Dec 19, 2012

Urasimishaji sekta ya burudani: TRA inapojitwisha zigo isilolifanyia utafiti kwa lengo la kuongeza pato!


Wasanii wakifuatilia semina ya TRA kwenye ukumbi wa maonesho wa Makumbusho ya Taifa, Jumanne wiki hii

Pia nilikuwepo kwenye semina hiyo, hapa nipo na mdau

NIMEKUWA nikisisitiza kuwa hakuna 'excuse' yoyote kwa wasanii katika kukuza pato lao, kuondokana na umaskini na hata kushindana kimataifa kama hawataingizwa kwenye mfumo rasmi ambao utawafanya watambulike ndani na nje ya nchi ili kujenga mazingira ya wao kuweza kukopesheka, kupata fursa za kikazi na kukuza kazi wanazozifanya. Katika mataifa mengine wasanii wako rasmi na wameweza kuvuma na kupaa kiuchumi.

Lakini pia nimekuwa nikitoa wito kwa serikali kutumia fursa ya kuirasimisha tasnia ya burudani hususani filamu kwa kutuanzishia chombo cha kusaidia maendeleo ya miradi kama sehemu muhimu ya kuifanya sekta hii ifikie tunapopataka, na ni msingi muhimu ambapo mkakati wowote wa utengenezaji wa filamu unapaswa kujengwa.

Badala yake wiki hii tumeshuhudia kioja ninachoweza kukiita cha karne kilichotokea kwenye Semina ya TRA ya urasimishaji wa tasnia ya muziki na filamu, ambayo iliisha kwa kusambaratika bila hata kuagana rasmi kutokana na wasanii kuja juu baada ya maswali waliyouliza kupata majibu ya kisiasa na ya kukatishana tamaa.

Semina hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa maonesho wa Jumba la Makumbusho ya Taifa katikati ya Jiji, kwanza ilichelewa kuanza, badala ya kuanza muda uliotajwa wa saa tatu ilianza saa tano huku wasanii mbalimbali wa filamu na muziki wakiitikia mwito huo.

Upande wa serikali kulikuweko na Maafisa kutoka Kurugenzi ya Utamaduni ya Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Basata, Cosota, Bodi ya Filamu na TRA, ambao ndio walikuwa wasemaji wakuu. Semina ilianza kwa maelekezo kuhusu nini kitakachofanyika ili kuanza kuhakikisha stempu za TRA zimebandikwa kwenye kila kazi ya sanaa.

Kama ambavyo imeanza kutangazwa kuwa kuanzia Januari 2013, kazi zote mpya na ambazo ziko dukani zitatakiwa kuwa na stika hizo kufikia July 2013. Kazi zote zilizotakiwa kusambazwa nchini kuanzia sasa, zingelazimika kwanza kupitia Cosota, kisha Basata (kwa muziki), au Bodi ya filamu (kwa filamu) kabla ya kuruhusiwa kupewa stempu na TRA.

Cosota ndiyo itakayokuwa ikihakikisha uhalali wa kazi, Basata na Bodi ya filamu zitahakiki maadili ya kazi husika na ndipo stempu maalum zitakapotumika kabla hazijaingia sokoni. Kwa kweli ni mfumo mzuri ingawa imegundulika kuwa serikali haina nia njema kwa tasnia ya burudani kama nitakavyoeleza baadaye.

Mpango huu unaodaiwa ni wa kurasimisha sekta hii ili kuiboresha umekuwa na maswali mengi mno bila majibu, hasa kutokana na kile kinachoonekana kuwa upande wa serikali (kupitia taasisi zake) hauelewi upande wa pili unatendaje kazi zake, unataka kuchukua haki ya upande wa pili na kutokana na upya wa dhana yenyewe pande zote hazielewi nini kinatakiwa.

