Sep 13, 2014

Unachokiandika kinakutafsiri ulivyo


 
IMEANDIKWA, “Kila siri iliyo moyoni kwa mwandishi, kila aina ya maisha aliyoyapitia, au kipimo cha akili ya mwandishi vimeainishwa kwa kiasi kikubwa katika maandishi yake...” hii inamaanisha kuwa kazi za kimaandishi za waandishi huwaonesha wao ni kina nani, wametokea mazingira gani, wana uwezo gani wa kufikiri na wanataka kuwa nani.

Kupitia kujielewa wenyewe na kuridhika katika uasili wetu, mchakato wa kuandika huwa unakuwa wa hiari zaidi na hauzuiliki. Tunapoelewa kuwa tuna talanta (kipaji) ya kipekee ya uandishi tuliyotunukiwa na Mungu, inatusaidia zaidi katika kuandaa makala au hadithi nzuri.

Tunakuwa na ujasiri zaidi pale tunapojikubali na kujijua tulivyo. Tunapojiweka katika mahitaji na tamaa zetu, tunajiweka huru zaidi kutumia vitu kutoka katika maisha yetu wenyewe na maisha ya wale ambao wametuimarisha. Husika zetu zinakuwa imara zaidi tunapojibainisha kwa wote ambao tunawajua katika hali ya kibinadamu.

Hivyo, mwandishi huanzaje? Anza kwa kuangalia kwanza kinachokusukuma kama mwandishi. Ni kipi kinakusukuma zaidi? Baadhi ya waandishi husukumwa zaidi na shauku ya kuandika, wengine husukumwa zaidi na hofu, na hata wengine husukumwa na vyote viwili. Kile tunachokitamani sana mara nyingi pia ndicho tunachokiogopa. Hii hutokea pasipo kufahamu kwa watu wakati wote.

Waandishi wa filamu, kwa mfano, hutamani sana kuuza kazi zao, hutaka kuona kazi zao zikifanikiwa kwa kuoneshwa kwenye “screen” kubwa ndani ya majumba ya sinema na hata kuwa na mapato makubwa kupitia Box Office, lakini wanaweza kuhofia changamoto zinazoambatana na mafanikio ambayo huja kwa kazi hiyo. Ni suala la asili tu kuhofu kile tunachokijua kwa kiasi kidogo. Sisi ni viumbe wenye tabia fulani. Elewa mabadiliko hayaji kirahisi na hii haijalishi hata kama matokeo yake yatakuwa ni ya kuvutia.

Hatari ambayo waandishi wengi wanaikabili ni kule kujiweka kwenye kutarajia matokeo makubwa wakati wakiwa hawajajua ni kwa nini wamechagua kazi ya kuandika.

Yapo maswali kadhaa ambayo kama mwandishi unayopaswa kujiuliza:
- Je, ni lini ulijigundua kwa mara ya kwanza kwamba unataka kuwa mwandishi?
- Ulikuwa wapi?
- Ni nini kilikuongoza kufanya uamuzi wa kuandika?

Tunapojibu maswali haya na kujiweka zaidi katika mahitaji yetu, tunaweza kuanza kutafakari juu ya kile kinachotujenga na kulisha nafsi za uandishi wetu.
Ieleweke. kila mwandishi ana njia yake ya kuandika. Kwa baadhi, ni suala tu la kuendeleza utamaduni wa kuandika, ni kama vile kusugua meno yao kila asubuhi au kula chakula kwa wakati maalum. Kwa wengine, ni suala la umuhimu wa kuumba dunia mpya na kuwa pamoja kama waandishi wengine, haijalishi iwapo ni waandishi marafiki wachache, kikundi au kwenye semina. Ufunguo muhimu wa kutufanya kuandika vizuri ni kujielewa zaidi, nini kinachotusukuma na kipi kinachochochea uandishi wetu.

Uandishi hutegemea sana Ubunifu (Creativity). Ubunifu wa mtu hufanyika kutoka kwenye sehemu mbili. Kwanza kuna Ubunifu wa Awali (Primary Creativity) ambao hutokea kwenye sehemu ya ubongo wa kulia, eneo ambalo ndiyo chanzo cha mawazo/mipango na utambuzi. Ni eneo ambalo msukumo wa mwandishi hutokea na kuchangia asilimia 10 tu ya mchakato mzima wa ubunifu.

Kisha, kuna Ubunifu wa Pili (Secondary Creativity), ambao hutokea kwenye sehemu ya kushoto ya ubongo na huchangia asilimia 90, sehemu ambayo hujumuisha uhariri, nidhamu, mantiki, muundo, mazoea ya kuandika, taratibu na mpangilio.

Ili kuwa mwandishi mbunifu ni kuwa na ujasiri wa kuweza kurudia kumbukumbu zako za utotoni, ambapo ulikuwa huru na hukuwa na msongo wa mawazo au kufikiria sana maisha kama ulivyo sasa. Unapoanza kuandika, ruhusu upande huo wa ubunifu wa asili kujitokeza kupitia maneno yako bila kuyakosoa au kuyachambua maandiko yako.

Kabla hujaanza kupata taswira kichwani mwako (visualization), kwanza tulia, fumba macho yako na jilegeze huku ukivuta pumzi ndefu. Ukipenda unaweza kusikiliza muziki wenye kukubembeleza. Endelea kuvuta pumzi hadi unapohisi misuli ya mwili wako inalegea. Baada ya kulegeza kabisa viungo, pata taswira yako ukiwa mtoto mdogo. Jenga picha yako ukiwa kwenye eneo lenye uoto asili kama vile konde lenye kijani kibichi, kwenye kiwanja cha michezo, porini, au ufukweni mwa bahari.

Unapopata picha, jaribu kuwa sehemu ya tukio ukijumuisha fahamu zako zote. Vuta hewa ya bahari, sikiliza sauti za ndege wakiimba, sikia sauti ya upepo ukivuma kwenye majani, angalia rangi ya maji ya bahari na onja radha ya chumvi ya maji hayo. Endelea kuzama kwenye tukio na jifikirie kuhusu uwepo wako hapo ukijumuisha fahamu zako zote. Je, umevaa nini? Nywele zako zikoje? Uko katika hali gani? Uko peke yako au na rafiki? Chukua muda kidogo na pata picha ya unachokifikiria katika sehemu hii nzuri ya utotoni. Je, una furaha? Huzuni? Mpweke? Unacheza? Uko huru?

Sasa chukua kalamu yako na anza kuandika kuhusu ulichokiona. Tumia nafsi ya kwanza — wakati uliopo. Andika ukijumuisha fahamu zako zote, ielezee picha yote uliyoiona. Usiache kuandika hadi utakapokuwa umeandika kwa dakika ishirini. Usiiondoe kalamu yako kwenye karatasi wakati ukiandika na usisome chochote unachokiandika hadi ukiwa umemaliza. Ni muhimu kwako kuwa huru unapoandika na wala usihofu kuhusu matumizi ya sarufi, herufi au alama za vituo.

Ukikwama au kama huwezi kufikiri chochote kingine cha kuandika, basi andika kuhusu hisia za kukwama na kushindwa kuandika. Haijalishi — usiache kuandika hadi ingalau dakika ishirini zipite. Ukipenda, unaweza kutegesha saa na usiache kuandika hadi utakaposikia mlio. Mtindo huu wa kuandika kuhusu jambo hili bila kufuata muundo wowote au sheria, utakusaidia kutengeneza hadithi nzuri yenye kuleta msisimko zaidi na kumbukumbu zako za nyuma.

Tukutane wiki ijayo.

No comments: