Wachekesha maaruf nchini, marehemu Hussein Mkiety (Sharomilionea) na Amri Athuman maaruf KIng Majuto
NILISHANGAA binti yangu, Magdalena, 10, aliposema siku hizi hapendi kuangalia comedy
za Tanzania akidai hazichekeshi. Comedy ni neno la Kiingereza lenye asili ya
Ugiriki likimaanisha futuhi au ucheshi kwa Kiswahili. Ni vichekesho vyenye
lengo la kufurahisha, kufundisha na kuburudisha watazamaji, katika televisheni,
filamu, na kwenye majukwaa. Unapocheka ndivyo maisha yanavyokua bora zaidi!
Ucheshi
ni mwanga unaouangazia moyo, ni igizo lililobuniwa kuchekesha, kuburudisha, na
kumfanya mtu astarehe. Muundo wa ucheshi ni kuzidisha hali ya mambo ili kuleta
uchekeshaji, kwa kutumia lugha, matendo, na hata wahusika wenyewe. Ucheshi
huhoji na kufuatilia yalipo mapungufu, makosa au hitilafu, na vitu vinavyokatisha
tamaa ya maisha, na kuleta uchangamfu na wasaa wa kufurahia maisha.
Kuna
wakati comedy zilijizolea umaaruf mkubwa nchini na kufanya vijana wengi kuingia
kwenye sanaa ya vichekesho. Hata hivyo, ucheshi haukuanza leo, nakumbuka nikiwa
mdogo tulizowea kusikiliza Mahoka, na vichekesho vya Pwagu na Pwaguzi
vikirushwa Redio Tanzania, hakuna shaka kuwa hawa jamaa walikuwa vinara wa
vichekesho kwa jinsi walivyoweza kupangilia vituko vyao japo tulisikia sauti
tu.
Na
waliokwenda kwenye kumbi mbalimbali hasa Dar es Salaam na miji mikubwa walishuhudia
vikundi vya sanaa kama Kibisa, Muungano, Mandela, Bima, vikundi vya Jeshi nk.
kwa kweli walifurahia vichekesho vya kina King Majuto, Branco Minyugu,
Bartholomew Milulu na wengineo. Ukija kwenye magazeti pia ungekutana na
Chakubanga na Polo, na Kingo. Pia jarida la Sani lenye vikaragosi kama Kipepe,
Madenge, Pimbi, Sokomoko, Ndumilakuwili, Lodi Lofa nk.
Wachekeshaji
ni wasanii wenye umuhimu wa aina yake katika jamii. Ndiyo hutufanya tusahau
uchungu wa maisha kwa jinsi ambavyo wanatuvunja mbavu tukiwasikiliza redioni,
kuwaona kwenye televisheni au hata kukutana nao mitaani.
Miaka ya
1990 baada ya kuanzishwa vituo vya televisheni, viliibuka vipindi vya ucheshi vya
kina Mzee Small, Mzee Majuto, na Onyango na wengine, ambao nikiri kuwa
walituburudisha sana. Baadaye wakaibuka Max na Zembwela na 'Mizengwe' yao na
kutupa burudani kulingana na wakati. Baada ya kifo cha Max, Zembwela na
Mizengwe walianza kuchuja, ndipo wakaibuka Ze Comedy (EATV) waliouteka umma wa
Watanzania kwa vichekesho na staili ya aina yake.
Ndipo
kukaibuka wasanii na vikundi vingi wanaoigiza kinachoitwa vichekesho kwenye TV
na filamu kila kukicha. Lakini kwa sasa wachekeshaji wetu wanachoigiza sidhani
kama kinapaswa kuitwa vichekesho bali mizaha.
Komedi
kwa kawaida imegawanyika katika mifumo ya aina kuu mbili: comedian-led (wachekeshaji), kwa
kutuletea kichekesho kilichopangiliwa vizuri, utani au michoro na situation-comedies (sit-com) ambayo
huelezea kisa kilichomo ndani ya hadithi inayosimuliwa.
Sikatai,
Tanzania tunao baadhi ambao ni wachekeshaji wazuri sana lakini wamekosa
mwongozo.Ila nyingi ya hizi zinazoitwa komedi zipo kwenye ‘stage’ ya mwisho ya
'mzunguko wa maisha'. Mzunguko wa maisha hufuata vielelezo vinne: kuzaliwa,
kukua, kukomaa na kuzeeka kabla ya kifo, mwanadamu hufa baada ya stage hizo,
lakini komedi kama wachekeshaji wakitambua kwamba vichekesho vyao vinaboa
wanaweza kufanya kitu fulani na ikazaliwa upya na kufuata tena ngazi hizo.
Wachekeshaji
wetu wanapaswa kuongeza wigo wa ubunifu na kujifunza zaidi kama wanataka
kuendelea kutusisimua, aidha wanashauriwa kufuatilia vichekesho vya wenzetu,
wawashirikishe wengine, wabadili mfumo, watafute maoni, watumie lugha sanifu,
wazame ndani ya akili za wateja wao kujua mahitaji yao na wasome alama za
nyakati.
Kinachoua
sanaa ya ucheshi ni pamoja na kukosa ubunifu, dharau, kukosa malengo, kutojua
watazamaji wanataka nini, na kulewa umaarufu. Vinginevyo ni bora turudi kwenye
visa na vituko vya kina Ndumilakuwili, Kipepe, Lodi Lofa, Madenge, Pimbi,
Kifimbo Cheza, Sokomoko na wengineo.
Alamsiki.
No comments:
Post a Comment