Pamoja na TRA kujidai kuwa wamefanya utafiti wa kutosha kabla ya zoezi zima za urasimishaji lakini ukweli hakuna utafiti wowote wa kitaalam uliofanyika, hasa kutokana na maelezo yaliyowasilishwa na hata majibu ya kukanganya yaliyotolewa na viongozi wa mamlaka hiyo.

Inashangaza sana pale viongozi wa TRA pamoja na kuelezwa ukweli wa matatizo yaliyopo na ambayo hayajapatiwa ufumbuzi kwa miaka mingi sasa kati ya wasanii kwa upande mmoja na taasisi za serikali (Cosota na Bodi ya filamu), lakini waliamua kufunika kombe mwanaharamu apite kwa kutoa majibu mepesi lakini wakisisitiza kuwa wao wanachotaka ni kukusanya kodi tu na hawatarekebisha chochote bali kukazia, masuala mengine hayawahusu!

Ki ukweli wasanii hawana imani kabisa na Cosota na Bodi ya filamu ambayo hata hivyo imebainika kuwa haipo kwa sasa. Sijui inawezekanaje kuwaambia wasanii wapitie kwanza kwenye taasisi ambazo hawaziamini kabla hawajapatiwa stempu?

Wasanii waliiuliza TRA kwanini inadai inawalinda wasanii wakati ni wazi katika hili kazi yake itakuwa ni kukusanya kodi kutoka kwa wasambazaji, jambo ambalo halina tija yoyote kwa wasanii binafsi? Majibu yaliyotolewa yalileta mvurugano kiasi cha kusababisha viongozi wote kuondoka kimyakimya kwa kupitia mlango wa nyuma na kuwaacha wasanii wakiendelea na kikao kisicho rasmi ambacho kilihamia nje na kufikia kutengeneza kamati ambayo itatayarisha mkutano mkubwa wa wasanii wote wa muziki na filamu kutoa tamko la pamoja.

Sielewi ni kwanini serikali imekuwa ikidharau tafiti zinazofanywa na wadau mbalimbali zinazoegemea kwenye hali halisi, tafiti ambazo zimekuwa zinakuja na muarobaini wa kutatua mambo. Mimi pia nimewahi kufanya utafiti kuhusiana na filamu ikiwemo urasimishaji, nikagusia mfumo unaotumika Afrika Kusini ambao ungetufaa sana.

Tatizo la serikali yetu limekuja pale wanapotaka kutumia utaratibu mpya kabisa ambao haujawahi kufanyika nchi nyingine yoyote, utaratibu usioeleweka na usiofanyiwa utafiti, sijui kwanini serikali inataka kugundua njia hiyo mpya ambayo mchambuzi mmoja anaiita ya ‘kibongobongo’ ili kulinda kazi za wasanii, wakati duniani kote taratibu zinafahamika? Hii maana yake nini? Kwamba serikali inahitaji kodi tu kutoka kwa wasanii lakini haina mpango wa dhati kuhusu wasanii. Kwangu hili halina ubishi.

Bila hata haya kiongozi wa TRA anasimama mbele ya wasanii na kusema kuwa wamefanya utafiti na kugundua kuwa wasanii wa Nigeria ni matajiri na sekta yao ni tajiri kwa kupitia njia hii wanayotaka kuifanya! Hivi ni utafiti upi alioufanya na kwa Nigeria ipi? Labda nyingine lakini si hii ninayoijua ambayo tasnia yake ya filamu inajulikaana kama Nollywood.

Nollywood imekufa! Imekufa kwa sababu ya viongozi waliopewa dhamana ya kuilinda na kulinda maadili kujiingiza katika kukusanya mapato kibao bila hata kujali itaathiri vipi soko la filamu la nchi hiyo. Fikiria, kwa sekta ya filamu iliyokuwa inatengeneza sinema mia moja kila mwezi katika siku za nyuma, hivi sasa haiwezi hata kutengeneza sinema saba katika mwezi! Hapa lazima kuna tatizo kubwa; 7/100!  Hakika huko ni kushindwa!

Nollywood kumebakia watu wachache kama Desmond Elliot, Uche Jumbo, Monalisa Chinda, Stephanie Okereke, Emem Isong na wengine wachache wanaojaribu kutoa sinema. Wao wanajaribu kupambana kama mtu mmoja mmoja. Pia ieleweke kuwa wao ni sehemu ya wasanii tu ambao wanapenda kufanya wakipendacho. Lakini unaweza kuona, wao si watayarishaji wa filamu, ni waigizaji tu.

Hivyo mwisho wa siku, watayarishaji halisi wa Nollywood hawatoi tena sinema. Kwa yeyote anayefuatilia tasnia ya filamu ya Nigeria atakuwa anajiuliza wako wapi kina Chico Ejiro, Zeb Ejiro, Fred Amata, Paul Obasele, Jetta Amata, Teco Benson, Fidelis Duker na wengine? Tujiulize, kwa nini Nollywood imesimama? Kwa nini haifanyi tena sinema katika Lagos? Hata Idumota au Ebinpejo Lane hazisikiki tena katika ulimwengu wa filamu? Kwa asiyejua, haya ndiyo maeneo maarufu ya Nollywood.

Kiongozi huyu wa TRA utafiti huo kaufanyia wapi? Pia kwa kiongozi mwandamizi wa TRA kusema kuwa mamlaka haitajali hata kama kazi za sanaa zitatumiwa ovyo bila makubaliano ili mradi tu ziwe na stempu ya TRA inaashiria nini? Hebu jaribu kutembelea mitaa ya Kariakoo, jijini Dar es Salaam, nyakati za mchana utakuta vijana wengi wameketi na kompyuta zao juu ya meza wakirudufu kazi za wasanii mbalimbali, wa sasa na wa enzi hizo, bila hofu yoyote. Hili TRA inasema ruksa ili mradi tu wawe na kazi zenye stempu ya TRA! Hivi hapa kuna urasimishaji kweli au wanataka kodi tu ili wafikie lengo walilowekewa na Rais linaloanzia 2013?

Mbali na Kariakoo, shughuli hizi zimekuwa zinafanyika karibu kila mahali jijini Dar es Salaam na katika miji mingine ya Tanzania. Wala huhitaji kutumia nguvu nyingi kuwatafuta na kuwakamata watu hawa. Wanaonekana kabisa tena mchana kweupe! Lakini inasikitisha pale TRA wanapodai haliwahusu! Hata taasisi inayohusika (Cosota) hawasemi chochote. Tukihoji tunaonekana tunalalamika.

Nathubutu kusema kuwa sijawahi kuona mpango mbovu kama huu, halafu bila aibu wanajisifu eti wamekuja na mkakati wa kuisaidia sekta ya burudani. Hapa wanamuongopea nani? Wanashindwa hata kubainisha ni vipi msanii atafaidika na hizi stempu za TRA huku vijana wanaorudufu kazi za msanii wakifanya wizi huu kwa uhuru kabisa na bila bugudha yoyote hadi huo uharamia wao wanaoufanya kuonekana kama ni jambo la kawaida!

Siku zote wasanii wa muziki, maigizo, filamu na tamthilia wamekuwa wakilia ‘njaa’ wakati kazi zao zikiibiwa kirahisi namna hii, Cosota ipo, Basata ipo, TRA wapo na taasisi zingine zipo na hazifanyi chochote kuwanusuru na kadhia hii.

Sitaki kuamini wala kukubaliana na kauli kutoka kwa mdau mmoja aliyeniambia kuwa katika hizi kazi za kiharamia (piracy) kwa kazi za sanaa baadhi ya vigogo na viongozi ndani ya Cosota wanahusika kwa kumiliki mitambo ya kurudufu kazi.

Nauliza tena, kwanini tusijifunze kutoka sekta ya burudani ya Afrika Kusini?

Nawasilisha…

No comments: