Aug 12, 2015

Uchaguzi 2015: Hivi Wasanii wamebeba ajenda gani?

* Waepuke kuendelea kutumiwa kisiasa
Msanii maaruf wa filamu, Jacob Steven (JB) akiwa kaongozana na
Rais Jakaya Kikwete, Katibu Mkuu wa CCM, Abrahman Kinana,
mgombea urais kupitia CCM, John Magufuli na viongozi wengine,
siku wasanii walipofanya sherehe kumuaga Rais Kikwete katika
Ukumbi wa Mlimani City

“TUMEPATA mafanikio ya kuridhisha kwa upande wa sanaa za filamu na muziki. Vijana wetu wa tasnia hizi wamekuwa wanafanya vizuri kiasi kwamba leo hii Bongo Flavor na Bongo Movie zimevuka mipaka ya Tanzania. Zinaitangaza sanaa ya Tanzania, lugha ya Kiswahili pamoja na nchi yetu. Vijana hawa wameitoa kimasomaso Tanzania na kutufutia unyonge tunaopata kwenye michezo. Tasnia hizi zimeajiri vijana wengi, wanalipa kodi na wanasaidia sana katika kuhamasisha na kufikisha ujumbe kwa mambo muhimu katika jamii.”


Maneno haya yalisemwa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete, katika hotuba yake wakati wa kuvunja Bunge la Kumi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuagana na Wabunge, katika Ukumbi wa Bunge, Dodoma mnamo 9 Julai 2015. Hii si mara ya kwanza kwa Rais Jakaya Kikwete kutoa kauli za aina hii zenye kutia matumaini kuhusu sekta za filamu na muziki.

Ni kweli, kwa kiasi fulani kuna mafanikio katika sekta za filamu na muziki. Ni kweli filamu na muziki vimevuka mipaka ya Tanzania (japo zimeishia ndani ya mipaka ya ukanda wa Afrika Mashariki). Ni kweli, filamu na muziki zinaitangaza sanaa ya Tanzania, lugha ya Kiswahili pamoja na nchi yetu. Lakini, mafanikio haya yanaweza yasionekane kwa sababu yanawabeba wasanii wachache sana, ukilinganisha na idadi ya wasanii wote nchini.

Hali iliyopo sasa, wapo wasanii wachache mno (wa filamu na muziki) wanaopata ‘promo mbuzi’ kwa sababu maalum. Wanapewa promo ili watumike kuuhalalisha mfumo dhalimu uliopo, hao ndiyo huwaponda wenzao wanaolalamika kuwa hawauzi, kwamba muziki wao au filamu zao hazikubaliki ndiyo maana wanaponda mfumo.

Kwa kawaida wanaotumika kutuliza upepo ni wachache sana, kwani kwa Tanzania hakuna msanii anayeweza kusimama na kujisifu kwamba anakula halali kulingana na wingi wa jasho lake. Kila mmoja anatambua kuna mfumo kandamizi, mfumo unaonyonya jasho la wasanii. Ila nafuu kidogo inatumika kusaliti wenzao.

Haya yanajulikana, ndiyo maana natoa wito wa uwepo wa soko huria, wasanii wa Tanzania wafanye biashara bila longolongo, watengeneze fedha, wafikie daraja la kuitwa matajiri – kama sekta yenyewe ilivyo tajiri – ili tuone raha yake.

Wasanii wapovuna stahili ya jasho lao na kutengeneza fedha za kutosha, inaweza kupunguza msongamano wa wananchi wanaojibana kutibu njaa katika sekta isiyo rasmi, kwani wengi wa waliopo huko, wana vipaji sana lakini hawavitumii kikamilifu kwa kuona na kuamini kwamba maisha kwenye sanaa ni magumu na hayalipi.

Pamoja na kauli za mara kwa mara za Rais Kikwete, kwamba sekta za filamu na muziki zinakua, lakini bado hatuoni kuwepo utashi wa kisiasa na hivyo kuzifanya kauli hizi kuwa sawa na porojo tu. Bado sekta hizi zinaendelea kutambuliwa kama sehemu ya utamaduni na burudani tu, na si sekta rasmi za kibiashara na chanzo muhimu cha kichumi kama ilivyo kwa nchi zingine.

Pamoja na ripoti ya Shirika la Hakimiliki Duniani (WIPO) ya mwaka 2012 kuonesha mchango wa mapato uliotokana na shughuli za Hakimiliki (sanaa) kuwa zaidi ya mchango wa Sekta ya Madini, au mchango wa ajira katika kazi zilizotokana na Hakimiliki kuwa zaidi ya madini, umeme, gesi, maji, usafirishaji, mawasiliano, ujenzi, afya, na ustawi wa jamii; inasikitisha kuona bado sekta hii inaendelea kuwa duni siku hadi siku.

Naamini kuna uchumi mkubwa sana ndani ya sanaa ila imekuwa vigumu sana kuuona au hata kuufikia kama soko lake linakuwa limebanwa. Lazima kwanza soko liwe jepesi na huria, wasanii watengeneze fedha na hapo ndipo itakuwa rahisi kuona manufaa mapana ya kiuchumi ndani ya jamii na taifa kwa jumla.

Ni wakati mwafaka sasa itambulike kuwa sanaa ni fedha, na sanaa ni uchumi. Sanaa inatosha kuwa mkombozi wa bajeti za serikali na kutoa mchango wa thamani katika Pato la Ndani la Taifa (GDP) na jumla katika Pato la Taifa (GNP).

Ni wakati mwafaka sasa, unapotembelea shuleni na kumuuliza mwanafunzi wa shule ya msingi au sekondari, matarajio yake nini kwa maisha yake ya baadaye, naye ajibu kuwa yeye ana kipaji, kwa hiyo anatamani kuwa msanii maarufu wa kimataifa, mwenye mafanikio na kutengeneza fedha nyingi. Msanii kwa kawaida mkondo wake ni maisha ya burudani. Starehe kwa sana!

Ni vigumu leo hii, umuulize mtoto anataka kuwa nani baadaye, naye akujibu kwamba anaota kuwa msanii mkubwa kwa sababu anapozungumza na wazazi wake, wanamwambia kazi nzuri ni Uinjinia, Udaktari, Urubani, Ubunge na ajira nyingine ambazo ni rasmi kwa sasa.

Mzazi mwenyewe anajua kwamba wasanii wanahangaika na njaa (wanaishi maisha ya kuigiza yasiyo na uhalisia). Hii ndiyo sababu mpaka leo, kila unapomuuliza swali msanii anayetambulika, alipotoka mpaka kufika alipo, atakwambia kwamba wazazi wake hawakutaka kabisa awe msanii. Si kwa sababu ni fani mbaya la hasha! Wanaona sanaa ni kupoteza muda, ni uhuni tu! Laiti wangeona mafanikio ya wasanii, wasingewakataza watoto wao hata kidogo.

Ifike wakati sanaa iwe ndiyo kimbilio la vijana wenye vipaji, na wazazi waone fahari kuwaunga mkono watoto wao pale wanapoona wanaonesha vipaji wakiwa wadogo kwa sababu ya kuamini kwamba watakuwa watu mashuhuri na wenye utajiri mkubwa.

Angalia Marekani: Mama yake Justin Bieber, alipoona mwanaye ana kipaji cha muziki, alimnunulia gita kwa sababu ya kuamini mwanaye anapita njia ya mafanikio. Leo hii anafaidi matunda ya kipaji cha mtoto wake. Ifike wakati, wazazi wote wawe na imani hiyo na wawekeze kwenye vipaji vya watoto wao.

Biashara ya sanaa inaposhika nafasi stahiki na kujaa kwenye mifereji yake, inaweza kuchangamsha ubunifu kwa watu na kufanikisha kutengeneza ajira, badala ya kufikiria kuajiriwa tu. Mafanikio hasi ya wasanii wa Tanzania, ni sababu ya vipaji vingi kupotea.

Watu wanashindwa kufikiria na kubuni njia ya kutengeneza fedha kupitia sanaa kwa sababu ya kuona jinsi wasanii wanavyoishi kwa tabu. Inahitaji mtu mwenye akili ya uthubutu kama mwendawazimu, ndiye anaweza kuona kitu fulani hakilipi na kimewapotezea dira wengi, kisha naye akifanye kwa kuamini kitampa mafanikio.

Ni ndoto ya kila mtu kuwa na maisha mazuri, kwa hiyo watu huangalia maeneo ambayo yanalipa. Mathalan, huko nyuma ilikuwa ndoto ya kila mtoto kuwa daktari, injinia na rubani kwa sababu ilionekana ndiyo mafanikio yanayotazamika na kupigiwa mfano. Siku hizi, vijana wengi wanatamani kuwa maofisa wa TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania) au Uhamiaji, kwa kuwa ndiko kunakoonekana kuna fedha nyingi za haraka.

Ni wazi kwamba hapa Tanzania inawezekana kabisa kufikia hatua nzuri na kuona matokeo ya faida ya sekta ya filamu, na sanaa zingine, katika ukuaji wa pato la taifa na la wasanii wenyewe kama wasanii watafanikiwa. Kujitangaza inahitaji fedha, msanii wa Kitanzania hawezi kujulikana kila kona ya Afrika, Ulaya, Asia, Marekani, Australia na kwingineko kama hajitangazi. Na bila mikakati mizuri, ikiwemo pesa atajitangaza vipi?

Huu ni wakati mwafaka kwa mamlaka za Utialii kama Tanapa, Bodi ya Utalii na kadhalika, kuamua kwa dhati kabisa kuwawezesha wasanii wa Tanzania, wadhamini kazi zao, watengeneze fedha na wawasaidie kwenda kujitangaza nje ya nchi. Baada ya hapo kutakuwa na matokeo yanayoonekana.

Alamsiki.

No comments: