Apr 22, 2015

Tunahitaji mapinduzi ya kweli ya sekta ya filamu Tanzania

Simon Mwakifwamba, Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania
Dilesh Solanki, Mkurugenzi wa Kampuni ya Steps Entertainment
HALI ya tasnia ya filamu nchini kwa sasa inakatisha tamaa, wasanii na viongozi wao wengi wamefikia ukomo wa kufikiri, wanaonekana kuridhika na hali ilivyo au pengine wamekata tamaa, ingawa bado wana nafasi kubwa ya kufanya vizuri zaidi. Vyombo vya kuwasimamia, likiwemo Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), vimekosa dira.

Ni wasanii wenyewe kupitia chombo chao, ndiyo wamesababisha sekta hii ishuke kutokana na tabia zao, hii inawagusa wasanii wote, wanawake na wanaume. Wamechukulia kada hii kama sehemu ya kujitangaza zaidi kuliko kazi, viongozi wao wanachukulia nafasi zao kama fursa ya kuwakutanisha na wakubwa au matajiri ili wapige vibomu, ilimradi siku ziende.