Kazi za utengenezaji sinema kama hizi zinahitaji nidhamu
na maadili ya taaluma kama ilivyo kwa taaluma nyingine.
TAKRIBANI mwezi mmoja tu kuanzia sasa, nchi yetu itasherehekea miaka hamsini tangu tujipatie uhuru kutoka kwa wakoloni wa Kiingereza. Baada ya uhuru wa Tanganyika serikali katika kuthamini sanaa na utamaduni ilianzisha Wizara ya Utamaduni wa Taifa na Vijana iliyoundwa mwaka 1962, na rais wa Tanganyika na baadaye Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alitamka wazi kuwa Utamaduni ndiyo kiini na roho ya Taifa.
Katika jitihada zake, nchi yetu ilipata kusifiwa sana kwa jitihada hizo za kushughulikia ukuzaji wa utamaduni katika duru nyingi za kimataifa. Hata hivyo, wakati tukiwa tunajiandaa kusherehekea miaka hii hamsini tangu uhuru, hali ilivyo sasa inatisha na kama hatua za dhati hazitachukuliwa, kazi iliyofanywa miaka ya nyuma, hasa mara baada ya uhuru na miaka takriban 20 iliyofuata, itapotea na tutajikuta tukiwa taifa lisilo na utamaduni wake.