Oct 7, 2015

KAMPENI 2015: U wapi uchumi na utajiri wa wasanii? - 2

Wasanii wa filamu, Anti Ezekiel na Jackline Wolper,
wakiunga mkono siasa za Chadema
Msanii wa vichekesho, Steven Mengere (Steve Nyerere),
katika mikutano ya CCM
WIKI HII nimelazimika kuendeleza mjadala wa ‘uchumi na utajiri wa wasanii’, hasa baada ya baadhi ya wasomaji wangu kunitumia ujumbe kutaka ufafanuzi katika mambo fulanifulani. Hata hivyo, wengi wao wanakubaliana na hoja yangu kwamba sanaa siyo sekta ya kuchezewachezewa, wala haipaswi kupuuzwa hata kidogo na wanasiasa wetu.

Ndiyo maana nasisitiza kuwa ni muhimu wasanii wakawa matajiri kwa ajili ya ukombozi mpana wa vijana katika soko la ajira na mzunguko mzuri wa kiuchumi. Kwanza msanii mwenyewe ni ajira. Akifanikiwa ataweza kuajiri watu ili wamsaidie kufanya kazi zake. Kazi zake zinapoingia sokoni, kuna mnyororo mrefu wa mauzo mpaka kumfikia mnunuzi wa mwisho. 

Hivyo, msanii mwenye mafanikio lazima ataajiri walinzi, madereva, mameneja na watumishi mbalimbali watakaorahisisha kazi zake. Kutokana na tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa msanii mmoja anaweza kutengeneza ajira za watu mpaka 200. Kama wasanii 1000 watafanikiwa kufanya vizuri kibiashara, wanaweza kutengeneza ajira za watu 200,000 na zaidi.

Katika sekta ya uwekezaji, sanaa inapofanikiwa wawekezaji mbalimbali hujitokeza na kujenga majumba ya maonesho, kumbi za burudani na starehe. Upo uwekezaji mpaka wa vyuo vya sanaa kwa sababu sanaa inapolipa, huongeza hitaji la watu kuisomea kwa undani zaidi fani ili waifanye kwa weledi.

Hivyo basi, uwekezaji wa sanaa unaenda sambamba na kutanuka kwa elimu. Kwa msingi huo, mafanikio ya wasanii, yanakuwa na matokeo makubwa kabisa.

Pia kuna uwekezaji wa studio na makampuni ya usambazaji. Inawezekana kampuni ya nje ikatamani kuwekeza kwa msanii wa hapa nchini kama ambavyo makampuni hayo yanavyowekeza kwenye nchi zenye mfumo mzuri wa sanaa.

Tatizo kwa hapa kwetu hakuna kampuni, prodyuza wa muziki au filamu, anayeweza kuja Tanzania kuwekeza kwa sababu soko lake lina giza. Hakuna mwekezaji anayeweza kuingiza uwekezaji wake kwenye mazingira ambayo haoni fursa ya kutengeneza fedha itakayolipa gharama na kumpa faida.

Japo inasemwa kuwa sekta ya filamu ya Tanzania ni sekta inayokua kwa kasi kiasi cha kuwa tishio katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, lakini ukweli ni kwamba hatuwezi kujilinganisha na nchi kama Afrika Kusini, Nigeria au Ghana. Kwa mfano Afrika Kusini, ripoti zinabainisha kuwa zaidi ya asilimia tano ya raia wa nchi hiyo, wameajiriwa kupitia mnyororo wa sanaa. Na hii imetokana na wanasiasa wa nchi hiyo kuhakikisha kuwa nchi ina dira na sera nzuri kuhusu sanaa.

Kwa Nigeria hivi sasa inaonekana kuwa moja ya mataifa makubwa barani Afrika kwa sababu tu sanaa imeweza kuitangaza nchi hiyo. Filamu zao, sekta yao ya filamu (Nollywood), imeweza kuwatangaza kwa kiasi kikubwa mno. Hali hii haikuzuka hivi hivi tu kama ambavyo wanasiasa wetu wanataka kutuaminisha. Ulitengenezwa mkakati madhubuti wa kuhakikisha inapatikana Sera ya Taifa ya Filamu mnamo 1991.

Filamu za Nigeria zimeweza kuteka soko la Afrika na dunia kwa kiasi fulani, kwa hiyo taifa hilo limeweza kupata matangazo mengi kupitia sanaa ya maigizo, na zaidi kuvuta watalii kutoka pande mbalimbali za dunia.

Hata kwenye sekta ya muziki, kwa kiasi kikubwa wanamuziki wa Nigeria wamefanikiwa sana kuifanya Nigeria kuwa taifa linalotajwa mara nyingi na watu mbalimbali duniani kila yanapoibuka mazungumzo au majadiliano ya kukua kwa muziki barani Afrika.

Hakuna ubishi kuwa sanaa (filamu na muziki) imechangia ukuaji wa sekta ya utalii nchini Nigeria kwa kiasi kikubwa sana. Mamilioni ya watu huingia Nigeria kila mwaka kwa ajili ya shughuli mbalimbali za utalii lakini zaidi kuona na kujifunza namna wasanii wa nchi hiyo wanavyofanya sanaa za filamu na muziki.

Nimewahi kusoma machapisho fulani kuhusu Benki ya Dunia kutambua umuhimu wa sanaa na nguvu yake kwa ukombozi wa kiuchumi kwa vijana wenye vipaji na jamii kwa jumla, ambapo Juni 2000 ilifanya kongamano la kujadili njia za kusaidia maendeleo ya muziki kwa nchi sita za Bara la Afrika: Afrika Kusini, Zimbabwe, Ghana, Nigeria, Senegal na Mali.

Ieleweke kuwa nchi hizo zilizotajwa, kutoka mwaka 2000 hadi 2010, kila moja ilikuwa imeshatengeneza wanamuziki ambao, uwezo wao wa kifedha kwa kulinganisha na sarafu ya Tanzania, ni haki kuwaita mabilionea.

Kama Benki ya Dunia inaweza kuwekeza kwenye sanaa Afrika kwa kuamini inaweza kuwa mkombozi wa kiuchumi katika uwanja mpana, ni kwanini Tanzania mpaka leo, hakujawa na dhamira ya dhati ya kuifanya sanaa kuwa sekta rasmi na iweze kutumika katika mageuzi ya kiuchumi?

Hata Ghana, baada ya kongamano la Benki ya Dunia, imefanikiwa kuingiza fedha nyingi katika Pato la Ndani la Taifa kupitia sanaa, hasa baada ya waigizaji na wanamuziki wake kufanikiwa kupenyeza kazi zao katika mataifa mbalimbali duniani. Afrika na nje ya Bara ya Afrika.

Sekta ya sanaa ya Ghana imesaidia kutanuka kwa sekta ya Utalii baada ya wasanii wa nchi hiyo kufanikiwa kutamba kimataifa. Leo hii, nchi hiyo imekuwa ikipokea mamilioni ya wageni ambao wamekuwa wakitembelea vivutio mbalimbali, ikiwemo sanaa lakini sababu kuu ni kwa kuvutiwa na kazi za wasanii na kusoma sanaa ya Afrika.

Kuna kitabu kinachoitwa “Ghana and the World Music Boom”, kilichoandikwa na John Collins, mkufunzi katika Shule ya Sanaa za Maonesho katika Chuo Kikuu cha Ghana, kinaelezea mafanikio ya Ghana kiutalii, baada ya wasanii wa Ghana kufanikiwa kutamba nje ya mipaka ya nchi hiyo.

Ukisoma kitabu hiki utagundua kuwa mwaka 2003, Ghana ilianza kuwa na ingizo kubwa la wageni, hivyo kuinufaisha sekta ya Utalii. Inasemwa kuwa jumla ya watu 550,000 waliingia nchini humo, ikiwa ni mara mbili zaidi ya kabla sanaa haijawa na umaarufu wa kimataifa.

Mwaka 2004, idadi ya watalii ilipanda kwa 100,000 zaidi hadi kufikia 650,000. Na sasa Ghana inapokea mamilioni ya wageni kila mwaka kutokana na mchango mkubwa wa sanaa. Na inatambulika rasmi kwamba sanaa nchini Ghana inawezesha sekta ya Utalii kushika nafasi ya tatu kwa kuingiza fedha za kigeni baada ya dhahabu na mbao.

Nirudi kwenye mada, wanasiasa wetu wangekuwa na dhamira ya dhati kuhusu kuinua sekta ya sanaa na wasanii, ni wazi kwamba Tanzania ingeweza kabisa kufikia hatua nzuri na kuona matokeo ya faida ya sanaa katika Utalii kama wasanii wangefanikiwa.

Wanasiasa wangesaidia kuja na mkakati mzuri na sera madhubuti ya kuhakikisha Mamlaka za Utalii kama Tanapa, Bodi ya Utalii na kadhalika, zina ajenda muhimu yaa kuwawezesha wasanii wa Tanzania, kudhamini kazi zao ili watengeneze fedha na kuwasaidia kwenda kujitangaza nje ya nchi. Baada ya hapo kungekuwa na matokeo yanayoonekana.

Kampeni za mwaka huu zimeshuhudia baadhi ya wanasiasa wakijinadi kuwa serikali zao zitakuwa za viwanda, lakini sina uhakika kama kweli wanayo mikakati na dhamira ya dhati kufufua viwanda, au ni porojo tu za kuombea kura! Nijuavyo, kazi za sanaa zinategemea viwanda kwa utengenezaji wake. Pale wasanii wanapotengeneza fedha, huutafsiri mzunguko wa sanaa kwamba ni mzuri na kwa hivyo, huchagiza mwamko wa sekta ya Viwanda na Biashara.

Wasanii wanapokuwa na fedha ni fursa nzuri kwa wafanyabiashara mbalimbali. Mathalan wenye maduka ya nguo, watauza sana kwa sababu kubadili mwonekano ni sehemu ya sanaa. Lazima msanii abadili mavazi katika maonesho yake kwa lengo la kujipa heshima na thamani zaidi ya kibiashara.

Hata wabunifu wa mavazi ambao pia ni wasanii, wangepata kazi nyingi kwa ajili ya kuwapendezesha wenzao katika sanaa tofauti, hususan waigizaji na wanamuziki.

Pia wasanii wanapokuwa kwenye maonesho yao, wafanyabiashara wa vitu mbalimbali, hujitokeza kuuza chakula, vinywaji, mavazi na hata nakshi za aina tofauti. Hii ni sehemu ya biashara, ingawa inaweza kubeba tafsiri ya soko la ajira kwa upana wake.

No comments: