Nov 11, 2013

KWA KUANDAA MAFUNZO: Wasanii mkoani Iringa wanapaswa kuigwa


Mmoja wa wasanii mjini Iringa akikabidhiwa cheti cha kuhitimu mafunzo na Rais wa TAFF, Simon Mwakifwamba

ILIONEKANA kama masikhara, wengi waliwabeza, hata rafiki zao waliona kuwa walichokuwa wakikifanya ulikuwa ni upuuzi mtupu. Hatimaye siku zikaanza kujongea taratibu, mara wiki, mbili, hadi ukatimia mwezi tangu waanze kuchukua mafunzo yaliyobeba dhana nzima ya kujitambua, kujifunza misingi ya uigizaji, uandishi, uongozaji na utayarishaji wa filamu.

Mafunzo haya ya mwezi mmoja yaliandaliwa na Taasisi Isiyo ya Kiserikali ya Tanganyika Center for Development and Advocacy (TCDA) ya mjini Iringa na kufadhiliwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF), Fredrick Mwakalebela. Taasisi hii ni matokeo ya vijana wawili waliomaliza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika fani tofauti na kukumbana na changamoto za ajira baada ya kurudi mtaani. Moja ya malengo ya Taasisi hii ni kuwaelimisha vijana umuhimu wa kujiajiri kwa kutumia fursa zilizopo.

Walianza kwa kuwakusanya vijana kutoka kwenye vikundi vya sanaa vilivyoonekana kama ni vya vijana waliokosa kazi ambao hukutana katika kumbi mbalimbali kufanya mazoezi kidogo na kupiga porojo pasipo manufaa yoyote.

Wasanii wa Iringa walipopata taarifa njema kuhusu ujio wa mafunzo hayo, waliamua kuchangamkia fursa hiyo, japo wengi waliwabeza.

Ilionekana kama ni vijana wenye ndoto za alinacha, wanaotaraji makubwa wakati uwezo huo hawana, lakini mwisho wake, waliocheka sasa wanatamani fursa kama hiyo iwashukie wao pia. Hatimaye mafunzo yalifungwa na Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF) kwa kutoa vyeti maalum vinavyotambuliwa na Shirikisho hilo.

Vijana na wasanii hawa wa Iringa ni kama walishaliona tatizo kubwa katika filamu zetu la kukosa watu wenye weledi nchini wasio na mafunzo ya msingi (nitty-gritty) ya namna ya kutengeneza au kuongoza kazi zao katika kiwango kinachokubalika ambacho kinaweza kuwasaidia kuzifanya sinema zao angalau zifikie kiwango chenye kuridhisha, tangu wakati huo wakaanza kuonesha nia thabiti ya kuhitaji mafunzo miongoni mwao ili waweze kujikosoa wenyewe kabla ya kukosolewa na wengine.

Mafunzo haya yaliendeshwa na vijana wawili wanataaluma kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano (IJMC). Baada ya kumaliza mafunzo hayo, vijana hawa sasa wanahitaji mafunzo ya kina zaidi katika fani mbalimbali zikiwemo uandishi wa miongozo ya filamu, uongozaji, utayarishaji wa filamu, uigizaji na fani zingine. Na wanasema kuwa wako tayari kulipia gharama za mafunzo hayo.

Ndiyo maana ninasema kuwa vijana hawa wa Iringa wanapaswa kuigwa na wadau wote wanaopenda maendeleo ya sanaa. Wanapaswa kuungwa mkono kwani kumekuwepo changamoto kubwa ya kubezwa, kutelekezwa, kutoungwa mkono na watu waliopaswa kuwasapoti. Kiukweli kwa sisi wenye kupenda maendeleo ya sanaa, vijana hawa wanatia moyo sana na wanaweza kuifikisha mbali tasnia hii ya filamu.

Inaaminika kuwa kukosekana kwa mafunzo na kutojielewa ni sababu kubwa ya filamu zetu kuwa ni kitu kisichozingatia au kuhitaji taaluma yoyote. Wengi wamekuwa wanalipua kazi na wanafanya mambo bila kuzingatia utaalam kwa kuwa tu hawajitambui. Wanafanya mambo ili mradi wanajua watauza na kupata pesa, basi. Hali hii imekuwa ikiwakatisha tamaa hata wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika tasnia hii.

Pia kukosa mafunzo kumewafanya walio wengi kujawa na ubinafsi (kwa kuwa hawajiamini) ambao umekuwa ni sababu kuu ya kuufanya uwanja wa filamu wa Tanzania kuwa ni sehemu inayoongoza kwa kutokuwa na mgawanyo wa majukumu. Si ajabu kuona mkurugenzi wa kampuni ya kutengeneza filamu, ndiye aliyeandika skripti, ndiye muongozaji mkuu, ndiye muigizaji mkuu na kadhalika! Na mwisho wa siku hawapendi kukosolewa.

Siku za karibuni nilikuwa na kikao na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Prof. Elisante ole Gabriel, aliyetuita viongozi wa Shirikisho la Filamu Tanzania ili tujadili changamoto zilizopo zinazopaswa kufanyiwa kazi.

Niliiomba Serikali kuwa, kama kweli wamedhamiria kutusaidia basi wanapaswa kuanzisha mpango maalum wa mafunzo kwa wasanii na watendaji wengine wakiwemo waandishi wa miongozo, waongozaji, wapiga picha, wahariri na wengineo kama uliopo nchini Afrika Kusini kupitia taasisi yao ya National Film and Video Foundation (NFVF), mpango unaoweza kuwasaidia wajasiriamali katika tasnia ya filamu nchini kutengeneza kazi nzuri zitakazokidhi ubora wa soko letu na hata nje ya mipaka yetu.

Kwa mpango huu wa wasanii wa Iringa kuamua kuchangamkia mafunzo wakishirikiana na Taasisi ya TCDA itasaidia sana kuwaongezea ufahamu na kujitambua, kitendo ninachoamini kitapunguza matatizo ya filamu zetu ambazo si ajabu kumuona mwigizaji akiigiza analia lakini uso wake umebeba tabasamu la chati kama ambavyo msomaji mmoja aliwahi kuniomba nitoe ufafanuzi. Au yale matukio ya utekaji nyara katika filamu huku mtekwaji akionesha dalili zote za kukaa tayari kwa kutekwa!

Kwa kuwa nilibahatika kukutana na wasanii hawa siku ya kuhitimu kwao, niliombwa niseme nao maneno machache kama usia wangu kwao, nami niliwaeleza wazi kuwa wasivunjike moyo kwani jambo waliloamua kulifanya lina changamoto zake, wasitarajie njia ya mkato kuwafikisha kwenye mafanikio bali wanahitaji kufanya maamuzi magumu kwenye baadhi ya mambo ili kufikia mafanikio.

Niliwapa moyo kuwa wasijione wanyonge kwa kukosa elimu ya darasani, kwani kuna njia nyingi za kupata mafunzo ikiwemo njia waliyoitumia wao, ambayo naamini kama watayazingatia waliyofundishwa yatawasaidia mno katika kazi zao. Kukosa elimu ya darasani si mwisho wa kujifundisha, kwani hata Hollywood kuna waigizaji na waongozaji ambao hawakupata elimu rasmi katika vyuo vya filamu lakini wameweza kuwa waongozaji wazuri na wanaoheshimika sana duniani.

Waongozaji hao ni pamoja na; Steven Soderbergh, Robert Rodriguez, Quentin Tarantino, Richard Linklater, Spike Jonze...

Kwa njia kama hizi nakubaliana na mwalimu wangu, Dk. Urassa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Shule ya Biashara (UDBS) kuwa ili ufanikiwe unahitaji kupitia kipindi kigumu chenye changamoto. Mwalimu huyu aliwahi kunisimulia kisa cha ndege tai (the story of the eagle).

Tai ni ndege anayeishi maisha marefu kuliko ndege wengine wa aina yake. Lakini ili kufikia umri huo anatakiwa kuchukua maamuzi magumu. Ana uwezo wa kuishi hadi miaka 70. Kwa kawaida akifikia umri wa miaka 40 makucha yake hurefuka na kupinda na hivyo hayawezi tena kunyakuwa au kubeba chakula. Mdomo wake huota gamba gumu na kupinda, mabawa yake huota manyoya mengi na kuwa mazito, hunasia kwenye kifua chake na kumpa ugumu wa kuruka. Sasa anapofikia hatua hii huwa ana njia mbili za kufanya; asubiri kufa au afanye maamuzi magumu kwa kupitia kipindi kigumu chenye mateso kwa siku 150.

Kipindi hiki hukitumia kwenda milimani na kukaa kwenye kiota chake, hapo hugonga mdomo wake kwenye miamba au kitu kigumu hadi gamba lililoota litoke. Baada ya kutoka tai husubiri hadi gamba jipya liote kisha ataanza mchakato wa kuhakikisha anagonga magamba yaliyoota kwenye kucha zake hadi yatoke, baada ya kucha mpya kuota ataanza mchakato wa kuhakikisha anapiga mbawa zake kwenye miti na miamba hadi manyoya ya uzeeni yapukutike.

Miezi mitano baada ya kupita kipindi hiki kigumu tai huwa amezaliwa upya na huwa ana nafasi ya kuishi miaka mingine 30. kisa hiki kinatufundisha kuwa ili kufanikiwa tunapaswa kuwa tayari kwa mabadiliko, mabadiliko ambayo hayaji kirahisi kama tunavyotarajia. Tunahitaji wakati mwingine kuachana na mambo ya kufanya kazi “kibongobongo”, tuachane na kufanya kazi kwa mazoea na kuchangamkia fursa zilizopo.

Wasanii wa Iringa kama watakuwa na uelewa wa kina wa jinsi sinema inavyotengenezwa, kuwa na ubunifu mkubwa (creative vision), ufahamu wa namna ya kuandika miongozo ya filamu na kujitoa kwa dhati (commitment) katika kufanikisha kazi nzima huku wakikubali kupitia kipindi kigumu cha mabadiliko ya kweli, naamini watafanikiwa mno.

Ni matumaini yangu kuwa wasanii hawa wa Iringa waliohudhuria mafunzo haya ya mwezi mzima watakuwa wamepata msingi mzuri sana na kuwa mfano mzuri kwa wale waliokuwa wakiwabeza au ambao hawakupata fursa kama hii muhimu popote nchini, na ninaamini kuwa wataendeleza yale mazuri waliyofundishwa na wakufunzi wao.

Sitegemei kuwaona wakirudia makosa yaleyele hata baada ya kupata ufahamu kuhusu utayarishaji wa filamu.

Alamsiki...

No comments: