Jun 11, 2014

Wasanii wanajifunza nini kwenye vifo mfululizo vya wasanii wenzao?

Marehemu Said Ngamba maaruf kwa jina la Mzee Small



KWANZA naomba nianze kwa kutoa pole kwa familia nzima ya wasanii na wadau wa filamu nchini kufuatia vifo mfululizo vya wasanii wa filamu ndani ya wiki tatu; Adam Kuambiana, Rachel Haule, George Otieno “Tyson) na Said Ngamba maarufu kama Mzee Small. Mfululizo wa vifo hivi umeambatana na uvumi au dhana potofu inayosambaa kwa kasi, eti vifo mfululizo vya wasanii vinatokana na kafara inayofanywa na baadhi ya wadau (wasanii) ndani ya tasnia ya filamu kwa lengo fulani lenye maslahi kwao.

Uvumi huu umejitokeza hasa baada ya kushuhudia kundi la watu fulani likiwa ndiyo kinara wa kukumbatia misiba ya wasanii nyota, kuunda kamati mbalimbali na kuchangisha fedha nyingi ambazo baadhi yake zimekuwa zikitumika kununulia majeneza ya bei mbaya, vyakula vya gharama (utadhani kuna sherehe) na shughuli zingine ikiwemo ukodishaji wa magari ya kusindikiza msafara wakati wa mazishi. Lakini kama hiyo haitoshi, kumeripotiwa pia kufanyika kwa ubadhirifu wa pesa.

Sekta ya filamu nchini ni sekta kubwa sana, yenye nguvu kubwa na ushawishi mkubwa mno, lakini ndiyo sekta isiyopewa kipaumbele kama sekta muhimu (kwa kuwa inachukuliwa kama utamaduni na burudani na si biashara) inayoweza kuchangia pato kubwa kwa maendeleo na ukuaji wa uchumi wa taifa letu.

Ikumbukwe kuwa kwa miaka mingi sasa, wasanii na watengenezaji wa sinema miongoni mwa wadau wengine wa sanaa wameendelea kutoa sinema hapa Tanzania ili kujipatia riziki kutokana na kazi yao bila mafanikio. Ingawaje sekta ya filamu ni sekta yenye thamani ya mabilioni ya fedha, lakini wengi wameishi na kufa maskini.

Hali hii ya umasikini kwa wasanii nchini itaendelea kuwa hivi kama wasanii wenyewe hawataonesha mshikamano na kupigania maslahi yao kwa kuwa kuwategemea wanasiasa itakuwa ni ndoto ya alinacha kwani wamekuwa wakiahidi sana hasa katika kipindi cha uchaguzi, lakini wakishapata huwapa visogo. Haki za wasanii na watayarishaji wa filamu zitaendelea kuporwa, kwa kutumia unyonge wao na umasikini wao wataendelea kutumika kwa maslahi ya wachache, na mwishowe watakufa wakiwa masikini lakini wenye majina makubwa, tena bila hata kuwaachia wategemezi wao urithi unaoeleweka.

Nimekuwa nikiandika sana kuhusu suala hili, na niliwahi kuwaandikia Rais Kikwete na Waziri mwenye dhamana wakati fulani kuwataka waiokoe tasnia hii kwa serikali kuelekeza nguvu nyingi katika suala la utoaji wa mafunzo kwa wasanii na watengeneza filamu. Lakini baada ya kuona kuwa sekta ya filamu si moja ya vipaumbele vya serikali nikawahimiza wasanii kupigania uwepo wa sera ya filamu (kama mwongozo).

Kama nchi, tunahitaji sekta hii ichukuliwe kama sekta nyeti sana kupitia kamati za mipango, na Bunge la Jamhuri. Tunahitaji Rais, Mawaziri, Wabunge, na Wakuu wa Idara ambao hawataishia tu kusifia kazi zetu kwenye hotuba zao, kuuza sura kwenye misiba yetu tunapokufa na kutoa ahadi ambazo wanajua kabisa hawawezi kuzitekeleza.

Bado naamini kuwa Serikali kama kweli wameazimia kwa dhati kusaidia tasnia ya filamu, inapaswa kuandaa mwongozo (roadmap) utakaotuongoza kwenye mafanikio ya soko letu. Tunahitaji kuwa na vyombo madhubuti katika kusimamia kazi zetu.

Inashangaza sana kuona kwenye nchi za wenzetu jinsi wasanii wanavyoweza kutengeneza pesa nyingi hata pale msanii anapokuwa amefariki dunia, hii ni kutokana na nchi hizo kuwa na sera nzuri na sheria nzuri za miliki bunifu na hakimiliki, huku serikali ikiithamini sekta ya filamu na kuwasimamia watu wake na viongozi kutimiza wajibu wao ipasavyo.

Chukuliwa wasanii kama Kurt Cobain, Elvis Presley, Charles M. Schulz, John Lennon, Albert Einstein, Andy Warhol, Dr. Seuss (Theodor Geisel), Ray Charles, Marilyn Monroe, Johnny Cash, J.R.R. Tolkien, George Harrison, Bob Marley, Michael Jackson, Whitney Huston na wengine wengi, ambao wamekuwa wakivuna mapesa hata baada ya vifo vyao na hivyo kuwafanya wategemezi wao kuendelea kujipatia pesa kupitia kazi zilizoachwa na wapendwa wao.

Hapa kwetu, chukulia mfano wa aliyekuwa msanii nguli, Steven Kanumba, hadi mauti yanamfika alishatoa zaidi ya filamu 40, je, sinema zake zimeisaidiaje familia yake iliyobaki? Hadi leo wategemezi wake, akiwemo mama yake “wanalia njaa” huku tukiambiwa kuwa kazi alizoacha kanumba zinaendelea kufanya vizuri sokoni.

Naamini kwa mtu aliyefanya kazi nzuri, kufariki siyo mwisho. Anaweza kuendelea kuishi hata baada ya kifo, kwani kazi zake, pamoja na nembo zake zinaweza kuendelea kuvuna mashabiki ambao wanamkumbuka, na wale waliozaliwa muda mrefu baada ya kufa, na kuingiza mapesa kibao kama inavyotokea kwa mastaa niliowataja hapo juu.

Wasanii katika nchi za wenzetu waliofariki miaka mingi sana iliyopita wameendelea kuchuma mamilioni ya dola. Wameendelea kukusanya fedha katika mikataba mbalimbali waliyoingia enzi za uhai wao ikishirikisha vyote; kazi zao na haki za kutumia majina yao kibiashara na kampeni za masoko.

Vipi kuhusu wasanii wa Tanzania? Wana mpango gani kuhakikisha yanawekwa mazingira mazuri yatakayowahakikishia wategemezi wao baada ya vifo vyao? Wanatumiaje nguvu ya sekta ya filamu kuibana Serikali ili iweke mipango na mazingira mazuri yatakayowahakikisha wasanii waliopo na waliofariki kuendelea kuvuna pesa na kuzifaidisha familia zao na wategemezi wao waliobakia? Au ndo’ ule msemo wetu wa ‘Asiyekuwepo na lake halipo?’.

Watengezaji wa filamu nchini wamekuwa wanalalamika kila mara kuwa wanaibiwa au kuwekewa masharti magumu na wasambazaji ambayo yanadumaza tasnia ya filamu ikiwemo kuuza haki zao, lakini wamekuwa wakionekana wendawazimu.

Kwa sasa imekuwa ni jambo la kawaida kusikia kuwa mtayarishaji wa filamu kauza kazi zake kwa msambazaji, jambo linaloshangaza sana hasa kwa nchi kama hii inayoanza kupiga hatua katika tasnia ya filamu. Sababu za kushangaza ni nyingi; ya kwanza kubwa ni kuwa majukumu ya msambazaji yanajulikana wazi kuwa yeye kazi yake inapaswa kuishia kwenye kusambaza kazi husika tu, sasa anaponunua haki zote ndipo inapotia shaka kubwa! Kwa nini anunue haki ya msanii? Kwa nini msanii amuuzie haki yake? Je, wasanii wanalitafakari jambo hili?

