Feb 23, 2018

Tutumie filamu na muziki kutangaza utalii

Mlima Kilimanjaro

KATIKA nchi hii kuna maeneo bora ya upigaji picha, kuanzia Tanzania Bara hadi Zanzibar, kuanzia kwenye mlima mrefu hadi kwenye maziwa yenye kina kirefu kabisa katika Bara la Afrika.Tanzania ni nchi ya maajabu na vivutio: mlima mrefu Afrika (Mlima Kilimanjaro), mbuga bora yenye wanyama wa kuvutia duniani ya Serengeti, yenye stori ya wanyama wanaohama kila mwaka na kurejea.

Bila kuzunguka, hebu tutafakari ni kwa namna gani filamu na muziki vimeweza kuitangaza Nigeria? Tuanzie filamu, tasnia yao ya filamu (Nollywood) imeweza kuwatangaza kwa kiasi gani? Tutapata jibu la haraka kwamba taifa hilo limetangazika kwa kiwango ambacho siyo cha kawaida wala cha chini.

Steven Kanumba, enzi za uhai wake

Kama filamu za Nigeria zimeweza kuteka soko la Afrika na dunia kwa kiasi fulani, haiwezi kutufanya tuumize kichwa sana kujua kwamba taifa hilo, limeweza kupata matangazo mengi kupitia maigizo, na zaidi kuvuta watalii kutoka pande mbalimbali za dunia.

Baada ya hapo hebu tujaribu kuwaza, ni kwa kiasi gani kundi la muziki la P-Square limefanikiwa kuifanya Nigeria kuwa taifa linalotajwa mara nyingi na watu mbalimbali duniani kila yanapoibuka mazungumzo au majadiliano ya kukua kwa muziki barani Afrika? Je, tunaweza kuona matunda ya wanamuziki kufanikiwa?

Tangu mwaka 1983, Nigeria ilishaanza kung’ara kimataifa kupitia sanaa. Kuchomoza kwa mwanamuziki Sunny Ade, kisha kampuni kubwa ya muziki duniani ya Island Records kubeba jukumu la kutangaza muziki wa staa huyo, kuanzia albamu yake “Synchro-System” hadi ziara zake, kulifanya watu wa mataifa mbalimbali kuanza kuifuatilia Nigeria.

Ongezea mafanikio ya wanamuziki wa kizazi kipya: 2face Idibia, D’Banj, Davido, Iyanya na wengine wengi. Jumlisha na ukweli kwamba zama hizo hakukuwa na mtandao mkubwa wa mawasiliano kama ilivyo sasa.

Kisha pata jawabu ni kwa kiasi gani, sanaa imeiweka Nigeria kwenye ramani ya dunia. Ukweli kwamba Nollywood imefikia mafanikio makubwa na kushika namba tatu kwa utengenezaji na uuzaji wa filamu duniani kwa sasa baada ya Hollywood, Marekani na Bollywood, India. Kwa kweli Sanaa ni mtaji mkubwa nchini Nigeria.

Bila shaka mpaka hapo, tutakuwa tumeshajiridhisha pasipo shaka kuwa sanaa imechangia ukuaji wa Sekta ya Utalii nchini humo kwa kiasi kikubwa sana.

Mamilioni ya watu huingia Nigeria kila mwaka kwa ajili shughuli mbalimbali za utalii lakini zaidi kuona na kujifunza namna wasanii wa nchi hiyo wanavyofanya sanaa za filamu na muziki.

Kwa kuangalia mfano wa Nigeria, ni wakati sasa kwa mamlaka husika nchini kuamua kwa dhati kabisa kuwawezesha wasanii wa Tanzania kwa maslahi ya Taifa.

Uwekwe mkakati mahsusi wa kuwatambua watayarishaji/ wasanii na kudhamini kazi zao, watengeneze fedha na wasaidiwe kwenda kujitangaza nje ya nchi. Baada ya hapo kutakuwa na matokeo yanayoonekana.

Mfano mdogo tu, aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alimchukua msanii wa filamu nchini, Aunty Ezekiel, walikwenda Marekani kufanya kile ambacho walikisema kuwa ni kuutangaza Utalii wa Tanzania. Ni mfano mzuri endapo unafanywa kwa nia ya dhati kutangaza vivutio vyetu, japo sitaki kuzungumzia suala la kuwepo matumizi mabaya ya fedha za umma.

Ni kwa sababu Tanzania yetu haina utaratibu wa kufuatilia wageni wanaokuja nchini.
Kwa mfano, wakati Kanumba (marehemu Steven Kanumba) alipokuwa anatingisha katika soko la filamu, watu mbalimbali walikuwa wanakuja nchini kutoka mataifa tofauti kufuata filamu za Kanumba na za wasanii wengine, nao walikuwa wanakwenda kuuza.

Kanumba alipofariki dunia, idadi ya watu waliokuja nchini kufuata filamu zake iliongezeka maradufu. Watu walikuwa wengi sana. Hata sasa watu huwa wanakuja lakini si kwa idadi kubwa kama kipindi kile. Wengi wanaokuja sasa mahitaji yao huwa ni filamu za kina JB, Ray, Gabo, Jully Tax na wengine japo siyo sana.

Pia kuchomoza kwa wanamuziki kama Nasibu Abdul (Diamond Platnumz) na ushindani wake na Ali Kiba, kumekuwa na matokeo ya ujio wa wageni wengi, kuja nchini kununua kazi zao (ingawa kimagumashi kwani serikali haipati kitu) na kwenda kuziuza kwao.

Diamond Platnumz
Ali Kiba

Ripoti ya Mtafiti mmoja inathibitisha kuwa wauzaji CD za muziki na filamu, wanabainisha kuwa kuna kundi la watu kutoka Comoro, Sudan, Ethiopia, Uganda, Kenya, Burundi, Rwanda, DRC, Congo Brazzaville na kwingineko mpaka Afrika Magharibi kuja nchini.

Miongoni mwao wapo mpaka ma-DJ ambao mbali na kazi za Diamond na Ali Kiba, hufuatilia za wanamuziki wengine wa hapa nchini ili kwenda kuboresha ladha ya kazi zao.
Kwa mujibu wa mtafiti huyo, mafanikio ya kina Diamond nje ya Tanzania, yamesababisha ujio wa wageni wengi na kufanya biashara ya muziki iende vizuri kila wanapokuja. Wapo wafanyabiashara wanaokuja kununua CD kwa wingi, tena kwa jumla, nao husema wanakwenda kuzirudufu ili wakauze kwenye nchi zao na kupata faida.

Kwa kawaida huanza kuulizia nyimbo za Diamond na Ali Kiba, baadaye hutaka kujua wanamuziki wengine ambao wanafanya vizuri.

Kuna ma-DJ, ambao hutaka mseto wa nyimbo za wasanii wa Tanzania ili wakawarushe katika madisko yao, na inasemekana wanakuja Tanzania kwa sababu wanajua ndiyo nyumbani kwa kina Diamond, Ali Kiba na wengine na hivyo hata muziki wa wasanii hawa unakuwa rahisi kuupata.


Hali hii inaonesha kuwa kama Sekta za Filamu na Muziki zitakuwa rasmi [kwa maana ya rasmi na si kuwekewa stempu za TRA pekee] na kuwekewa utaratibu, inaweza kusababisha utambuzi sahihi wa idadi ya wageni wanaowasili nchini kitalii kwa matilaba ya sanaa na kadhalika.

No comments: