Jun 8, 2016

Mgogoro TAFF ni vita vya panzi, furaha kwa kunguru

Kutoka kushoto; Katibu Mtendaji wa BASATA Godfrey Mungereza, Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Joyce Fisoo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole Gabriel, na Rais wa TAFF Simon Mwakifwamba. Hii ilikuwa ni siku ya uzinduzi wa Tuzo za TAFA

NIKIWA sijui hili wala lile hivi karibuni nilijikuta natumiwa ujumbe wa WhatsApp kwenye simu yangu kutoka kwa mdau mmoja wa filamu. Ujumbe ambao nilipoutazama kwa makini nikagundua kuwa haukuwa umeandikwa na mdau aliyenitumia bali ama alitumiwa au aliukopi kutoka kwa mdau mwingine.

Ujumbe huu uliandikwa hivi: “Habari? Mungu hulipa hapa hapa, tulimpakazia Bishop kila aina ya hila kulinda mambo yetu lakini tukajiona washindi bila kujua dhambi kubwa tuitendayo itatuhukumu tulipo. Kwa tatizo hili la Tanzanite film festival, Katibu tena atang’oka? Nasubiri muujiza. Hongera sana ndugu yangu Bishop, dhuluma uliyofanyiwa inawahukumu.”


Ujumbe huu ukanifanya kutafakari sana nini maana yake kwa kuwa sikuwa najua kile kilichokuwa kinaendelea kwenye sekta ya filamu, hasa baada ya mimi kuamua kukaa kando na kutokujishughulisha tena na masuala ya wasanii wala harakati za vyama vyao.

Katika kufuatilia kwangu nikaambiwa kuwa kuna mtafaruku mkubwa umeibuka ndani ya Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), baada ya Bodi ya shirikisho hilo kumtuhumu kiongozi wake mkuu, Simon Mwakifwamba, kuwa na tabia ya kufanya maamuzi pasipo kufuata katiba wala kuishirikisha bodi yake. mtafaruku huu umechangiwa na uzinduzi wa tamasha la filamu la Tanzanite uliofanyika jijini Arusha, ambapo Bodi ya TAFF imedai kuwa kiongozi wao anatumia mwamvuli wa shirikisho kujinufaisha binafsi.

Siku chache baadaye nikatumiwa jumbe nyingine mbili-tatu za WhatsApp kutoka kwa wadau tofauti, kati yao mmoja akinukuu makala moja yenye kichwa cha habari “Waliokimbia harakati za TAFF kwa mwenendo mbovu na fitina za rais.”

Katika makala hayo mambo mengi na ya kushangaza yalitajwa kuhusiana na tuhuma za kiongozi wa TAFF, Simon Mwakifwamba, na namna ambavyo amekuwa akifanya njama za kuhakikisha wale wanaoonekana kuwa tishio kwake wanang’olewa ili afanye mambo yake kwa uhuru. Ikatajwa orodha ndefu ya viongozi walioondoka au kuondolewa katika nafasi zao ndani ya shirikisho, wakiwemo makatibu wakuu wawili, makamu wa rais na wajumbe wa bodi kadhaa.

Makala hayo yanaendelea kupasha kuwa ndani ya harakati za wasanii kuna unafiki mkubwa kwani lile kundi la watu waliokuwa wakimuunga mkono kiongozi huyo mkuu wa TAFF, sasa wamegeuka na kuanza kumshambulia wakitaja tuhuma zake nyingi alizozifanya miaka ya nyuma, eti hana msaada katika sekta ya filamu! Kama hiyo haitoshi, nikapigiwa simu na wadau kadhaa wakitaka kujua msimamo wangu kuhusu sakata hili.

Jibu langu lilikuwa rahisi tu, sijui chochote na sitaki kujua kichoendelea kwa kuwa sina maslahi yoyote kutoka upande wowote wa mgogoro huo. Nilisema hivyo nikijaribu kupima faida na hasara za malumbano haya, maana huko nyuma kumekuwepo malumbano ya muda mrefu kati ya Mwakifwamba na lililokuwa kundi la Bongo Movies Unit, ambayo hayakuwa na tija zaidi ya kuchafuana. Nikakumbuka ule usemi wa “vita vya panzi ni furaha ya kunguru.”

Sekta ya filamu imesheheni utajiri mkubwa sana lakini inaongoza kwa wadau wake kuwa fukara (kwani imefukarishwa makusudi na watu wachache) na inazongwa na matatizo makubwa. Ni sekta inayoshika namba moja kwa migogoro. Tathmini nyingi zilizofanyika na zinazoendelea kufanyika zinabainisha kuwa chanzo kikuu cha matatizo haya ni kukosa dira, unafiki mkubwa miongoni mwa wasanii na wadau wa filamu na mgawanyiko miongoni mwao.

Siku zote nimekuwa naamini kabisa kuwa misuguano baina ya wasanii nchini imekuwa inawafanya wawekezaji waliokuwa tayari kuwekeza katika sekta ya filamu kusita kuingia kwa sababu kukosekana kwa umoja (maelewano), hili ni tatizo kubwa linaloathiri sekta nzima ya filamu kwa ujumla na kufanya utendaji kazi kuwa mbovu.