Hakuna jambo kubwa kama kujifunza kwa waliotutangulia, hasa kwa kuangalia makosa waliyoyafanya ili sisi tusije tukayarudia. Mfano marehemu Kanumba alikuwa mmoja wa wasanii waliojiona ni washindi kwa kuingia mikataba inayowafanya kuuza haki zao kwa msambazaji na kuishia kupewa gari na pesa zinazowasaidia kwa miezi michache, masikini hakujua kabisa kuwa atakapoaga dunia haki yake itakuwa imeishia hapohapo. Hivyo, hawa waliobaki wanapaswa kujifunza kupitia wasanii kama Kanumba na wengine walioaga dunia.

Sheria ya Hakimiliki ya nchi yetu inasema wazi kuwa hakimiliki hudumu kwa mwenye haki kwa maisha yake yote na miaka hamsini baada ya kifo chake. Kwa nchi kama Marekani wameongeza hadi miaka sabini. Ndiyo maana utaona kuwa kuna kazi nyingi ambazo zinaendelea kuwa maarufu miaka mingi baada ya wenye kazi kufariki, huku zikiwanufaisha warithi wao.

Kwa kawaida kazi za filamu (kama ilivyo kwenye muziki) zina haki zipatazo kumi ambazo zimetajwa katika kifungu na 9(1) cha Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ya 1999.

Haki hizo ni: (i) Kurudufu kazi, (ii) Kusambaza kazi, (iii) Kukodisha, (iv) Kuonesha hadharani, (v) Kutafsiri, (vi) Kubadili matumizi ya kazi, (vii) Kufanya maonesho ya hadhara, (viii) Kutangaza kazi katika vyombo vya utangazaji, (ix) Kutangaza kwa njia nyingine zozote, na (x) Kuingiza kazi nchini.

Kwa hiyo ukiangalia haki hizo kama zilivyoainishwa utaona wazi kuwa msambazaji anahitaji haki mbili tu za mwanzo, haki nyingine zinamruhusu mwenye mali (mtayarishaji) aendelee kufaidi matunda ya kazi yake kwa maisha yake yote na kuwaachia warithi wake miaka hamsini mingine baada ya kifo chake.

Inapotokea ukauza haki zako kwa msambazaji basi ujue unauza hata zile haki nane zilizobakia ambazo kimsingi huwezi tena kuzitumia, kwa kuwa tayari utakuwa umeshazipoteza. Hivi ukiamua kuuza kazi zako kwa maana ya kumuachia haki zote msambazaji, unatarajia kuwaachia nini warithi wako, au unataka kubaki na ile sifa tu ya kuwa uliwahi kuwa na kazi?

Hivyo, badala ya kuanza kutafuta mchawi kwa vifo vya wenzao, nadhani wasanii wangetumia nafasi hii kujitafakari upya hasa katika kupigania umoja wenye nguvu kwa ajili ya maslahi yao, ya sasa na ya baadaye, hasa baada ya kifo.

Alamsiki.

1 comment:

MOHAMMED AL BALUSHI said...

HAKIKA NDUGU UMESEMA NI JAMBO MUHIMU WASANI WAJIPANGE NA HATA KUANZISHA COMPANY YA USAMBAZAJI BADALA YA KUTUMIA PESA ZAO KWENYE MAMBO YASIYO NA MAANA KAMA HARUSI MILION 70 HII FAIDA GANI NI MUHIMU KUANZISHA COMPANY YA USAMBAZAJI WENYEWE MAANA WANA SIASA WOTE DUNIANI HUANGALIA MASLHAI YAO NASIYO VINGINEVYO