutana
nao katika dunia yao
kupitia Jukwaa la Sanaa.
Tatizo ni kwamba tumeingia
kwenye biashara ya filamu bila kujua vigezo muhimu vinavyoweza kutuongoza
katika dhana nzima ya mafanikio ya biashara ya filamu, kama
Jukwaa la Uwasilishaji (Media Delivery Platforms), lakini tunabaki kulalamika.
Nchi yoyote iliyofanikiwa
katika filamu watazamaji wake huhitaji majukwaa ya habari, sehemu ambazo
hukutana na waandaaji, wasanii na watendaji wengine ili kupashana habari.
Falsafa hii ni muhimu kama ambavyo tunapaswa
kulitumia Jukwaa la Sanaa ambalo Basata wametupa fursa kwa maana ileile ya
jukwaa la uwasilishaji, siyo tu kupashana habari bali hata katika kukuza biashara
ya usambazaji wa kazi za sanaa.
Jukwaa la uwasilishaji
katika dunia ya kisasa haliishii tu kwenye kupeana taarifa, linakwenda ndani
zaidi ya kile hasa soko la filamu linachotaka. Jukwaa husaidia kuwasilisha
mawazo kwa watu katika njia itakayojumuisha mitazamo yao .
Ufanisi katika uwasilishaji
huweza kuchangia utoaji haki ya kuchagua; yaani kuyaleta maudhui kwa watazamaji
katika dunia yao
wenyewe. Kulingana na uwezo mkubwa wa soko la Tanzania, Jukwaa la Sanaa kama
litatumika ipasavyo ni nyenzo muhimu sana na muafaka kumfanikisha kwa urahisi
mtengenezaji wa filamu kuendana na ushindani wa soko.
Tutake tusitake, ili tuweze
kupiga hatua tunahitaji nguvu kubwa katika utoaji habari za filamu na kujenga
jamii yenye wafuasi kupitia Jukwaa la Sanaa, na humo, mijadala inaweza
kujadilika, kipengele muhimu kabisa cha kuleta ufahamu au kampeni ya
kujitangaza.
Katika Jukwaa, watu wataweza
kupata habari zaidi, kushiriki katika mijadala, kujiunga na majarida, na
kubadilishana ujuzi na mawazo na watu wengine, kwa lengo la kupanua wigo mkubwa
wa watazamaji.
Hivi kwa nini tunaichezea
fursa nzuri kama hii tuliyoipata? Ni kweli
tunajua umuhimu wa majukwaa ya kupashana habari au tunadhani ni blah blah?
Tujiulize: kwa nini tasnia ya filamu Tanzania ambayo imeshamiri kwenye
teknolojia ya video, bado kuna ubabaishaji katika kuhakikisha sekta hii inakua?
Kudhani kuwa watazamaji wa
filamu wataendelea na mazoea ya kununua filamu kwa sababu tu zinapatikana au
kusambazwa, au watanunua filamu kwa sababu tu eti fulani na fulani wamecheza ni
kujidanganya. Tunahitaji kubadilika sasa.
Tunapodhani kuwa tunasukumwa
na uzalendo wa kutaka kuliokoa soko letu na majangili wa kazi za sanaa huku
tukipuuza jukwaa muhimu linaloweza kutufanya kupaza sauti zetu zikafika
tunakokutaka ni kujidanganya. Hili jukwaa linaandaliwa na taasisi ya serikali,
ni rahisi kwa serikali kusikia kilio chetu na kuyashughulikia matatizo yetu kama tutalitumia jukwaa kusema. Lakini ni vigumu kupata
ufumbuzi kama tunasemea uchochoroni ambako si
rasmi.
Ninachokiamini katika
ukombozi wa wasanii ni kutumia majukwaa ya habari na kuwa na Umoja wa kweli,
wenye nguvu utakaohakikisha kilichokusudiwa kinafanyika huku wanaoongoza
wanakijua na kunakuwepo mikakati endelevu katika ustawi na maendeleo ya sanaa.
Lakini badala yake wasanii wamelisusa jukwaa la upashanaji habari na kuishia
kulalamikia pembeni, wakijengeana chuki, majungu na ubinafsi miongoni mwao huku
wakilifanya jukwaa kuwa la wachache tu.
Kwa kutumia majukwaa ya
upashanaji habari itakuwa vizuri pia kuuchunguza mfumo wa usambazaji ili kupata
ufumbuzi wa kutangaza na kusambaza kazi ambao umesaidia sana
kurekebisha tasnia za filamu katika nchi nyingine, ili uigwe katika sekta ya
filamu Tanzania .
Tunasahau kuwa filamu ni ‘brand’, kama zilivyo
brand/ bidhaa nyingine, kuzitangaza na kuzisambaza ni vitu vyenye umuhimu sawa.
Lakini si kuzitangaza kwa njia tuliyoizoea ya kuzua skendo ‘feki’ kwenye
magazeti ili tuuze.
Kwa tasnia za filamu
zilizopiga hatua, filamu za kibiashara huanza na ‘Box Office’ (mfumo maalum
unaoanzia kwenye uoneshaji wa sinema ndani ya majumba ya sinema), kutolewa
katika njia ya sinema, baadaye kwenye video, kurushwa kwenye vituo vya
televisheni za kulipia, katika televisheni za umma, na hatimaye kwenye vyombo
vingine saidizi vya habari (video games, katuni na kadhalika) na mwisho
kutolewa kama bidhaa rasmi (DVD, VHS) kwa matumizi ya nyumbani.
Huu ni mfumo maalum wa
kimasoko nchini Uingereza, Marekani ,
India na hata
Afrika Kusini. Tunapaswa kuanza kujiuliza: kuna tatizo gani katika usambazaji
wa filamu Tanzania ?
Kuanzishwa kwa teknolojia ya digitali katika video na mafanikio yake na
kukubalika kimataifa kumefungua fursa mpya katika ulimwengu wa utengenezaji
filamu na utaalamu unaoambatana na tasnia hii.
Ukweli kwa sasa, studio
kubwa za Hollywood zinajaribu kurekebisha mgawanyo wao katika mfumo wa
usambazaji ili kwenda na wakati wa teknolojia ya video, mwaka 2004 mapato yaliyotokana
na mauzo ya DVD peke yake yalifikia Dola za Kimarekani bilioni 20.9
ikilinganishwa na dola bilioni 7.4 zilizotokana na tiketi za sinema kwa mwaka
huo.
Leo hii, imekuwa ni mkakati
wa kimasoko kutumia maonesho ya sinema kama
njia ya uzinduzi kwa ajili ya kutoa DVD. Kwa kweli filamu zilizooneshwa
zinafikia karibu asilimia 80 ya maktaba za video. Wengi wa watengenezaji filamu
huukwepa mfumo wa sinema na kwenda moja kwa moja kwenye DVD, kama ilivyo kwa
tasnia ya filamu hapa Tanzania .
Ukiachia njia nyingine
inayotumiwa kwenye nchi zilizoendelea ya kujenga jamii ya watazamaji kupitia
vyombo vya habari za mtandao (website) kwa kutoa makala, vipande vifupi vya
filamu (film clips), njia ya jukwaa la habari ni muhimu sana kufikisha ujumbe kwa watazamaji.
Na baada ya kupashana
habari kupitia majukwaa ya habari, tunapaswa kuanza sasa kuzionesha filamu
kwenye matamasha ya filamu jambo ambalo linaweza kusaidia sana kuongeza wigo wa taarifa. Matamasha ya
filamu husaidia kueneza taarifa miongoni mwa wapitiaji wa filamu na watazamaji,
na inaweza kuongeza umaarufu wa filamu na watazamaji kuwa wengi kama mapitio yake yatakuwa ya kuvutia.
Wakati sisi tukiendelea
kukaa katika ulimwengu wetu wa 'uvivu wa fikra' sehemu nyingine ya dunia
inasonga mbele kwa kasi zaidi kwa kutumia majukwaa ya habari kuliko
tunavyodhani.
Hii imekuwa njia nzuri yenye
kuleta faida kama tunavyoweza kuona maendeleo
kupitia masoko ya nchi zingine. Uwezo wa kiuchumi ni suala lililo nje ya
mtazamo wetu na matarajio ya watayalishaji kuendelea kujenga maudhui
yatakayoambatana na uelewa huu yanapaswa yaanze sasa kwa kutumia majukwaa ya
habari.
Nawasilisha.
No comments:
Post a Comment