Utengano ni tatizo ambalo hata aliyekuwa Waziri wa Habari Vijana Utamaduni na Michezo, Dk. Emmanuel Nchimbi, aliwahi kuthibitisha kulijua. Hili tatizo mara nyingi huchangiwa kwa kiasi kikubwa na kukosa uelewa, kukosa dira, kutokuwewepo malengo, kuwa na mipango mibovu na uchoyo usiokuwa wa lazima.

Pia husababishwa na kutokujiamini kwa baadhi ya wasanii, watayarishaji na hata viongozi ndani ya harakati za filamu nchini. Ukweli ni kwamba wapo watu wachache wanaofaidika kutokana na mgawanyiko huu, na kusababisha soko la filamu kuparanganyika na watu walioko sokoni kujaribu tu kupata faida iliyo kubwa zaidi bila kuangalia upande wa pili unafaidikaje. Kwa maana hiyo, mgawanyiko unachochewa zaidi na uchoyo na ubinafsi.

Pamoja na kuwepo malumbano kwa kipindi kirefu, lakini hali ya malumbano ya sasa imechukua sura mpya baada ya kujitokeza makundi mawili, moja ni la wanaotaka kumng’oa kiongozi wa TAFF, ambao wamefikia hatua ya kudai haki yao kwa kuupeleka mgogoro huu kwenye ngazi za juu serikalini, na kundi la pili linaona kuwa kuna chuki binafsi na kwamba kiongozi huyu anaonewa.

Ilinishtua sana juzi (Jumatano) baada ya kupokea simu kutoka kwa mtendaji mmoja serikalini akiniuliza kuhusu mgogoro huu ambao kwa maelezo niliyopewa ni kwamba kwa sasa umetua katika Ofisi ya Makamu wa Rais!

Baada ya kutafakari sana kuhusu malumbano haya na hatua zinazochukuliwa nikajikuta najiuliza maswali mengi ambayo sikuwa na majibu, ingawa pia nilijaribu kuwauliza baadhi ya wadau wa kundi linalotaka kiongozi wao ang’oke.

Nilijiuliza kuwa kama tuhuma za kiongozi huyu wa TAFF zimekuwa zinafahamika kwa kipindi kirefu (si za jana wala leo), na huko nyuma ziliwahi kufanyika juhudi za kutaka kumuondoa madarakani, na badala yake katibu wake akatolewa kafara. Je, kwanini hawa wanaotaka kumng’oa waliamua kumchagua kwa kura za kishindo (asilimia 97) katika uchaguzi wa hivi karibuni kama walijua kuwa si muadilifu?

Katika kipindi kisichozidi mwezi tangu kiongozi huyu achaguliwe, zikaanza juhudi za kutaka kumng’oa (tena kutoka kwa walewale waliompigia kura)! Je, hawaoni kama tuhuma wanazozielekeza kwa kiongozi wao zitatafsiriwa kama ni chuki binafsi? Inawezekanaje mtu awe na tuhuma mbaya kwa miaka minne, kisha ndani ya kipindi kifupi cha uchaguzi tuhuma zifutike na mara tu baada ya uchaguzi kupita tuhuma ziibuke upya (tena kutoka kwa walewale waliompa sifa kemkem na kumchagua kwa kishindo)?

Kwa maswali haya na mengine nikaukumbuka wimbo wa msanii mmoja wa Bongo Fleva, 20 Percent wa “Ya Nini Malumbano”. Nilidhani baada ya kambi mbili zilizokuwa hasimu (za TAFF na Bongo Movies) kuungana na kufanya uchaguzi basi wangefungua ukurasa mpya, hasa baada ya sisi wengine kuonekana huenda tulikuwa kikwazo, kumbe ni mwanzo wa mgogoro mpya!

Hivi migogoro hii itaisha lini? Ingawa mimi si mtabiri lakini nauona mwisho wa mgogoro huu kuwa mbaya zaidi ya ilivyowahi kutokea kabla. Mgogoro na malumbano yaliyopo sasa hayaishii kuwachafua wale wanaolengwa tu, bali yanaichafua sekta nzima ya filamu, na hivyo wote waliomo ndani ya sekta ya filamu kuonekana hawajitambui.

Kwa mtazamo wangu, nadhani walikuwa bado wana nafasi ya wao wenyewe kukaa na kuzungumza mambo yao kwenye vikao vyao vya ndani na kufikia muafaka, badala ya njia hii ya kuanika matatizo na tuhuma zao kwenye mitandao na hata kuandika barua kwenye wizara na idara za serikali kuelezea matatizo yaliyomo ndani ya chombo chao.

Hebu tujiulize; nani mfaidika wa mgogoro huu? Kwa vyovyote si kundi la kiongozi anayetakiwa kung’oka wala kundi la wale wanaokusudia kumng’oa madarakani. Kinachokwenda kufanyika sasa kwa makundi yote mawili ni “bora tukose wote”. Ninashuhudia mikakati mizito na muda si mrefu tutashuhudia watu wakianza kugawana mbao!

Ni bora kuangalia mustakabali wa sekta ya filamu kwa maendeleo ya filamu badala ya kuongozwa na maslahi binafsi, maana yeyote atakayeshinda katika mgogoro huu asifikiri atadumu milele. Huo utakuwa ni mwanzo wa vita mpya!


Alamsiki.

No comments: